Unafanya Nini Sasa Ujitayarishe?
WATANGAZA habari wanatabiri nyakati zenye magumu wakati ujao. Je! kuna lo lote tunaloweza kufanya tujitayarishe?
Je! utajaza mashine yako ya barafu na mamia ya ratili za chakula? Je! utaweka kwa ubahili vyakula vyote vya mikebe unavyoweza kununua? Je! utajifunza kulenga shabaha kwa bastola ili ujilinde na wavunja sheria? Au utanunua bunduki nyingi ulinde chakula chako ulichoweka kwa ubadili? Je! utahamia mahali pa mbali pasipo na ustaarabu?
Lakini fikiria vile matayarisho hayo yote yangeweza kuwa ya bure tu. Mkondo wa stimu au gas unapokatika, chakula kilichogandishwa na barafu kinaharibika. Wakati chakula kinapokuwa kidogo sana, wenye kukiweka kwa ubahili wanakuwa katika hatari ya kunyang’anywa na kuuawa pia. Hakuna kinachoweza kuzuia watu wenye njaa. Bunduki hazitazuia wavunja sheria. Kwa kweli, kwa kawaida wavunja sheria huchukua hata “tonge” lile la mwisho wanapokushambulia kwa ghafula. Tena, kuna hatari nyingi zaidi za wakati ujao.
HATARI KUU
Hatari hiyo inatokana na chanzo cha juu. Ni siku ya kutoa hesabu ambayo Mungu atafanya na taratibu nzima ya mambo—ya kidini, ya kisiasa na ya kibiashara. Hatari zisizomalizika katika kila upande zaonyesha kwamba taratibu ya ulimwengu ‘imepimwa katika mizani ikaonekana kuwa imepunguka,’ na kwamba karibuni itaondoka.—Dan. 5:27; 1 Yohana 2:17.
Kwa hiyo, jambo la kwanza kujitayarishia si namna ya kujilinda na yanayoweza kufanywa na wanadamu, bali kujitayarisha kuokoka Mungu. aharibupo ulimwengu huu mwovu. Jitayarishe ili upate upendeleo wake naye apate kukuangalia. Ikiwa hakuangalii, matayarisho mengine yote ni ubatili, ni ya bure tu. (Zab. 127:1) Ukijitayarisha kwa kusudi la kumpendeza Mungu, huna haja ya kuwa na wasiwasi juu ya magumu yanayotazamiwa wakati wa kuangamia kwa ulimwengu huu wa zamani, hata upinzani na mateso yake.
KUPAMBANA NA MAGUMU YA UCHUMI
Ni hakika kwamba idadi yote ya dunia inakabiliwa na magumu ya namna nyingi. Utukuzo wa taifa, vyama vyenye kujitakia faida zao wenyewe, kutia na vya kisiasa, mabishano juu ya kusimamia wafanya kazi, kupunguzwa kwa matumizi ya vitu, kupunguzwa kwa thamani ya pesa, upungufu wa chakula, njaa kuu mahali mahali—hayo ni mambo ambayo yamekwisha leta magumu makubwa na bado yataleta taabu kuu zaidi. Yametuzunguka sana hata hatuwezi kupanga kimbele tuyaepuke kabisa. Lakini tunaweza kutumia kwa hekima vitu tulivyo navyo sasa. Kwa njia gani?
Mtume Paulo alimwandikia Timotheo, mwangalizi katika kundi la Kikristo, akamwambia hivi: “Walio matajiri wa ulimwengu wa sasa uwaagize wasijivune, wala wasiutumainie utajiri usio yakini, bali wamtumaini Mungu atupaye vitu vyote kwa wingi ili tuvitumie kwa furaha. Watende mema, wawe matajiri kwa kutenda mema, wawe tayari kutoa mali zao, washirikiane na wengine kwa moyo; huku wakijiwekea akiba iwe msingi mzuri kwa wakati ujao, ili wapate uzima ulio kweli kweli.”—1 Tim. 6:17-19.
Yanayosemwa hapa yanahusu pia wale wasio matajiri. Wote lazima wajifunze kutegemea sana Mungu. Vilevile, lazima tusijifikirie wenyewe tu. Hiyo ni tofauti kabisa na njia ya ulimwengu ya kuwaza lakini inafanya mtu apate (ashike sana, NW) uzima ulio kweli kweli.
Katika Mahubiri yake juu ya Mlima, Yesu alisema maneno yenye kufariji wenye kumtumikia Mungu, ambao huenda wakawa wana mashaka juu ya mahitaji yao ya kila siku. Alisema: “Msisumbukie maisha yenu, mle nini au mnywe nini; wala miili yenu, mvae nini. Maisha je! si zaidi ya chakula, na mwili zaidi ya mavazi?” Halafu akamalizia: Msisumbuke, basi, mkisema, Tule nini? na Tunywe nini? au Tuvae nini? Kwa maana hayo yote Mataifa huyatafuta; kwa sababu Baba yenu wa mbinguni anajua ya kuwa mnahitaji hayo yote. Bali utafuteni kwanza ufalme wake, na haki yake; na hayo yote mtazidishiwa. Basi msisumbukie ya kesho; kwa kuwa kesho itajisumbukia yenyewe. Yatosha kwa siku maovu yake.—Mt. 6:25-34; linganisha Waebrania 13:5, 6.
Kwa hiyo, kama Yesu alivyotaja, Wakristo wana njia ya kutatua tatizo la uchumi. Njia hiyo yakazia kumtumaini Mungu na kufikiria wengine—kuwa na nia ya kuwagawia vitu. Wafanyapo mambo hayo, Mungu huwaangalia.
Bila shaka, iko mikazo mingine ambayo lazima ikabiliwe pia. Yesu aliambia wanafunzi wake hivi: “Mtakuwa watu wa kuchukiwa na mataifa yote kwa ajili ya jina langu.” (Mt. 24:9) Wewe waonaje kukabiliwa na mateso?
JE! UNAOGOPA MATESO?
Bila shaka, hakuna mtu anayefurahia mateso, na kila mtu huyaogopa. Kwa hiyo ikiwa una woga wa kawaida, usiwe na wasiwasi; wewe si mtu asiye wa kawaida. Lakini je! wewe una woga wa kupindukia, hofu yenye kugonjwesha, woga unaokufanya ujisikie unataka kurudi nyuma? (Ebr. 10:39) Basi yakupasa uchukue hatua za kujizoeza ifaavyo kiroho.
Jambo zuri kufanya ni kutazama mifano ya Biblia ya wanaume na wanawake waliopatwa na mateso lakini wakafaulu. Twaona kwamba walipata nguvu nyingi kupitia kwa sala. Eliya alikuwa mmoja. Aliogopa akakimbia wakati Mfalme Ahabu na mkewe Yezebeli walipotaka kumwua. Lakini alisali kwa Mungu kwa sababu ya kukata tamaa, kisha Yehova akamtia nguvu kupitia kwa malaika. Halafu Eliya akarudi kijasiri akatimize agizo lake la kinabii. (1 Wafalme sura ya 19) Mfalme Daudi aliendelea kuwa na nguvu katika mateso mengi kwa sababu ya sala. Zaburi 55 mpaka 57 ni baadhi ya sala hizo. Mwandikaji wa Kitabu cha Waebrania ataja mifano mingi ya wavumilivu walioshinda. Halafu anamaliza, akikaza fikira kwenye mfano mkubwa hata zaidi wenye kutuongoza sana tuvumilie:
“Basi na sisi pia, kwa kuwa tunazungukwa na wingi kubwa la mashahidi namna hii, . . . na tupige mbio kwa saburi katika yale mashindano yaliyowekwa mbele yetu, tukimtazama Yesu, mwenye kuanzisha na mwenye kutimiza imani yetu; ambaye kwa ajili ya furaha iliyowekwa mbele yake aliustahimili [mti wa mateso] na kuidharau aibu, naye ameketi mkono wa kuume wa kiti cha enzi cha Mungu.”—Waebrania sura 11; 12:1, 2.
Je! wewe unasema kama wengine, ‘Mimi sijui kama naweza kuvumilia mapigo, kuteswateswa mwili na kunyimwa riziki?’ Au, ‘Nisomapo yaliyopata mashahidi wa Yehova katika kambi za mateso za Nazi naogopa kwamba siwezi kushikamana na ukamilifu wangu nikipatwa nayo’?
Ikiwa unajisikia hivyo, jiulize, Nitafanya nini SASA? Ukristo ni njia ya maisha; ni jambo la kila siku. Je! unaishi kulingana na kanuni za Biblia? Au unafikiri kivivu, ukiepuka jambo ambalo unajua wapaswa kufanya? Je! unafuatia faida ya kimwili na kuachilia madaraka, mashirika na utendaji wa Kikristo? Je! unashikilia tabia au mazoea fulani yanayokurudisha nyuma? Je! watu unaoshirikiana nao ni wale wasiopendezwa na makusudi ya Mungu?
Unapenda nini? “Kwa kuwa hazina yako ilipo, ndipo utakapokuwapo na moyo wako.” (Mt. 6:21) Je! unapenda starehe na raha sana hata zinakuzuia usifanye mambo unayojua wapaswa kufanya? Je! unapenda anasa fulani inayoharibu hali yako ya kiroho? Ikiwa ndivyo, iondolee mbali sasa, au sivyo moyo wako wote, au nusu yake, utaielekea nyakati zote. Usipoelekeza moyo wako wote kwa Mungu huwezi kuendeleza ukamilifu ujaribiwapo.—Yak. 1:5-8.
Walakini, jambo kuu si lile usilofanya. Bali, ulizo ni, Unafanya nini? (Yak. 1:23-25) Yesu hakuambia “kondoo” katika mfano wa kondoo na mbuzi kwamba walikuwa wameepuka kudhuru kusudi lake, lakini alisemaje? “Nalikuwa na njaa, mkanipa chakula; nalikuwa na kiu, mkaninywesha; nalikuwa mgeni, mkanikaribisha; nalikuwa uchi, mkanivika; nalikuwa mgonjwa, mkaja kunitazama; nalikuwa kifungoni, mkanijia. . . . kadiri mlivyomtendea mmojawapo wa hao ndugu zangu walio wadogo, mlinitendea mimi.”—Mt. 25:35-40.
Kwa upande mwingine, Yesu aliambia “mbuzi” nini? “Kadiri msivyomtendea mmojawapo wa hao walio wadogo, hamkunitendea mimi.” (Mt. 25:45) Hakusema kwamba bila shaka “mbuzi” walizoea mabaya makubwa, ingawa wengine walifanya hivyo. Kutomtunza Kristo, ndugu zake waliozaliwa kwa roho na kutiwa mafuta, au kutojali ujumbe na kazi yao kulitosha.
THAMINI CHAKULA CHA KIROHO SASA
Wanaume na wanawake wa Kikristo walioendelea kuwa waaminifu katika mateso makali sana ya kambi za mateso za Nazi wanasema kwamba wale waliokuwa na msingi mzuri kwa kujifunza Biblia na kushirikiana na ndugu zao ndio waliokuwa na nguvu, ndio waliovumilia.
Mmoja wa mashahidi wa Yehova aliyekaa katika magereza ya Kikomunisti zaidi ya miaka kumi, saba kati yake katika kizuizi cha kuwa peke yake kabisa Ujeremani ya Mashariki, alisema: “Namshukuru sana Yehova kwamba kwa msaada wa roho yake niliweza kuendelea kuwa mwenye nguvu za kiroho miaka kumi hii ya kutenganishwa kabisa na tengenezo lake. Ningependa kutia kila mtu moyo athamini inavyofaa chakula chote cha kiroho tunachopewa, kwa maana hatujui namna kitakavyotufaa wakati fulani. Tukila chakula cha kiroho cha wakati wake kwa kawaida, kitatusaidia tukiwa katika nyakati zenye magumu makubwa na tukiwa peke yetu, ili tumtumainie Yehova na kuvumilia tukiwa thabiti upande wake.”
Shauri la Yesu, “Utafuteni kwanza ufalme wake, na haki yake,” linatuonyesha kweli njia ya kuokoka. (Mt, 6:33) Kutafuta Ufalme kwatia ndani kuzijua sheria zake na kazi yake na kuunga mkono kwa ushikamanifu. Kutafuta haki ya Mungu kwatia ndani kumpenda Mungu na wale walio na roho yake.
Ikiwa tunataka msaada wa Mungu katika majaribu, lazima tushirikiane na watu wake sasa na kusikiliza yanayosemwa katika makusanyiko yao, na kuonyesha imani yetu wenyewe pia mbele yao. Yatupasa kushiriki na watu wa Yehova kuutolea Ufalme ushuhuda. Vilevile tutasaidia watu wengine wajitayarishe pamoja nasi kwa mambo yaliyoko mbele. Tukifanya hivyo sasa, tunaweza kuwa na dhamiri njema, tukijua kwamba tunajitayarisha ifaavyo, tukiweka msingi imara wa uzima ulio kweli kweli.—1 Pet. 3:16, 17.