Mshahara wa Kutoaminika
Makala hii ni ya kutumia kwa mafunzo ya kitabu ya kundi
1-3. Mwendo wa Yuda Iskariote waonyeshaje wazi mshahara wa kutoaminika?
HAKUNA nafasi ya mtu asiyeaminika katika mpango wo wote wa Mungu au mwanadamu. Hasa ndivyo ilivyo kwa wale waliowekwa katika vyeo vyenye daraka. “Inayohitajiwa katika mawakili, ndiyo mtu aonekane kuwa mwaminifu,” yasema Biblia.—1 Kor. 4:2.
2 Yesu Kristo alipokuwa duniani wanaume kumi na wawili walikuwa na nafasi isiyo na kifani ya kuwa washikia wake wa karibu—kujifunza moja kwa moja kutoka kwake na kuwa wanafunzi wake wenye madaraka zaidi. Walakini, mmoja wao aliacha kuthamini akawa asiyeaminika, akisababisha matata mengi kwa Yesu na mitume waaminifu kumi na mmoja. Kutoaminika kwa Yuda Iskariote kulimpotezea zawadi nzuri sana ya uzima wa kimbinguni kama mfalme-mshirika na kuhani mdogo wa Kristo. Alifukuzwa katika kikundi cha Yesu cha usiri kabla Yesu hajaanzisha chakula cha Ukumbusho naye aliikosa ahadi ya Kristo kwa wale waaminifu kumi na mmoja kwamba “ndinyi mliodumu pamoja nami katika majaribu yangu. Nami nawawekea ninyi ufalme, kama vile Baba yangu alivyoniwekea mimi.”—Luka 22:28, 29; 13:22-30.
3 Mshahara wa kutoaminika kwa Yuda ulikuwa nini? Kwa upande mmoja, vipande 30 tu vya fedha (bei ya mtumwa akiuawa na ng’ombe dume wa mtu)—upande mwingine, kuchukiwa na Mungu na mauti. (Kut. 21:32) Hata adui za Yesu, ambao Yuda alishirikiana nao kupanga mipango yao, walimdharau msaliti huyu. Baada ya Yesu kulaaniwa na baraza kuu ya Kiyahudi, Yuda alipatwa na maumivu makuu sana akilini, hata akaitupa fedha ya usaliti na kutoka nje akajinyonga. Hii haikuwa kwa kutubu kwa kweli, bali kwa sababu aliona kwamba alikuwa amepoteza kila kitu. Yesu alimwita “mwana wa upotevu.”—Yohana 17:12; Mt. 27:3-10.
LAZIMA KILA MTU AJIANGALIE
4. (a) Jamii ya “mtumwa mwaminifu mwenye akili” ilianzishwa wakati gani, na ni wakati gani ilipoanza Kulisha jamaa ya waaminio? (b) Je! jamii ya “mtumwa mwaminifu mwenye akili” ingekuwa ‘mtumwa asiyeaminika’ wakati wo wote?
4 Muda mfupi baada ya ufufuo wa Yesu na kupaa mbinguni yeye alilianzisha kundi la Kikristo, siku ya Pentekoste ya mwaka wa 33 C.E. Huko jamii ya “mtumwa mwaminifu mwenye akili” ilianza kulisha watu hao mmoja mmoja katika ‘jamaa ya waamini’ wa Mungu iliyoanzishwa karibuni chakula cha kiroho. (Matendo 2:1, 14, 46, 47) Jamii hii ya “mtumwa,” kundi la Kikristo lililotiwa mafuta kwa roho, ingeendelea kuwa nyaminifu mpaka wakati wa kuja kwa Kristo aiharibu taratibu mbovu ya mambo iliyopo.—Mt. 28:18-20.
5. (a) Kwa kweli ni nini kilichotangulia kuamriwa mapema kwa habari ya Israeli wa kiroho? (b) Kwa sababu gani, basi, onyo lilikuwa lazima litolewe juu ya kutoaminika?
5 Hata hivyo, Yesu aliwapa onyo kwa habari ya uaminifu. Kwa sababu gani? Basi, kama jamii, kundi la Mungu lingeendelea kuwa jaminifu. Biblia yaonyesha kwamba hesabu ya 144,000 iliyotangulia kuamriwa mapema ingekamilishwa. Hesabu hiyo mwishowe ‘ingetiwa muhuri’ kama nyaminifu. (Ufu. 7:1-8; 14:1-5) Hivyo ‘Israeli wote [wa kiroho], au, [Israeli wa Mungu] wangeokolewa.’ (Rum. 11:26; linganisha Wagalatia 6:16.) Lakini kwa habari ya watu mmoja mmoja ambao wangefanyiza kundi hilo au jamii hiyo ya “mtumwa,” walipaswa wajaribiwe na kutakiwa wahakikishe ukamilifu na uaminifu wao. “Mwenye kuvumilia hata mwisho, ndiye atakayeokoka,” kasema Yesu.—Mt. 24:13; Yak. 1:3; Ufu. 14:12.
6. Yesu alitoa onyo juu ya kutoaminika kwa maneno gani?
6 Kwa hiyo, baada ya kusema juu ya “mtumwa mwaminifu mwenye akili” ambaye angekuwa mwaminifu mpaka kuja kwake, Yesu aliendelea kusema: “Lakini ikiwa mtumwa mwovu huyo atasema moyoni mwake, ‘Bwana wangu anakawia,’ na aanze kupiga watumwa wenzake na kula na kunywa na walevi kabisa wa siku nyingi [kwa halisi, (wale) wanaolewa], bwana wa mtumwa huyo atakuja katika siku asiyoitazamia na katika saa asiyoijua, naye atamwadhibu kwa ukali ulio mwingi zaidi sana [kwa halisi, yeye atakata vipande vipande huyo] naye atamgawia sehemu yake na wanafiki.”—Mt. 24:48-51; Luka 12:45, 46, Kingdom Interlinear Translation.
7. Alipokuwa akitoa onyo lake katika Mathayo 24:48-51 na Luka 21:36 Yesu alitangulia kujua nini mapema?
7 Twaona kwamba Yesu hakusema kwamba “mtumwa mwaminifu mwenye akili” angekuwa asiyeaminika. Lakini, kwa habari ya washiriki mmoja mmoja wa jamii hiyo ya “mtumwa,” Yesu alionyesha tu uwezekano wa kwamba si wote wangekuwa waaminifu, kama vile mmoja wa wale kumi na wawili, Yuda, alivyogeuka kuwa mbaya baada ya kuwa na mwanzo ufaao. Yehova Mungu atakubali watu waaminifu tu waliojaribiwa wawe warithi wa Ufalme. (2 Pet. 1:10, 11) Kwa hiyo Yesu alionya kila mmoja wa wafuasi wake waliozaliwa kwa roho na kutiwa mafuta ajiangalie. Aliwaambia wanafunzi wake wote hivi: “Basi, kesheni ninyi kila wakati, mkiomba, ili mpate kuokoka katika hayo yote yatakayotokea, na kusimama mbele za Mwana wa Adamu.”—Luka 21:36.
MATENDO YA “MTUMWA MWOVU” NA THAWABU YAKE
8. Kila mmoja wa jamii ya “mtumwa” wa Kristo angepaswa aangalie nini?
8 Kwa hiyo, ilimpasa kila mmoja aangalie sana asiwe mwenye kujitegemea, mzembe au mwenye kusinzia. Mtume Paulo alishauri hivi: “Anayejidhania kuwa amesimama na aangalie asianguke.” (1 Kor. 10:12) Bila shaka wakati wa kulewa ulikuwa umepita, ama kwa kutumia divai halisi, au kwa njia ya kiroho pamoja na walevi wa kidini.—Isa. 29:9; 1 Pet. 4:3.
9. Maneno ya Yesu katika Mathayo 24:48-51 yaonyesha watu wanaokuwa “mtumwa yule mbaya” wangefuata mwendo gani wa tendo?
9 Yesu aeleza katika Mathayo 24:48-51 namna ambavyo mtu anayekuwa asiyeaminika angefikiri, kusema na kutenda. Wengine kati ya waliokuwa washiriki wa jamii ya “mtumwa” wakati mmoja wangepoteza furaha yao ya kutazamia mema nao wangechoshwa na kungojea kuja kwa Bwana. Wangekuwa wenye kujitafutia yao wenyewe. Wenye kufuata mwendo huo wangekuwa rafiki za ulimwengu, hivyo adui za Mungu. (Yak. 4:4) Wangeanza ‘kupiga watumwa wenzao’ kwa maneno, wakiwapinga wao na kazi yao ya kutangaza habari njema za Ufalme. Katika “siku za mwisho” hizi wako wengine wa namna hiyo wafanyizao jamii hiyo, kulingana na mwenendo wao, wasiotambua kuwapo kwa Kristo kusikoonekana na wasiofahamu na kukubali kwamba wakati wa kuja kwake kuharibu taratibu ya ulimwengu ya mambo u karibu.
10. Nia ya wale waliogeuka kuwa wasioaminika ingekuwa nini, na je! wangefanikiwa katika kutenganisha au kutawala kundi la Kristo?
10 ‘Kupiga watumwa wenzao’ huku kwa maneno kungekuwa kwa sababu walitaka kutawala au kutumia uwezo juu ya wengine. Walitamani cheo kikubwa wapate kuheshimiwa. Lakini hawakuweza kupata makuu waliyotamani. Kristo hakuwaruhusu wasioaminika hao watawale wala wavunje kundi lake na kukomesha kazi linayofanya. Bali, baada ya kukagua, Kristo ‘angewakata hao vipande vipande,’ akiwatenga watu hao mmoja mmoja na jamii ya “mtumwa mwaminifu mwenye akili.”
11, 12. (a) Je! Kristo alitangulia kuamuru mapema kwamba kungekuwa na jamii ya “mtumwa yule mbaya”? (b) Wasioaminika wanakuwaje kama wanafiki wa Jumuiya ya Wakristo, nao wanagawiwaje sehemu yao na wanafiki?
11 Ingawa Kristo alieleza mwenendo ambao ungeonyesha wasioaminika, bila shaka yeye hakutangulia kuamuru mapema kwamba ndivyo wangekuwa hata kabla ya wao kuwa hivyo. Wao wanafuata mwendo wa kutoaminika kulingana na uchaguzi wao wa hiari na tamaa zao. Wao wanafanana na “mtumwa mbaya na mlegevu” wa mfano wa talanta. (Mt. 25:24-30) Wao ni ‘mawakili’ wasioaminika na kwa hiyo hawawezi kubaki katika watu wa nyumba ya Kristo. (Mt. 24:45) Ukristo wao unakuwa wa unafiki nao wanakuwa pamoja na wanafiki wa kidini wa Jumuiya ya Wakristo (Kristendomu). Kwa kweli, wengine wao wameanza kuamini tena mafundisho ya uongo ya Jumuiya ya Wakristo, kama vile Utatu, kutokufa kwa nafsi ya kibinadamu na mateso halisi katika ‘moto wa mateso’ ya milele. Wengine wamejiunga na makanisa ya Jumuiya ya Wakristo na jitihada zao kupinga mashahidi wa Yehova wasihubiri habari njema.
12 Kati ya wanafiki wa Jumuiya ya Wakristo wasioaminika hawa hawapati furaha yo yote ya kiroho nao lazima washiriki yatakayowapata wanafiki hao. Kwa habari ya “mtumwa” mwovu huyo, “ndiko kutakuwako kilio na kusaga meno,” kasema Yesu. (Mt. 24:51) Semi zao si za toba ya kweli, bali ni za wasiwasi na kukata tamaa, “huzuni ya dunia” ambayo “hufanya mauti.” (2 Kor. 7:10) Hawana tamaa ya kushirikiana wala kufanya kazi pamoja na “mtumwa mwaminifu mwenye akili” katika utumishi wa kweli kwa Bwana.
WAKATI WA WOTE KUFIKIRI KWA UZITO
13. Kwa sababu gani wale leo wasimamao upande wa mtumwa “mwaminifu mwenye akili” wamepaswa pia wafikirie onyo la Kristo?
13 Kwa kuwa Kristo asema kwamba atafikiliza hukumu, ‘ianzayo katika nyumba ya Mungu,’ ni lazima kwa kila mtu aliye upande mmoja na jamii ya “mtumwa mwaminifu mwenye akili” ajiangalie. (1 Pet. 4:17) Amepaswa ajichunguze sikuzote juu ya uaminifu wake mwenyewe. Ajua kwamba uaminifu wa kutoka moyoni watakiwa. Katika siku hizi yawezekana kuwa mateka ya “dhambi ile ituzingayo kwa upesi”—kupoteza imani. (Ebr. 12:1) Iko hatari zaidi ya kufanya hivyo sasa kwa maana Ibilisi ajua ana wakati mfupi naye apiga vita kali juu ya waliozaliwa kwa roho wa Mungu na kutiwa mafuta walio duniani na pia wo wote washirikianao nao katika kuzihubiri habari njema za Ufalme.—Ufu. 12:12, 17; linganisha 1 Petro 5:8.
14. Ingawa ni vema kujua kwamba mwisho u karibu, lazima tuangalie nini?
14 Kwa kuwa twauona wazi utimizo wa unabii wa Kristo juu ya wakati wetu—tukiitambua “ishara” yenye kuhakikisha tunaishi katika “mwisho wa taratibu ya mambo,” yatupasa ‘tuinue vichwa vyetu juu kwa kuwa ukombozi wetu unakaribia.’ Pia, lazima tujiangalie sana na maisha tuishizo. Yesu alipokuwa akisema kwa faida ya wanafunzi wake waliokuwa naye wakati uo huo, alisema hivi pia: “Hilo niwaambialo ninyi, nawaambia wote, Kesheni.”—Marko 13:37; Luka 21:28.
15. Petro alituandikiaje yanayotiwa katika uaminifu, naye alionyeshaje uzito na lazima ya jambo hili?
15 Kwa hiyo, hali iliyopo ndiyo nzito kupita zote. Mtume Petro alimalizia kueleza hali yetu aliposema hivi: “Basi, kwa kuwa vitu hivi vyote vitayeyushwa hivi, imewapasa ninyi kuwa watu wa tabia gani katika mwenendo mutakatifu na utawa, mukitazamia na kutaka sana kuya kwa siku ya Mungu, kwa sababu yake, mbingu zikilungula zitayeyushwa, na viumbe vya asili vitayeyuka kwa moto mukali? Lakini kama ilivyo ahadi yake, tunatazamia mbingu mpya na inchi mpya, pahali haki inapoikala. Kwa hivi, wapenzi, kwa kuwa munatazamia maneno haya, fanyeni kwa nguvu ili mwonekane katika salama, pasipo kipaku wala laumu mbele yake.”—2 Pet. 3:11-14, Swahiii Congo Bibie.
16. Tofautisha mshahara wa kutoaminika na ule wa uaminifu.
16 Kwa hiyo, ingawa kuna vishawishi vingi na hata majaribu magumu, mshahara wa aliye mwaminifu ni kibali ya Mungu, furaha, amani na uzima wa milele. Kwa upande mwingine, kutoaminika huenda kukatoa uradhi wa tamaa za kimwili kwa muda mfupi, lakini karibuni kwaleta huzuni, aibu na mauti tu.
—Kutoka Kitabu God’s Kingdom of a Thousand Years Has Approached.