MAKALA YA 38
WIMBO 120 Igeni Upole wa Kristo
Waonyeshe Heshima Wengine
“Kuheshimiwa ni bora kuliko fedha na dhahabu.”—MET. 22:1.
JAMBO KUU
Jifunze kwa nini tunahitaji kuwaonyesha heshima wengine na jinsi tunavyoweza kufanya hivyo chini ya hali ngumu.
1. Kwa nini wanadamu wanafurahi wanapoonyeshwa heshima? (Methali 22:1)
JE, WEWE hufurahi wengine wanapokuonyesha heshima? Bila shaka unafurahi. Kuheshimiwa ni uhitaji wa msingi wa wanadamu. Tunahisi vizuri tunapoheshimiwa. Haishangazi kuwa Biblia inasema kwamba “kuheshimiwa ni bora kuliko fedha na dhahabu”!—Soma Methali 22:1.
2-3. Kwa nini si rahisi sikuzote kuwaonyesha wengine heshima, na tutachunguza nini katika makala hii?
2 Huenda isiwe rahisi sikuzote kwetu kuwaonyesha wengine heshima. Sababu moja ni kwamba ni rahisi kwetu kuona udhaifu wa wale wanaotuzunguka. Pia, tunaishi katika kipindi cha wakati ambapo ni kawaida kwa watu kutokuwa na heshima. Lakini sisi tunapaswa kuwa tofauti. Kwa nini? Kwa sababu Yehova anataka tuwaheshimu “watu wa namna zote.”—1 Pet. 2:17.
3 Katika makala hii, tutachunguza kinachomaanishwa na kuwaheshimu wengine na jinsi tunavyoweza kuwaonyesha heshima (1) watu wa familia, (2) waabudu wenzetu, na (3) watu walio nje ya kutaniko. Tutakazia fikira jinsi tunavyoweza kuonyesha heshima chini ya hali ngumu.
KUWAHESHIMU WENGINE KUNAMAANISHA NINI?
4. Kuwaheshimu wengine kunamaanisha nini?
4 Ungefafanuaje neno heshima? Neno heshima linarejelea mtazamo wetu kumwelekea mtu na jinsi tunavyomtendea. Tunapowaheshimu wengine tunawaona kuwa wanastahili uangalifu na ufikirio wetu, huenda kwa sababu ya sifa zao, mambo waliyotimiza, au mamlaka waliyo nayo. Pia, tunawaonyesha wengine heshima kwa kuwatendea kwa njia ambazo watahisi wanathaminiwa na kuonyeshwa staha. Na bila shaka, ni muhimu tufanye hivyo kutoka moyoni.—Mt. 15:8.
5. Ni jambo gani linaloweza kutusaidia kuwaonyesha wengine heshima?
5 Yehova anataka tuwaonyeshe heshima wengine. Kwa mfano, anataka tuziheshimu “mamlaka zilizo kubwa.” (Rom. 13:1, 7) Lakini huenda baadhi ya watu wakasema, “Niko tayari kuwaonyesha heshima wengine, maadamu wanastahili.” Je, njia hiyo ya kufikiri inafaa? Tukiwa watumishi wa Yehova, tunatambua kwamba heshima yoyote tunayowaonyesha watu haipaswi kutegemea tu matendo yao. Inategemea jambo kubwa zaidi—upendo wetu kwa Yehova na tamaa yetu ya kumfurahisha.—Yos. 4:14; 1 Pet. 3:15.
6. Je, inawezekana kumheshimu mtu ambaye hakuonyeshi heshima? Eleza. (Tazama pia picha.)
6 Huenda baadhi ya watu wakajiuliza hivi: ‘Je, kweli inawezekana kumheshimu mtu ambaye hakuonyeshi heshima?’ Ndiyo, inawezekana. Fikiria mifano ifuatayo. Mfalme Sauli alimwaibisha Yonathani, mwana wake, mbele ya watu wengine. (1 Sam. 20:30-34) Hata hivyo, kwa heshima Yonathani alimtegemeza baba yake vitani hadi siku Sauli alipokufa. (Kut. 20:12; 2 Sam. 1:23) Kuhani Mkuu Eli alimshutumu Hana kwamba alikuwa amelewa. (1 Sam. 1:12-14) Licha ya hilo, Hana alizungumza kwa heshima na Eli, ingawa ilijulikana katika Israeli yote kwamba hakutimiza vizuri majukumu yake akiwa baba na kuhani mkuu. (1 Sam. 1:15-18; 2:22-24) Na wanaume wa Athene walimtukana mtume Paulo, wakimwita “mpigadomo.” (Mdo. 17:18) Licha ya hilo, Paulo alizungumza nao kwa heshima. (Mdo. 17:22) Inapaswa ionekane wazi kwamba upendo wetu wenye kina kwa Yehova na tamaa yetu ya kumpendeza inatuchochea kuwaonyesha heshima wengine, si tu inapokuwa rahisi, bali pia inapokuwa vigumu kufanya hivyo. Acheni tuchunguze tunapaswa kumwonyesha heshima nani na kwa nini.
Ingawa baba yake alimwaibisha, Yonathani aliendelea kumtetea na kumuunga mkono baba yake akiwa mfalme (Tazama fungu la 6)
WAONYESHE HESHIMA WATU WA FAMILIA
7. Ni nini kinachoweza kufanya iwe vigumu kwetu kuwatendea kwa heshima watu wa familia?
7 Changamoto. Tunatumia wakati mwingi na watu wetu wa familia. Matokeo ni kwamba tunajua sifa zao nzuri na udhaifu wao. Huenda baadhi yao wana ugonjwa unaofanya iwe vigumu kwetu kuwatunza, au huenda wana ugonjwa wa kuwa na wasiwasi kupita kiasi. Wengine wanaweza hata kusema na kutenda kwa njia ambazo zinatuumiza. Badala ya kujitahidi kufanya nyumba zao ziwe mahali penye utulivu na amani, baadhi ya watu husababisha vurugu kwa kutowatendea kwa heshima watu wa familia. Matokeo ni kwamba hakuna upatano katika familia. Kama ugonjwa wa yabisi kavu unavyozuia sehemu za mwili kufanya kazi pamoja vizuri, ukosefu wa heshima huzuia watu wa familia kufanya kazi pamoja kwa umoja. Lakini tofauti na ugonjwa wa yabisi kavu ambao sisi wenyewe hatuwezi kuutibu kikamili, tunaweza kuzuia ukosefu wa heshima uharibu uhusiano mzuri tulio nao na watu wa familia.
8. Kwa nini ni muhimu kuwaonyesha heshima watu wa familia? (1 Timotheo 5:4, 8)
8 Kwa nini uonyeshe heshima? (Soma 1 Timotheo 5:4, 8.) Katika barua yake ya kwanza kwa Timotheo, Paulo alizungumzia jinsi watu wa familia wanavyopaswa kushughulikia mahitaji ya watu wao wa familia. Alifafanua kwamba jambo kuu linalopaswa kutuchochea kuwaheshimu watu wa familia kwa njia hiyo ni “ujitoaji-kimungu,” na si kutimiza tu wajibu. Ujitoaji-kimungu unarejelea kumwabudu na kumtumikia Mungu kwa ushikamanifu. Yehova ndiye mwanzilishi wa mpango wa familia. (Efe. 3:14, 15) Hivyo, tunapomheshimu mtu wa familia, kimsingi tunamheshimu Yehova, Mwanzilishi wa familia. (1 Tim. 5:4) Hiyo ni sababu muhimu sana ya kuwaonyesha watu wa familia heshima!
9. Wenzi wa ndoa wanawezaje kuonyeshana heshima? (Tazama pia picha.)
9 Jinsi ya kuonyesha heshima. Mume anayemheshimu mke wake anaonyesha kwamba mke wake ni mwenye thamani kwake iwe wako mbele za watu au peke yao. (Met. 31:28; 1 Pet. 3:7) Kamwe hatampiga, kumwaibisha, au kufanya ahisi kwamba hana thamani. Ndugu anayeitwa Ariel,a anayeishi nchini Argentina, anasema hivi: “Kwa sababu ya ugonjwa ambao mke wangu anao, mara nyingine yeye husema mambo yanayoniumiza. Hilo linapotokea, ninajikumbusha kwamba maneno yake hayaonyeshi jinsi anavyohisi kikweli. Hali zinapokuwa ngumu sana, mimi hukumbuka andiko la 1 Wakorintho 13:5, linalonichochea kuzungumza naye kwa heshima badala ya kumkasirikia.” (Met. 19:11) Mke anamheshimu mume wake kwa kutaja sifa zake nzuri anapozungumza na wengine. (Efe. 5:33) Anaepuka dhihaka, kejeli, na matusi; anatambua kwamba mwenendo huo ni kama kutu inayoharibu ndoa. (Met. 14:1) Dada mmoja nchini Italia ambaye mume wake ana ugonjwa wa kuwa na wasiwasi kupita kiasi anasema hivi: “Nyakati nyingine, ninahisi kwamba mume wangu ana wasiwasi kupita kiasi. Zamani, maneno na ishara za uso wangu zilionyesha kwamba sikumheshimu. Lakini nimeona kwamba kadiri ninavyoshirikiana na watu wanaowazungumzia wengine kwa heshima, ndivyo ninavyochochewa kumwonyesha heshima mume wangu.”
Tunapowaonyesha heshima watu wetu wa familia, tunamheshimu Yehova, Kichwa chetu cha familia (Tazama fungu la 9)
10. Vijana wanawezaje kuonyesha kwamba wanawaheshimu wazazi wao?
10 Enyi vijana, tiini sheria ambazo wazazi wenu wamewawekea. (Efe. 6:1-3) Onyesheni heshima mnapozungumza na wazazi wenu. (Kut. 21:17) Kadiri wazazi wako wanavyokuwa na umri mkubwa zaidi, waonyeshe heshima kwa kuwapatia msaada wanaohitaji. Fanya yote uwezayo ili kuwatunza. Fikiria mfano wa María, ambaye baba yake si Shahidi wa Yehova. Baba yake alipougua, alifanya iwe vigumu kwa María kumtunza. Anakumbuka hivi: “Nilisali ili niwe na mtazamo wenye heshima kumwelekea baba yangu, na pia niweze kumwonyesha heshima. Nilijiambia kwamba ikiwa Yehova ameniagiza niwaheshimu wazazi wangu, basi bila shaka atanipatia nguvu za kufanya hivyo. Baada ya muda, nilitambua kwamba baba yangu hahitaji kubadili mwenendo wake ili nimtendee kwa heshima.” Tunapowaheshimu watu wa familia yetu licha ya udhaifu wao, tunathibitisha kwamba tunaheshimu mpango wa Yehova.
WAONYESHE HESHIMA WAABUDU WENZAKO
11. Kwa nini huenda ikawa vigumu kuwaonyesha heshima waabudu wenzetu?
11 Changamoto. Waabudu wenzetu wanaishi kulingana na viwango vya Biblia; hata hivyo, pindi nyingine wanaweza kututendea kwa njia isiyo ya fadhili, wakatuhukumu kwa njia isiyo ya haki, au wakatuudhi. Ikiwa mwabudu mwenzetu atatupatia “sababu ya kulalamika,” huenda ikiwa vigumu kwetu kuendelea kumwonyesha heshima. (Kol. 3:13) Ni nini kinachoweza kutusaidia kuendelea kuonyesha heshima?
12. Kwa nini ni muhimu kuwaonyesha heshima waabudu wenzetu? (2 Petro 2:9-12)
12 Kwa nini uonyeshe heshima? (Soma 2 Petro 2:9-12.) Katika barua yake ya pili iliyoongozwa na roho, Petro alisema kwamba baadhi ya watu katika kutaniko la Kikristo la karne ya kwanza walikuwa wakizungumza bila heshima kuhusu “watukufu,” yaani, wazee Wakristo. Malaika waaminifu walioona jambo hilo walitendaje? “Kwa sababu wanamheshimu Yehova,” hawakusema hata neno moja la matukano dhidi ya watenda dhambi hao. Wazia jambo hilo! Malaika wakamilifu walikataa kuzungumza kwa ukali kuhusu wanaume hao waliokuwa na majivuno. Badala yake, walimwachia Yehova awahukumu na kuwakemea. (Rom. 14:10-12; linganisha Yuda 9.) Tunaweza kujifunza kutoka kwa malaika hao. Ikiwa hatupaswi kuwatendea bila heshima watu wanaotupinga, basi tunapaswa kuwaonyesha heshima hata zaidi waabudu wenzetu. Tunapaswa ‘kuwa wa kwanza’ katika kuwaonyesha heshima. (Rom. 12:10) Kufanya hivyo kunaonyesha kwamba tunamheshimu Yehova.
13-14. Tunawezaje kuwaonyesha heshima wengine kutanikoni? Toa mfano. (Tazama pia picha.)
13 Jinsi ya kuonyesha heshima. Enyi wazee, jitahidini kuwafundisha wengine kwa njia ya upendo. (Flm. 8, 9) Ikiwa utahitaji kumpa mtu shauri, fanya hivyo kwa fadhili, na si ukiwa umeudhika. Akina dada, mnaweza kufanya mengi ili kuchangia hali ya kuheshimiana kutanikoni na kuilinda kwa kukataa kujihusisha katika porojo zisizofaa au uchongezi. (Tito 2:3-5) Sisi sote tunaweza kuonyesha kwamba tunawaheshimu wazee wa kutaniko kwa kuwaunga mkono na kuwaonyesha shukrani kwa kazi ngumu wanayofanya ya kuongoza mikutano, kazi ya kuhubiri, na kuwasaidia wale ambao wamechukua “hatua isiyofaa.”—Gal. 6:1; 1 Tim. 5:17.
14 Dada anayeitwa Rocío aliona ikiwa vigumu kumheshimu mzee aliyempatia ushauri. Anasema hivi: “Nilihisi kwamba amenionea. Nilipokuwa nyumbani, nilimzungumzia kwa njia mbaya. Ingawa nilijitahidi kutoonyesha hisia zangu, moyoni nilitilia shaka nia yake na kupuuza ushauri wake.” Ni nini kilichomsaidia Rocío? Anaeleza hivi: “Katika usomaji wangu wa Biblia, nilisoma andiko la 1 Wathesalonike 5:12, 13. Nilipotambua kwamba sikumwonyesha heshima ndugu huyo, dhamiri yangu ilianza kunisumbua. Nilisali kwa Yehova na kufanya utafiti katika machapisho yetu ili kupata habari hususa ambazo zingenisaidia kubadili mtazamo wangu. Hatimaye, nilitambua kwamba tatizo halikuwa ndugu huyo, bali kiburi changu. Sasa ninaelewa kwamba ninahitaji kuwa mnyenyekevu ili niweze kuwaheshimu wengine. Bado ninahitaji kuboresha sifa hiyo, lakini ninapojitahidi kuonyesha heshima, ninahisi nikiwa na amani pamoja na Yehova.”
Sisi sote tunaweza kuonyesha kwamba tunawaheshimu wazee wa kutaniko kwa kuwaunga mkono na kuwaonyesha shukrani kwa kazi ngumu wanayofanya (Tazama fungu la 13-14)
WAONYESHE HESHIMA WALIO NJE YA KUTANIKO
15. Kwa nini huenda ikawa vigumu kwetu kuwaonyesha heshima wale ambao wako nje ya kutaniko?
15 Changamoto. Mara nyingi tunakutana na watu katika huduma ambao wanaonekana hawapendi kweli za Biblia. (Efe. 4:18) Baadhi ya watu wanakataa kusikiliza ujumbe wetu kwa sababu ya malezi yao. Huenda tukahitaji kukabiliana na waajiri au walimu wakali, na wafanyakazi au wanafunzi wenzetu ambao ni vigumu kushughulika nao. Baada ya muda, huenda tukaanza kuacha kuwaheshimu na kuacha kuwatendea kwa njia ambayo sisi tungependa kutendewa.
16. Kwa nini ni muhimu kuwaonyesha heshima wale ambao kwa sasa hawamtumikii Yehova? (1 Petro 2:12; 3:15)
16 Kwa nini uonyeshe heshima? Kumbuka kwamba Yehova anakazia uangalifu jinsi tunavyowatendea watu wasio waamini. Mtume Petro aliwakumbusha Wakristo kwamba huenda mwenendo wao mzuri ungewachochea baadhi ya watu “wamtukuze Mungu.” Kwa sababu hiyo, aliwahimiza watetee imani yao “kwa upole na heshima kubwa.” (Soma 1 Petro 2:12; 3:15.) Iwe wanashtakiwa mahakamani kwa sababu ya imani yao au wanatetea imani yao wanapozungumza na jirani, Wakristo walipaswa kuwatendea watu wasio waamini kama tu ambavyo wangewatendea ikiwa wangekuwa mbele za Mungu. Isitoshe, Yehova anaona na anasikiliza mambo tunayosema na jinsi tunavyoyasema. Hiyo ni sababu muhimu sana ya kuwatendea kwa heshima wale ambao wako nje ya kutaniko!
17. Tunawezaje kuwaonyesha heshima wale walio nje ya kutaniko?
17 Jinsi ya kuonyesha heshima. Tunapokuwa katika huduma, tusingependa kamwe kuonekana kana kwamba tunawadharau wale ambao wana ujuzi kidogo au hawana kabisa ujuzi wa Biblia. Badala yake, tungependa kuwaona wengine kuwa wenye thamani kwa Mungu na bora kuliko sisi. (Hag. 2:7; Flp. 2:3) Ikiwa mtu atakutukana kwa sababu ya mambo unayoamini, usilipize kisasi, kwa mfano kwa kutumia maneno ya dhihaka. (1 Pet. 2:23) Ikiwa utasema jambo ambalo unajutia, mwombe msamaha bila kukawia. Unawezaje kuwaonyesha heshima wale unaofanya nao kazi? Jitahidi kuwa mfanyakazi mwenye bidii na jitahidi kusitawisha mtazamo mzuri kuwaelekea wale ambao unafanya nao kazi au waliokuajiri. (Tito 2:9, 10) Unapokuwa mfanyakazi mnyoofu na mwenye bidii, huenda ukawafurahisha watu au la, lakini bila shaka utamfurahisha Yehova.—Kol. 3:22, 23.
18. Kwa nini tutanufaika tunapositawisha na kuwaonyesha wengine heshima?
18 Tuna sababu nzuri sana za kusitawisha na kuwaonyesha heshima wengine! Tumeona kwamba tunapowaonyesha heshima watu wetu wa familia, tunamheshimu Yehova, Kichwa chetu cha familia. Vivyo hivyo, tunapowaonyesha heshima ndugu na dada zetu wa kiroho, tunamheshimu Baba yetu wa mbinguni. Na tunapowaonyesha heshima wale walio nje ya kutaniko, tunatengeneza mazingira bora kabisa kwa wao kumtukuza, au kumheshimu, Mungu wetu mkuu. Hata ikiwa baadhi ya wanadamu hawatatuonyesha heshima, tutanufaika tunapositawisha na kuwaonyesha wengine heshima. Kwa nini? Kwa sababu Yehova atatubariki. Anaahidi hivi: “Wale wanaoniheshimu nitawaheshimu.”—1 Sam. 2:30.
WIMBO 129 Tutaendelea Kuvumilia
a Baadhi ya majina yamebadilishwa.