Historia ya Mashahidi wa Yehova katika Nyakati za Kisasa
—Ujeremani
AFISI ya tawi ya Watch Tower Society katika Wiesbaden imekuwa na kazi nyingi kwa sababu ya kazi inayofanywa na mashahidi wa Yehova katika Ujeremani yote. Kwa sababu vitabu vyao vinatoka hapa, akina ndugu wanapendezwa nayo sana, na idadi kubwa wanakuja kutembelea makao ya Betheli na kiwanda chake. Ndugu anayefanya kazi katika meza ya ukaribishaji anaweza kukueleza namna maelfu ya wageni wanavyotembezwa katika makao yote ya Betheli na kiwanda, hasa nyakati za sikukuu. Wakati mmoja zaidi ya 4,000 walikuja. Mabas 51 yalikuwa yamesimama nje! Ndugu wa nchi nyingine wanafurahia pia kupitia hapa kutuona. Miaka kadha iliyopita mwungwana mmoja alitembelea Betheli na baadaye akatiwa moyo aanze kujifunza Biblia. Ndugu mmoja wa Betheli akaanza kuandikiana barua na mwungwana huyo na baadaye akaikubali kweli, akabatizwa, akaingia utumishi wa wakati wote na leo anatumikia kama mwangalizi wa mzunguko.
Mwaka wa 1968 Ndugu Knorr alitembelea Wiesbaden mara mbili. Ziara yake ya kwanza ilikuwa Juni naye akafurahisha jamaa kwa kutangaza kwamba mashine mpya ya uchapaji ya kuzunguka na mashine nyingine tatu za kufungia vitabu zitanunuliwa ziwe za kiwanda chetu. Muda mfupi baada ya hapo mbili za mashine hizo zililetwa zikaanza kazi. Wakati wa ziara yake ya Novemba Ndugu Knorr alifanya mipango mingi kuongeza kazi tuliyokuwa tukifanya kiwandani. Ndugu wakaanza kufanya kazi ya zamu, kumi na tano au ishirini hivi wakawa wakifanya kazi usiku. Ndugu Knorr alikuwa ametuonyesha ubora wa kuendeleza hali ya kiroho, kwa hiyo kundi la pekee lilianzishwa kwa faida ya ndugu wenye zamu ya usiku, ambao kama wasingalifanyiwa hivyo wasingaliweza kuhudhuria mikutano. Mikutano yao ilifanywa mchana.
Mwanzoni mwa mwaka wa utumishi wa 1973 walikuwako watangazaji wa habari njema 95,975 katika Ujeremani ya Magharibi na Berlin ya Magharibi, nao uchapaji wa vitabu vya kutimiza mahitaji yao ulifikia vilele vipya. Wakati wa mwaka wa utumishi vitabu vipya kumi na saba vilichapwa vikafungwa katika kiwanda cha Wiesbaden; vingine kati yavyo vilikuwa vya Ujeremani na vingine vya nchi za Scandinavia na Netherlands. Ebu wazia jamaa ya Betheli ilivyosisimuka wakati jumla ya vitabu vilivyochapwa ilipoonekana kuwa 3,500,000 kwa mwaka mmoja tu!
AMANI DUNIANI—LAKINI KUPITIA KWA UFALME WA MUNGU PEKE YAKE
Huko nyuma mwaka wa 1939 usemi aliokuwa akitumia Hitler katika siku ya kila mwaka ya kusherehekea Serikali yake mpya ulikuwa “Amani.” Sarafu za ukumbusho na stampu za pekee zilitolewa kwa ajili ya hii “siku ya Amani ya Kusherehekea Serikali.” Lakini mwadhimisho ulifutwa kwa sababu ya kutokea kwa vita. Miaka 30 baadaye, Agosti 1969, katika Zeppelin Meadows katika Nürnberg, yaani, katika viwanja vile vile ambapo “Siku ya Amani ya Kusherehekea Serikali” ingaliadhimishwa miaka 30 iliyopita, “Amani Duniani” Kusanyiko la Mataifa Yote la Mashahidi wa Yehova lilifanywa.
Akiwa katika mnara mkubwa wa jiwe, ambapo viongozi wa Chama cha Nazi walikuwa wamefikiria kuwa na “utawala wa miaka elfu,” Ndugu Knorr alitoa hotuba ya watu wote yenye kichwa “Amani Ikaribiayo ya Miaka Elfu” kwa wasikilizaji 150,645. Lakini hakuwa akitia wasikilizaji wake moyo wafikiri-fikiri juu ya mambo ambayo wanadamu wanaweza kudai kufanya. Alikuwa akionyesha njia ya pekee ambayo kwayo amani ya milele itawajia wanadamu, yaani, ufalme wa Mungu ukiwa mikononi mwa Yesu Kristo. Na alionyesha kutokana na Maandiko kwamba kipindi hicho kinakaribia sana!
Nani ametokea akiwa mshindi? Si Ibilisi. Wala si ulimwengu ulio katika mamlaka yake. Bali, mashahidi wa Yehova wa Kikristo ndio wametokea wakiwa washindi, ambao wamemwamini Mungu wa pekee wa kweli na Mwanawe. Ni kama vile mtume Yohana alivyoandika: “Kila mtoto wa Mungu ni mshindi juu ya ulimwengu usiomcha Mungu. Ushindi uushindao ulimwengu ni imani yetu, kwa maana n’nani aliye mshindi juu ya ulimwengu isipokuwa yeye aaminiye kwamba Yesu ndiye Mwana wa Mungu?” (1 Yohana 5:4, 5, The New English Bible) Ni kweli, wengine wao walifia mikononi mwa adui za Mungu, lakini kwa kuwa walikuwa na tumaini la kuwa warithi pamoja na Kristo katika ufalme wake wa kimbinguni na kuishi wakati wa kuwapo kwake, walifufuliwa “kwa dakika moja, kufumba na kufumbua,” wakiwa wameushinda ulimwengu. (1 Kor. 15:51, 52) Wengine wenye tumaini la uzima wa kidunia katika taratibu mpya ya Mungu walilazwa kwa muda, wakisadiki kwamba Mungu asiyeweza kusema uongo atawafufua chini ya utawala wenye haki wa ufalme wake. Maelfu mengine wameokoka mashambulio makali ya Shetani na mawakili wake wanaoonekana, kwa msaada wa Mungu. Wengi wao wangali hai, wangali wakihubiri habari njema, wangali wakihakikisha ni waaminifu kwa Yehova. Nao wamekata shauri kuendelea katika mwendo huo wa uaminifu hata wapatwe na majaribu gani siku zijazo.
Acheni wote wanaosoma ripoti hii watiwe moyo nayo kuvumilia kwa uaminifu. Kumbukeni maneno haya ya mtume Paulo yaliyoongozwa na Mungu: “Na tufurahi katika dhiki pia; tukijua ya kuwa dhiki, kazi yake ni kuleta saburi; na kazi ya saburi ni uthabiti wa moyo; na kazi ya uthabiti wa moyo ni tumaini; na tumaini halitahayarishi; kwa maana pendo la Mungu limekwisha kumiminwa katika mioyo yetu na [roho takatifu tuliyopewa] sisi.” (Rum. 5:3-5) Itikio lenu kwa upendo wa Mungu na liwavute kufanya mapenzi ya Mungu kuwa jambo lililo la maana zaidi maishani mwenu, mkiwa na matumaini kamili katika Ushindi wa Kimungu ambao sasa unakaribia sana.
—Kutoka 1974 Yearbook of Jehovah’s Witnesses.