Twauhitaji Ufalme wa Mungu
HAKUJAPATA kamwe kuwa na uhitaji mkubwa wa badiliko halisi katika mambo ya kibinadamu kama ilivyo leo. Walio maskini na wenye njaa wanataka chakula, mahali pa kukaa na mavazi. Wanaoonewa kisiasa wanataka uhuru. Waliochoshwa na vita na chuki wanataka amani ya kweli. Wengi wanaoumizwa na uvunjaji wa sheria wanataka usalama. Wagonjwa wanataka afya njema.
Walakini watu wengi zaidi na zaidi wanafahamu kwamba faida wanazotaka haziwezi kupatikana kikweli hivi karibuni. Hata wengi wanaoishi katika nchi zenye utajiri mwingi zaidi sana wanaona hali yao ya maisha ikiharibiwa au kuangamizwa na kupanda kwa bei ya vitu na magumu mengine ya kiuchumi. Hivyo mwalimu wa chuo kikuu katika United States alisema: “Sioni tumaini lo lote!”
Serikali za wanadamu, hata ziwe zenye unyofu wa namna gani, haziwezi kuleta faraja ya kweli na yenye kuendelea kutokana na magumu makubwa sana ya leo. Mara nyingi wanafanya kinyume, na kama matokeo, watu wanapoteza tumaini na uhakika. Hakimu wa mahakma kuu katika Amerika aliyejiuzulu kazi alisema hivi: “Watu wanaanza kushuku kila mtu kwa sababu ya upotovu katika afisi za serikali.”
MAGUMU YANAONGEZEKA
Maisha katika taratibu hii ya mambo yanakuwa magumu zaidi kila mwaka, nayo matatizo yanakuwa makubwa zaidi. Mikazo hii inaongezeka kwa sababu ya kuongozeka kwa idadi ya watu ulimwenguni—kama milioni 70 au 80 kila mwaka sasa, ongezeko kubwa likiwa katika nchi ambazo tayari zimelemewa na matatizo yasiyotatuliwa.
Vilevile, jeuri inaongezeka ulimwenguni kadiri kutoridhika na kukata tamaa kunavyoongezeka. Gazeti Il Giornale la Italia lilisema hivi: “Dalili ya tabia ya nyakati zetu ni maelekeo ya jeuri.” Lilionyesha kwamba Vita ya Pili ya Ulimwengu ilitokeza vifo milioni 55 na kuleta huzuni isiyoelezeka, na vilevile likasema kwamba tangu ije amani katika mwaka 1945 kumekuwako na “vifo milioni 30 katika mapigano na mauaji ndani ya nchi moja moja.” Gazeti hilo liliongeza kwamba: “Mchafuko unaoenea ulimwenguni . . . umeenea katika jamaa na shuleni, unatikisa makanisa na mataifa mpaka misingi yake.”
Gazeti la Bolivia El Diario lilisema hivi juu ya ulimwengu huu: ‘‘Sasa twaweza kusema kwa nguvu na kwa kufaa kwamba, si kwamba tu hauna usawa, una wazimu. Sehemu kubwa za ulimwengu zimeambukizwa wazimu wa chuki.”
KUNA YE YOTE ANAYEJUA?
Kwa maoni ya kibinadamu hali ni mbaya sana hata kwamba padre mmoja wa United Church of Canada alisema hivi: “Hakuna awezaye kusema kwa uhakika kwamba katika wakati ujao kutakuja siku nzuri. Hakuna ajuaye kama ustaarabu utatoweka au kama mwishowe kutakuwako jamii mpya yenye maisha marefu kwa wote.”
Walakini huo ni uongo mtupu! Ukweli ni kwamba yuko Mtu anayejua kwa hakika! Na si kwamba Mtu huyo anajua tu, bali pia ana uwezo, hekima na nia ya kutaka kufanya mabadiliko yanayotamaniwa ili kutokeza taratibu mpya ambayo itatosheleza mahitaji ya wanadamu.
Mtu huyo ni Muumba wa dunia na mwanadamu. Katika njia ya mawasiliano ambayo ameongoza kwa roho ili kutuongoza, Neno lake, Biblia, yeye anasema hivi: “Nitangazaye mwisho tangu mwanzo na tangu zamani za kale mambo yasiyotendeka bado; nikisema [kusudi] langu litasimama, nami nitatenda mapenzi yangu yote.”—Isa. 46:10.
BADILIKO LINALOHITAJIWA LINAKUJA
Mungu ambaye makusudi yake hayakosi kutimia anatuambia kwamba badiliko kubwa sana litakuja bila shaka. Katika unabii aliouongoza juu ya wakati wetu, Neno lake linatoa maneno haya: “Na katika siku za wafalme hao Mungu wa mbinguni atasimamisha ufalme ambao hautaangamizwa milele, wala watu wengine hawataachiwa enzi yake; bali utavunja falme hizi zote vipande vipande na kuziharibu, nao utasimama milele na milele.” —Dan. 2:44.
Je! wewe ulifahamu kwamba ni kusudi la Mungu kuziondolea serikali zote za dunia zilizopo mamlaka, ‘kuziharibu falme hizi zote’ kabisa? Je! ulifahamu uhakika wa kwamba “Mungu wa mbinguni atausimamisha ufalme ambao hautaangamizwa milele”?
Ndiyo, kusudi la Mungu ni kuweka serikali nyingine mahali pa serikali zilizopo za kibinadamu. Hapana, si kwa mwungano mpya wa mataifa, wala kwa masalio ya Umoja wa Mataifa wa leo. Tofauti yake, ufalme wa Mungu utakuwa serikali yake ikitawala kutoka mbinguni, ambako hakuna mwanadamu awezaye kuichezea au kuiharibu.—Yohana 18:36.
Unabii huo unaonyesha kwamba serikali hii ya Ufalme itasaga-saga mpango wote wa utawala wa kibinadamu uliopo uwe mavumbi. (Dan. 2:35) Hiyo ni kutia na watu duniani wanaounga mkono taratibu hii, “waungwana kwa watumwa, wadogo kwa wakubwa.”—Ufu. 19:11-21.
Ni nani watakaookoka badiliko hilo kubwa sana la ulimwengu? Ufunuo unatabiri kwamba “mkutano mkubwa” utaokoka. Kwa sababu gani wanaokoka? Kwa sababu wamekuwa wakitolea Mungu “utumishi mtakatifu mchana na usiku.”—Ufu. 7:9-15.
Badiliko hilo la ulimwengu linalohitajiwa litatoa nafasi kwa taratibu mpya kabisa ya mambo. Ndiyo sababu mtume Petro angeweza kusema juu ya “mbingu mpya na dunia mpya ambazo sisi tunangojea kulingana na ahadi yake, na katika hizi haki itakaa.”—2 Pet. 3:11-13, NW.
Hivyo, yatakayotokea yanalingana na yale yaliyoelezwa na daktari wa akili Erich Fromm katika kitabu chake The Anatomy of Human Destructiveness. Yeye alisema kwamba hali yenye jeuri na kutoridhika katika jamii ya kibinadamu ingeondolewa ‘ikiwa tu mahali pa taratibu nzima ya kijamii na ya kisiasa kama vile imekuwa ikiendelea kwa muda wa miaka 6,000 iliyopita ya historia pangechukuliwa na taratibu nyingine iliyo tofauti kabisa.’
Ijapokuwa Fromm hakuwa akiufikiria ufalme wa Mungu, hata hivyo, utaleta ‘taratibu nyingine iliyo tofauti kabisa,’ mahali pa taratibu iliyopo ya mambo. Hiyo itamaanisha jamii mpya ya kibinadamu hapa duniani, chini ya uongozi na mamlaka ya ufalme wa Mungu wa kimbinguni. Na chini ya utawala wa Ufalme huo, mahitaji yote na tamaa zote zinazofaa za watu wenye adabu nzuri zitatoshelezwa zaidi ya vile wanavyoweza kuwazia.
SABABU GANI MUDA MREFU HIVYO?
Sababu gani Mungu amengoja muda mrefu hivyo ili apate kuleta badiliko hili linalohitajiwa sana? Sababu moja ni kulijaribu dai la kwamba mwanadamu hahitaji uongozi wa Mungu ili apate kufanikiwa. (Mwa. 3:4-6) Walakini maelfu ya miaka iliyopita imeonyesha kabisa namna utawala wa kibinadamu usivyoweza kutosheleza mahitaji pasipo Mungu.
Kila namna ya serikali na jamii ya kibinadamu imejaribiwa. Sayansi na uvumbuzi wa juu sana umepata kutumiwa kusaidia. Walakini hakuna kitu ambacho kimepata kutatua matatizo ya kibinadamu, ambayo yameendelea kuwapo na kuzidi kuwa mabaya. Jambo ambalo limethibitishwa kuwa kweli pasipo shaka lo lote ni hili: “Njia ya mwanadamu haimo katika nafsi yake; kuelekeza hatua zake si katika uwezo wa mwanadamu.”—Yer. 10:23.
Yote hayo yanaonyesha kwamba twauhitaji ufalme wa Mungu ututawale. Na utakapochukua mamlaka kamili ya mambo ya dunia, utamaanisha nini kwako?