Historia ya Mashahidi wa Yehova Katika Nyakati za Kisasa
—Ujeremani (Inaendelea)
OKTOBA 7, 1934, itabaki milele kuwa jambo la pekee katika kumbukumbu za wale waliopata pendeleo la kushiriki katika matukio ya siku hiyo. Siku hiyo Hitler na serikali yake walikutana na tendo hodari la mashahidi wa Yehova—machoni pake wakiwa wachache wa kudhihakiwa.
Habari zote zilionyeshwa katika barua iliyotoka kwa Ndugu Rutherford, nakala yake ikawa itapelekwa na mjumbe wa pekee kwa kila kundi Ujeremani. Wakati uo huo wajumbe hawa waliagizwa wafanye matayarisho ya mikutano itakayofanywa Ujeremani mwote siku hii. Barua ya Ndugu Rutherford ilisema hivi, sehemu yake:
“Kila kikundi cha mashahidi wa Yehova katika Ujeremani kikusanyike pamoja katika mahali panapofaa mji wanamoishi, asubuhi ya Jumapili, Oktoba 7, 1934, saa 3:00. Barua hii isomwe kwa wote waliopo. Imewapasa mjiunge pamoja katika sala kwa Yehova mkimwomba kupitia kwa Kristo Yesu, Kichwa chetu na Mfalme wetu, uongozi wake, ulinzi, ukombozi na baraka. Mara baada ya hapo pelekeni barua kwa maafisa wa serikali ya Ujeremani ikiwa na maandiko ambayo yatakuwa yamekwisha tayarishwa mapema na yatakayopatikana wakati huo. Dakika chache zitumiwe kuzungumza Mathayo 10:16-24, mkikumbuka kwamba kwa kufanya kama andiko hili linavyosema, ‘mnasimamia maisha zenu.’ (Esta 8:11) Ndipo mkutano ufungwe nanyi mwaendee jirani zenu kuwapa ushuhuda juu ya jina la Yehova, juu ya Mungu wetu na Ufalme wake ulio chini ya Kristo Yesu.
“Ndugu zenu ulimwenguni mwote watakuwa wakiwafikiria ninyi nao watapeleka sala inayofanana na yenu kwa Yehova wakati ule ule.”
TANGAZO LA UMOJA LA KUAMUA KUMTII MUNGU
Ilikuwa lazima matayarisho yafanywe kwa siri kabisa, bila shaka. Kila ndugu aliyehusika alitakiwa akubali kutosema hata kwa mke wake mwenyewe au washiriki wengine wa jamaa juu ya yaliyokuwa yanapangiwa Oktoba 7. Kujapokuwa kujiangalia huku, hali ilitokea dakika ya mwisho ambayo, isingalikuwa ni kwa sababu ya mkono wenye nguvu wa ulinzi wa Yehova, kungaliweza kuwa na matokeo mabaya sana. Juu ya yaliyotukia katika Mainz, Konrad Franke asema hivi:
“Nilikuwa nimekamatwa mapema mwaka wa 1933 kwa mara ya kwanza nikatiwa katika kambi ya mateso, kwa hiyo baada ya kufunguliwa kwangu ilinilazimu mara nyingi niwafikie Gestapo (polisi), ambao walinishtaki kila mara juu ya kusimamia kazi katika mji huu, kuendelea kukamatwa kukitoa ushuhuda kwamba shughuli yenye kusimamiwa ya kuhubiri ilikuwa inaendelea. Kwa hiyo, nikatuma barua zangu kwa anwani ya siri, anwani ambayo Ndugu Franz Merck, msimamizi wetu wa utumishi wa jimbo, aliijua. Lakini kwa sababu isiyoelezeka yeye hakuwa amenipa mimi mwenyewe barua ya Ndugu Rutherford yenye maagizo ya maana kama ilivyokuwa imekubaliwa katika Basel, bali alinipelekea kwa posta kwenye anwani yangu ya kawaida na hasa ‘katika dakika ya mwisho.’ Linalofurahisha ni kwamba nilikuwa nimekwisha pashwa habari za shughuli hii na Ndugu Albert Wandres, ambaye nilifanya kazi naye karibu karibu sana, na kwa hiyo nilizifahamu habari zote zilizoandikwa katika barua. Kwa kuwa siku za kufikia Oktoba 7 zilikuwa zinapita upesi sana nami nilikuwa sijapokea bado habari hizi za maana kutoka kwa Ndugu Merck, niliendelea mbele bila msaada wake nikafanya mipango ya mkutano utakaofanywa katika nyumba ya ndugu katika kitongoji cha Mainz, karibu watu 20 wakakaribishwa kwenye mkutano huo.
“Siku mbili kabla ya mkutano huo kuwapo ikawa lazima badiliko la haraka sana lifanywe, kwa kuwa nyumba ambayo tungalikutania ilikuwa mahali penye hatari. Baada ya ndugu na dada wote kujulishwa mahali papya, iligunduliwa kwa ghafula kwamba jamaa katika nyumba hii walikuwa pia wameonyesha uadui mkubwa wakatisha kuagiza mtu ye yote waliyemjua kuwa mmoja wa mashahidi wa Yehova akamatwe mara moja akikanyaga nyumba yao wakati wo wote ujao. Kwa hiyo ndugu ambao nyumba ilikuwa yao, ambao katika nyumba yao mkutano ungalipaswa kufanywa asubuhi yake, wakaomba ufanyiwe mahali pengine. Kwa hiyo, ikawa lazima kutembelea ndugu wote tena Oktoba 6, kuwajulisha mahali pa tatu pa mkutano saa tatu asubuhi iliyofuata. Lakini mahali gani? Kulielekea kutokuwa na uwezekano uliobaki. Baada ya kufikiri kwa njia ya sala nikaamua kukaribisha akina ndugu kwenye nyumba yangu ndogo ya kipainia, ingawa hii ilikuwa hatari.
“Nikarudi nyumbani nimechoka sana jioni ya Oktoba 6 nami nikapewa barua na mke wangu ambayo ilikuwa imeletwa usiku sana kuliko nyakati za kawaida za kuleta barua, ijapokuwa ilikuwa barua ya kawaida tu si ya pekee, ambayo ingalihitaji wakuu wa posta waagize iletwe wakati huo. Nikaifungua nikagundua ilikuwa barua ya Ndugu Rutherford. Ndugu Merck alikuwa ameileta kwangu pengine kwa sababu hakuweza kunipa mimi mwenyewe wakati ufaao.
“Walakini, njia ya kuileta ilikuwa uhakikisho kwangu kwamba barua hiyo ilikuwa kwanza imekwenda kwa Gestapo (polisi)—kama ilivyokuwa kwa barua zangu zote za faragha—na kwamba ndipo walikuwa wamepanga kuileta, kwa wazi wakidhani kwamba sikuwa najua lo lote juu ya shughuli hiyo. Walidhani ndipo ningefanya mipango ya maana kupatana na yaliyokuwa ndani ya barua wakati fulani wa usiku, ili waweze kutupata sote pamoja watukamate hila kujitahidi sana asubuhi itakayofuata. Kwa kweli, kulikuwa kumekuwa na wakati wa kutosha kuonya maafisa katika Ujeremani yote. Lingekuwa jambo jepesi kukamata mashahidi wa Yehova wote watakaokusanyika pamoja katika miji mbalimbali asubuhi itakayofuata.
“Nifanye nini? Nyumba yangu, iliyokuwa katika jengo lenye mkahawa pia, haikuwa salama kabisa. Wote waliokuwa wanaishi katika nyumba hiyo, walikuwa wapinzani wakali, isipokuwa dada ambaye jengo lilikuwa lake na ambaye chumba chake mwa kulala kilikuwa kimeungana na nyumba yetu. Kwa upande mwingine, hakukuwa na uwezekano mwingine wa ambapo tungeweza kukutania. Nikimtumaini Yehova kwa msaada, nikaamua kutofanya mabadiliko yo yote zaidi wala kutia akina ndugu na dada wasiwasi isivyofaa, ambao wengi wao waliishi katika jamaa zilizofarakana na wasiokuwa na wazo lo lote la kusudi la mkutano huo. Kwa ndani nilikuwa nimejitayarisha kukamatwa tena.
“Saa moja asubuhi ya Oktoba 7, ndugu wa kwanza walikuwa wamekwisha fika, mipango ikawa imekwisha fanywa kila mtu aje mwenyewe kwa zaidi ya kipindi cha saa mbili ili jambo hili lisionekane. Akina ndugu walifika mmoja mmoja, wote wakitazamia sana ambayo yangetokea, ingawa kwa kupatana na maagizo hawakuwa wamepashwa habari za sababu yenyewe ya mkutano. Lakini hakukuwa na ye yote kati yao asiyeona kwamba hii ingekuwa siku ya maana sana sana. Kila mtu, kutia na akina dada ambao wengi wao waume wao walikuwa wapinzani na ambao wengi wao walikuwa na watoto wa kuangalia, alinivuta kama mwenye uamuzi na nia ya kufanya lo lote ambalo wangeombwa kufanya katika faida za kushuhudiwa kwa jina la Yehova.
“Kufikia saa tatu kasoro dakika kumi kila mtu alikuwa amekusanyika katika chumba chetu kimoja cha kipainia. Mimi nilitazamia sana kuona Gestapo (polisi) wakija wakati wo wote katika gari kubwa watukamate sote. Kwa hiyo, nikaona yanipasa kueleza akina ndugu na kuwapa nafasi ya kujitenga wasishiriki katika mkutano ikiwa wanaogopa matokeo yanayoweza kuwapo. Nikawaambia hivi: “Hali ilivyo ni kwamba sote tunaweza kukamatwa dakika kumi zinazokuja. Mimi sitaki ye yote kati yenu aweze kunilaumu baadaye kwa kuwatia katika hali hii bila kuwapasha habari za uzito wake. Kwa hiyo, nawaombeni mfungue Biblia zenu kwenye Kumbukumbu la Torati 20.’ Nikasoma mstari wa 8: ‘Ni mtu gani aliye hapa tena mwenye hofu na moyo mnyonge? aende akarudi nyumbani kwake, isije mioyo ya nduguze ikayeyuka mfano wa moyo wake.’ Baada ya kusoma hili kwa waliokuwapo, nikasema: ‘Ye yote anayeona kwamba hali ni yenye hatari mno sasa ana nafasi ya kujitenga asishiriki katika mkutano.’
“Lakini hakuna ye yote, hata dada wenye waume wasioamini na watoto, aliyefikiria kujitenga kwa woga. Sasa lililofuata ni jambo mtu asiloweza kueleza kwa maneno. Wakati wa dakika chache zilizobaki kufika saa tatu kukawa kimya kabisa chumbani. Ilikuwa wazi kwamba wote waliokuwapo walikuwa wanakabidhi mkono wa Yehova wa ulinzi jambo hili katika sala ya kimya. Ikafika saa tatu. Na ingawa wazo liliendelea kutambaa akilini mwangu kwamba ‘Gestapo wataingia uani wakati wo wote sasa’ nikafungua mkutano kwa sala. Kwa ghafula sote tukajiona kwamba duara yenye nguvu ya ulinzi ilikuwa imewekwa kutuzunguka, ikitia ndani si ndugu waliohatirishwa Ujeremani tu bali pia ulimwenguni mwote ambao walikuwa wamekusanyika kupatana na maagizo katika nchi nyingi saa ile ile na ambao kwa kawaida walianza mikutano yao pia kwa sala, yote haya kwa kusudi la kuteta kwa Hitler juu ya ukatili kwa ndugu zao katika Ujeremani.
“Baadaye nikatolea akina ndugu hotuba nikirudia-rudia mawazo makuu ya hotuba iliyostahili kufikiriwa ya Ndugu Rutherford katika Basel nipate kutia ndugu wa Ujeremani moyo. Ilitoa uhakikisho wa Biblia kwamba, zijapokuwa hali zilizobadilika, hatukuwa tumewekwa huru na daraka letu mbele za Yehova kukusanyika pamoja kwa kawaida tujifunze Neno lake na kumsifu yeye, wala na wajibu wetu kutumikia kama mashahidi wake na kuujulisha Ufalme waziwazi.”
Kupatana na hatua iliyokuwa inachukuliwa na mashahidi wa Yehova katika Ujeremani wote, kila mtu katika kikundi akakubali kwa shauku barua inayofuata ipelekwe kwa serikali siku hiyo kwa utumaji uliohakikishwa:
“KWA MAAFISA WA SERIKALI:
“Neno la Yehova Mungu, kama lilivyoandikwa katika Biblia Takatifu, ndiyo sheria kubwa kupita zote, na kwetu sisi ndicho kiongozi cha pekee kwa maana sisi tumejitoa kwa Mungu na tu wafuasi wa kweli na wanyofu wa Kristo Yesu.
“Mwaka jana, na tofauti na sheria ya Mungu na kwa kuvunja haki zetu, mmetukataza sisi kama mashahidi wa Yehova tusikutane kujifunza Neno la Mungu tumwabudu na kumtumikia. Katika Neno lake yeye anatuamuru kwamba hatutaacha kujikusanya pamoja. (Waebrania 10:25) Yehova anatuamuru hivi: ‘Ninyi ni mashahidi wangu kwamba mimi ni Mungu. Kawaambieni watu ujumbe wangu.’ (Isaya 43:10, 12; Isaya 6:9; Mathayo 24:14) Sheria yenu na sheria ya Mungu zinapingana moja kwa moja, nasi, kwa kufuata uongozi wa mitume waaminifu, ‘inatupasa kumtii Mungu kuliko wanadamu,’ nasi tutafanya hivyo. (Matendo 5:29) Kwa hiyo hii ni kuwajulisheni kwamba kwa vyo vyote sisi tutatii amri za Mungu, tutakutana pamoja kwa funzo la Neno lake, nasi tutamwabudu na kumtumikia kama ambavyo ameamuru. Ikiwa serikali yenu au maafisa wenu watatufanyia jeuri kwa sababu tunamtii Mungu, basi damu yetu itakuwa juu yenu nanyi mtamjibu Mungu Mwenye Nguvu Zote.
“Sisi hatupendezwi na mambo ya kisiasa, bali tumejitoa kabisa kwa ufalme wa Mungu ulio chini ya Kristo Mfalme wake. Sisi hatutaumiza wala kudhuru ye yote. Tungefurahia kukaa katika amani na kufanya mema kwa wanadamu wote kadiri tulivyo na nafasi, lakini, kwa kuwa serikali yenu na maafisa wake wanaendelea kutulazimisha tusitii sheria iliyo juu zaidi ya ulimwengu wote, sisi tunalazimika kuwapeni taarifa ya kwamba kwa neema yake tutamtii Yehova Mungu na kumtumaini Yeye kabisa atukomboe na uonezi wote na waonezi wote.”
Kwa kuunga ndugu zao Wajeremani mkono kabisa, mashahidi wa Yehova duniani mwote walikutana Oktoba 7 wakapelekea serikali ya Hitler simu ya chini baada ya sala ya umoja kwa Yehova:
“Ukatili wenu kwa mashahidi wa Yehova unashtua watu wema wote wa dunia na kulidharau jina la Mungu. Acheni kutesa mashahidi wa Yehova; ama sivyo Mungu atawaharibu ninyi na chama chenu cha kitaifa.”
Jambo la kushangaza ni kwamba, ndugu wachache walikamatwa siku hiyo, ingawa Gestapo (polisi) walikuwa wamegundua lililopaswa kufanywa hata ikiwa ni katika dakika ya mwisho tu. Na turudie ripoti ya Ndugu Franke:
“Ujapokuwa uhakika wa kwamba zaidi ya nusu saa ilikuwa imepita tangu tulipokuwa tumemaliza mkutano kwa sala, hakuna ye yote wa Gestapo aliyekuwa ameonekana mpaka wakati huo. Sasa wa kwanza wakaanza kuondoka, kama hapo kwanza, hawa baada ya wale. Karibu ndugu wanane walikuwa wangali wapo nilipoondoka nikapande baiskeli yangu kuelekea kwenye mji jirani wa Wiesbaden nipelekee wakuu wa posta barua mimi mwenyewe. Barua hiyo ilikuwa imeandikwa wakati wa usiku ikaachwa Wiesbaden, ambako akina ndugu wangalipaswa kuwa wameituma ikiwa walikuwa wamekamatwa, kama nilivyotazamia sana. Nilipokuwa nikiendesha baiskeli kupita mlango wa bustani, wakili wa Gestapo akaja amepanda baiskeli lakini akakosa kunitambua. Ndugu wengine wanane walionywa wakakimbilia chumba mwa kulala kilichokuwa karibu cha Dada Darmstadt, dada ambaye nyumba ilikuwa yake. Maulizo ambayo wakili wa Gestapo aliuliza mke wangu alipokuwa anapekua nyumba yetu yalionyesha kwamba Gestapo walijua mambo yote juu ya mkutano wetu. Ijapokuwa hili, wala mimi wala ye yote wa ndugu wengine hakukamatwa siku hiyo. Ilikuwa miezi kadha tu baadaye nilipokamatwa mara ya pili na Gestapo waliponiambia walikuwa na barua ya Ndugu Rutherford.”
Ndugu wengine walipokuwa na shughuli wakitembelea jirani zao mara tu baada ya mkutano huo na kukaza fikira zao kwenye ufalme wa Mungu, kulikuwa na fadhaa nyingi katika afisi nyingi za posta nje ya Ujeremani. Hasa katika bara ya Ulaya, wakuu wa posta mahali pengi walikataa kukubali simu. Ndivyo ilivyokuwa katika Budapest. Martin Potzinger alihudhuria mkutano huko akaombwa apeleka simu hiyo (telegram) kwenye afisi ya posta. Yeye anasema hivi: “Simu ilikubaliwa, lakini kesho yake nikapashwa habari na afisi kuu ya posta nifike huko mwenyewe. Sote tulidhani Gestapo wangenipeleka kifungoni, wanifukuze nchini, na kwa njia hiyo wakomeshe utendaji wangu . . . lakini haikuwa hivyo. Niliambiwa tu Hungary isingepitisha simu hiyo nikarudishiwa pesa zangu.” Katika Doorn (Holland), ambako Kaiser Wilhelm II wa Ujeremani aliishi uhamishoni, afisi ya posta kwanza ilikataa kuipeleka simu, lakini baadaye ikampasha habari Hans Thomas, aliyekuwa ameipeleka kwao, kwamba ilikuwa imepelekwa na kwamba kufika kwake Berlin kulikuwa kumehakikishwa.
Namna barua, na hasa simu, zilivyomhusu Hitler inaweza kuonekana kwa ripoti iliyoandikwa na Karl R. Wittig, iliyoshuhudiwa na karani wa serikali katika Frankfurt (Main) Novemba 13, 1947:
“TANGAZO—Oktoba 7, 1934, nilimtembelea Dr. Wilhelm Frick kwa kuwa nilikuwa nimeamriwa nifanye hivyo hapo nyuma, naye wakati huo alikuwa Waziri wa Mambo ya Ndani wa Milki ya Ujeremani na Prussia, katika afisi ya kwao ya Milki ya Ujeremani, iliyokuwa Berlin, 6 am Koeningsplatz, kwa kuwa mimi nilikuwa mjumbe mkuu wa General Ludendorff. Nilipaswa nikubali mawasiliano, yaliyokuwa na jaribio la kumwomba General Ludendorff aache kuchukia serikali ya Nazi. Wakati wa mazungumzo yangu na Dr. Frick, kwa ghafula Hitler alitokea akaanza kushiriki katika mazungumzo. Mazungumzo yetu yalipokuwa lazima yawe juu ya hatua iliyochukuliwa kwa International Bible Students Association [mashahidi wa Yehova] katika Ujeremani mpaka sasa, Dr. Frick akamwonyesha Hitler simu kadha zikiteta juu ya mateso ya Serikali ya Tatu juu ya Wanafunzi wa Biblia, akisema hivi: ‘Wanafunzi wa Biblia wasiponyoka tutawachukulia hatua mara moja tukitumia njia kali zaidi kuliko zote.’ Hitler akasimama mara moja amekunja ngumi imara akapaza sauti akiwa amepandwa na hasira: ‘Jamii hii itang’olewa Ujeremani!’ Miaka minne baada ya mazungumzo haya niliweza kujisadikisha kwa niliyoona mwenyewe wakati wa miaka yangu saba ya kuwa katika kifungo cha kulindwa katika mahali pabaya pa kambi za mateso za Nazi katika Sachsenhausen, Flossenburg na Mauthausen—nilikuwa gerezani mpaka nilipofunguliwa na Washirika—kwamba kuhamaki kwa Hitler hakukuwa tisho la vivi hivi tu. Hakuna kikundi kingine cha wafungwa wa kambi za mateso zilizotajwa walioonyeshwa uwazimu wa ukatili na askari wa SS kwa njia hiyo kama Wanafunzi wa Biblia. Ulikuwa uwazimu wenye ukatili ulioonyeshwa na mfululizo usiokwisha wa mateso ya kimwili na akili, ambayo vifani vyake hakuna lugha yo yote ulimwenguni inayoweza kueleza.”
Tulipokwisha kumpelekea Hitler barua zetu, ndugu walikamatwa mfululizo. Mji walikokamatwa zaidi ulikuwa Hamburg ambako, siku chache tu baada ya Oktoba 7, Gestapo walikamata ndugu 142.
KAZI YA SIRI YATENGENEZWA
Tulipokwisha kumpasha Hitler habari katika barua yetu ya Oktoba 7 kwamba tungeendelea kutii amri za Mungu peke yake ijapokuwa marufuku yake, tukajaribu kupanga ndugu na dada wote hodari na wenye nia vikundi vikundi wakisimamiwa na ndugu mwenye kukomaa, arnbaye wajibu wake ulikuwa kuangalia na kuchunga kondoo za Bwana kwa moyo wote.
Nchi iligawanywa katika majimbo kumi na matatu, na ndugu mwenye sifa njema za uchungaji aliwekwa katika kila jimbo atumikie kama msimamizi wa jimbo wa utumishi, kama alivyokuwa akiitwa siku hizo. Hawa walipaswa wawe ndugu wenye nia ya kuvifikia vikundi hivyo vidogo kuwapa chakula cha kiroho, kuwategemeza katika utendaji wao wa kuhubiri na kuwatia nguvu katika imani yao, hata zikiwapo hatari. Vyeo hivyo vilijazwa na watumishi wasiojulikana kabisa na akina ndugu mpaka wakati huo, isipokuwa vichache tu. Walakini, walikuwa wamehakikisha kwamba walikuwa na nia ya kutiisha faida zao wenyewe kwa zile za Ufalme baada ya Hitler kupata mamlaka.
KUNAKILI “THE WATCHTOWER” NA KULIGAWA
Akina ndugu walinakili wakagawa nakala za The Watchtower mahali pengi mbalimbali katika Ujeremani yote. Kwa mfano, katika Hamburg Helmut Brembach aliendelea kugawia akina ndugu katika Schleswig-Holstein na Hamburg nakala ambazo yeye na mkewe walinakili usiku. Dada Brembach anaeleza maono yanayofuata kati ya mengi ambayo yeye na mumewe waliona:
“Ilikuwa alasiri kengele ya mlangoni ilipolia kwa ghafula lakini kwa sauti kubwa kuliko kawaida. Nilipofungua mlango nikaona wanaume watatu wamesimama hapo. Nikawaza wao ni akina nani. Mmoja wao akasema ‘Gestapo’ (polisi) na wote watatu walikuwa nyumbani tayari. Moyo wangu ukanidunda mpaka kooni nilipofikiria vitu vilivyofichwa nyumbani. Nikitetema kwa ndani kwa sababu ya woga, nikasali kwa Yehova.
“Kutokana na maoni ya kibinadamu lisingalikuwa tatizo kuona Watchtower zilizofungwa pamoja na vifaa tulivyotumia kuzitengeneza. Kwa kuwa jamaa nyingi ziliishi katika nyumba yetu, kutia na zile za maafisa wawili wa polisi, hakukuwa na mahali pa kuficha cho chote, hasa tukikumbuka kwamba vifaa vya maana—karatasi, mashine ya kunakilia, taipureta na wino, na pia vifaa vya kufungia—vyote vilikuwa vikubwa. Bila ya kujua namna ya kuficha vitu hivi visionekane na wasiopaswa kuviona—nasi tulivihitaji kila juma mbili—tukaamua kufunga kila kitu pamoja na kuvitia katika pipa letu la viazi, lililokuwa katikati ya orofa ya chini na ambalo ye yote wa wakaaji wengine wa nyumba angaliweza kuingia ndani. Kila mara tulipomaliza kutengeneza The Watchtower, tulirudisha kila kitu kwa uangalifu katika pipa hili, tukavifunika na magunia matupu kisha tukakusanya visanduku vitupu vya nyanya juu yavyo mpaka upande wa chini wa dari, tukitumaini kwamba, mabaya yakiongezeka kwa mabaya, wale wanaojaribu kutafuta kitu ama wangekosa kukiona ama wangekuwa baridi mno na wavivu wasitake kuondoa kila kitu kilichokuwa juu ya pipa la viazi. Tukamtumaini Yehova; hatukuwa na jingine tuliloweza kufanya.
“Afisa akaniuliza kama tulikuwa na vitabu vyo vyote vilivyopigwa marufuku nyumbani. Ili kuepuka kusema uongo, nikasema: ‘Tafadhali jiangalilie pote mwenyewe.’ Wakapekua nyumba, wakifungua mlango wa kabati kwa njia ambayo walikosa kuiona taipureta, tuliyokuwa tumesahau kuiondoa kuitia ndani ya pipa na ambayo wangaliijua kuwa mashine iliyohitajiwa kuandikia The Watchtower, kama wangaliiona. Lakini Yehova aliwapofusha. Baada ya kutoona cho chote nyumbani, wakauliza kama wangeweza kupekua orofa ya chini. Sasa nikaona vifaa vyote na maandishi yote yasingekosa kuonekana. Nikajaribu kuficha wasione nina woga ijapokuwa moyo wangu ulikuwa unadunda-dunda hata zaidi. Isitoshe, sanduku la kuchukulia nguo lililojaa Watchtower, ambalo mume wangu angechukua kesho yake akiwa safarini, lilikuwa pale pale nyuma ya pipa. Lakini ikawaje? Maafisa watatu wale walisimama chumbani katikati, ebu wazia, pale pale lilipokuwa pipa sanduku lililojaa Watchtower likiwa nyuma yake. Lakini hakuna ye yote kati yao aliyeelekea kuliona; ilikuwa kana kwamba walikuwa wamepofushwa. Hakuna ye yote kati yao aliyefanya jitihada zo zote za namna yo yote kutazama pipani wala hata kuona kilichokuwa sandukuni. Mwishowe mmoja wa maafisa akauliza juu ya orofa yetu ya juu kabisa; huko wakaona vitabu kadha vikukuu, vilivyoelekea kuwaridhisha, kwa hiyo wakaenda zao. Lakini shukrani kwa msaada wa Yehova na ule wa malaika zake, vitu vilivyo vya maana zaidi hawakuviona.”
Visa vingi kama hivi vingeweza kuelezwa vikionyesha uongozi wa Yehova katika kusalimisha utendaji huu wa kunakili kwa vipindi virefu na hivyo kugawia watu wake vitabu.
(Inaendelea)
—Kutoka 1974 Yearbook of Jehovah’s Witnesses.