1 Timotheo
3 Taarifa hiyo ni ya uaminifu.
Ikiwa mtu yeyote anajitahidi kufikilia cheo cha mwangalizi, yeye ni mwenye kutamani kazi bora. 2 Kwa hiyo mwangalizi apaswa kuwa asiyelaumika, mume wa mke mmoja, mwenye kiasi katika mazoea, timamu katika akili, mwenye utaratibu, mkaribishaji-wageni, mwenye sifa ya kustahili kufundisha, 3 si mwenye fujo ya ulevi, si mpiga-watu, bali mwenye kukubali sababu, si mtaka-vita, si mpenda-fedha, 4 mtu anayesimamia watu wa nyumbani mwake mwenyewe kwa njia bora, akiwa na watoto walio katika ujitiisho pamoja na uchukuaji-mambo kwa uzito wote; 5 (kwa kweli ikiwa mtu yeyote hajui jinsi ya kusimamia watu wa nyumbani mwake mwenyewe, atatunzaje kutaniko la Mungu?) 6 si mtu aliyegeuka hivi karibuni, kwa kuhofu kwamba huenda akajitutumua kwa kiburi na kuanguka ndani ya hukumu iliyopitishwa juu ya Ibilisi. 7 Zaidi ya hayo, yeye apaswa pia kuwa na ushuhuda bora kutoka kwa watu walio nje, ili asipate kuanguka ndani ya shutumu na mtego wa Ibilisi.
8 Watumishi wa huduma wapaswa hivyohivyo kuwa wachukua-mambo kwa uzito, si wenye ndimi mbili, si wenye kujitoa kwa divai nyingi, si wenye pupa ya pato lisilo la haki, 9 wakishika siri takatifu ya imani kwa dhamiri safi.
10 Pia, acha hawa wajaribiwe juu ya kufaa kwanza, kisha acha watumike wakiwa wahudumu, kwa kuwa hawana shtaka.
11 Wanawake wapaswa hivyohivyo kuwa wachukua-mambo kwa uzito, si wenye uchongezi, wenye kiasi katika mazoea, waaminifu katika mambo yote.
12 Acha watumishi wa huduma wawe waume wa mke mmoja, wakisimamia watoto na watu wa nyumbani mwao wenyewe kwa njia bora. 13 Kwa maana watu wahudumuo kwa njia bora wanajipatia wao wenyewe msimamo bora na uhuru mwingi wa usemi katika imani kwa kuhusiana na Kristo Yesu.
14 Ninakuandikia wewe mambo haya, ingawa ninatumaini kukujia wewe upesi, 15 lakini endapo nakawizwa, ili upate kujua jinsi upaswavyo kujiendesha mwenyewe katika watu wa nyumbani mwa Mungu, ambao ni kutaniko la Mungu aliye hai, nguzo na tegemezo la ile kweli. 16 Kwa kweli, siri takatifu ya ujitoaji-kimungu huu ni kubwa kwa kukiri wazi: ‘Yeye alifanywa dhahiri katika mwili, alitangazwa kuwa mwadilifu katika roho, alionekana kwa malaika, alihubiriwa miongoni mwa mataifa, aliaminiwa katika ulimwengu, alipokewa juu katika utukufu.’