Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w80 11/15 kur. 22-24
  • Rwanda—Nchi Ambayo Subira ya Yehova Haikuwa ya Bure

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Rwanda—Nchi Ambayo Subira ya Yehova Haikuwa ya Bure
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1980
  • Vichwa vidogo
  • KUANZA BAADA YA KUCHELEWA
  • SUBIRA YA YEHOVA YATHAMINIWA
  • VIZUIZI VYASHINDWA
  • ROHO YA KUJINYIMA
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1980
w80 11/15 kur. 22-24

Rwanda​—Nchi Ambayo Subira ya Yehova Haikuwa ya Bure

KORONGO wenye vishungi vya rangi ya manjano wanakula chakula chao cha asubuhi katikati ya mafunjo kando-kando ya chanzo kinachopinda-pinda huko Niabarongo cha Mto Nailo ulio mkubwa. Karibu na hapo, matawi ya migomba yanatoa uvuli juu ya maduka machache madogo yaliyo kando-kando ya barabara moja ya mawe. Mihogo, mihindi, mibuni (miti ya kahawa), maharagwe na mazao mengineyo ya shamba yanapamba pande za mitelemko ya vilima, katikati yake mkiwamo nyumba zenye kutapakaa na mashamba yazo. Nyumba hizo zilizojengwa kwa matofali yaliyofanywa kuwa magumu na kufunikwa kwa vigae vya paa vya rangi nyekundu, zinavutia sana pamoja na kuta zake zilizopigwa lipu nyeupe au ya manjano.

Katika pande za vilima vyenye majani ya chanikiwiti (kijani-kibichi), wanawake waliovaa mavazi mekundu wanafanya kazi kwa bidii mashambani, huku mbuzi wachache na ng’ombe wenye pembe ndefu wakiwa kwenye wanja ndogo za malisho. Pakiwa katika mwinuko wa metre zipatazo 1,600 (futi 5,250) juu ya usawa wa bahari, hewa yake ni yenye kutia nguvu. Kule-e-e, vikiwa vimefunikwa kidogo na mawingu meupe, vilele vya vilima vya Virunga vyenye volkeno vinaipamba mandari hiyo.

Hapa ni Rwanda, nchi ambayo subira ya Yehova haikuonyeshwa bure. Katika kimojawapo cha vijia vingi, kikiwa kingali kinateleza kidogo baada ya mvua ya usiku, zaidi ya watu wazima sita pamoja na vijana wanapitia. Ni Jumamosi asubuhi, nao wako safarini ya kilometres 25 (maili 16) kuelekea Kigali, mji mkuu wa Rwanda. Wanakusudia kuhudhuria huko mikutano ya Kikristo ya kila juma na kufaidika na mafunzo ya Biblia ya binafsi. Kupendezwa kwao na kweli ya Kimaandiko kuliamshwa na mwanamke kijana kutoka katika sehemu yao ya nchi, baada ya yeye kufikiwa na ujumbe wa Ufalme huko Kigali. Wao ni kati ya watu mmoja mmoja katika Rwanda wanaothamini subira ya Yehova katika hizi “siku za mwisho.”​—2 Pet. 3:9; 2 Tim. 3:1.

KUANZA BAADA YA KUCHELEWA

Ni wakati wa karibuni tu Ukristo wa kweli ulipokuja Rwanda. Rwanda, nchi ndogo, yenye kusambaa (kuenea) kilometre za mraba 26,338 (maili za mraba 10,169) peke yake, ni nchi isiyo na bandari nayo imo ndani ndani ya Afrika. Idadi yake ya watu inayozidi milioni nne na nusu inatumia karibu kila kisehemu cha nchi kilichoko katika maelfu ya vilima vyake vyenye majani ya rangi ya chanikiwiti. Mpaka hivi karibuni, walipokuwa chini ya uongozi wa matengenezo machache ya kidini ya Jumuiya ya Wakristo, watu wamepata kuona njaa ya kiroho. (Amosi 8:11) Hata hivyo, katika mwaka 1971, watangazaji wa Ufalme watatu wa kigeni walianza kazi yao hapa, wakikaza fikira zao sana sana juu ya idadi ndogo ya watu wenye kuzungumza Kiswahili. Kufikia mwaka 1974 hesabu yao ilikuwa imeongezeka na kuwa 14, lakini kati yao walikuwa Wanyarwanda wachache sana. Tangu wakati huo, uhuru mwingi zaidi wa kidini umekuwako Rwanda, na mashahidi kadha wa Yehova wenye kuzungumza lugha ya Rwanda yenye kuzungumzwa na watu wengi, yaani, Kinyarwanda, wamejiunga pamoja nao.

Kati yao ni mwanamume mmoja mwenye jamaa ambaye, kama Wanyarwanda wengi, alikuwa akifanya kazi katika mashimo ya madini ya shaba katika Shaba (mbeleni iliitwa Katanga) katika kusini mwa Zaire. Mwanamume huyo alikuwa ametafuta kweli na mwishowe akaipata mwishoni mwa mwaka 1960 na kitu. Wengine walipoondoka alipata nafasi za kushiriki katika madaraka ya kundi na kwa njia hiyo akapata haraka sana ujuzi uliohitajiwa ili kuwa mchungaji wa kiroho mwenye kusaidia. Hata hivyo, mawazo yake na sala pia zilielekezwa Rwanda mara nyingi, huko mbali nyumbani kwake ambako hakuna mtu ye yote aliyekuwa akisikia “habari njema.” Muda mfupi baadaye, mwalimu wa mtaala maalum (pekee) uliotolewa kwa ajili ya waangalizi wa Kikristo alimtia moyo aingie katika kazi ya kuhubiri wakati wote katika nchi ya nyumbani kwake. Uwezekano huo ulifanya moyo wake ufurahi, kwa hiyo wala kupandishwa cheo kazini karibuni karibuni tu wala kuvunjwa moyo na watu wa ukoo, vyote hivyo visingeweza kumzuia. Yeye na mkewe waliuona mkono wa Yehova, kwa kuwa karatasi zilizohitaji kujazwa zilimalizwa kwa muda mfupi ajabu na kampuni hiyo aliyoifanyia kazi ikampa tikiti za kuruka kwa ndege mpaka Rwanda. Ujuzi wake katika kazi ya kufanya wanafunzi umechochea utendaji kweli kweli huku, pamoja na kazi ya bidii ya Mashahidi wengineo wenye juhudi.​—Mt. 28:19, 20, NW.

SUBIRA YA YEHOVA YATHAMINIWA

Wengi wa watangazaji wapya wa Ufalme wa Rwanda walikuwa washiriki wenye bidii wa dini nyingine hapo kwanza. Sasa wanaonyesha kuthamini sana subira ya Yehova, wakifanya maendeleo haraka na kujitahidi kutangaza “habari njema,” mara nyingi kama wainjilisti wa wakati wote. Mifano michache itaonyesha jambo hilo.

Mwinjilisti wa dini ya Pentekoste alimhurumia mhubiri kijana aliyekuwa painia wa pekee katika mji wake naye akaamua ‘kumnyosha.’ Walakini mazungumzo yaliyofuata yalikuwa na matokeo tofauti. Mwinjilisti huyo alimwendea kasisi wake akiwa na maulizo 18 ya mafundisho ya kidini, lakini kiongozi huyo wa kidini hakuweza kuyajibu vizuri. Mwinjilisti huyo alipoanza kujifunza Biblia pamoja na Mashahidi wa Yehova, kukatokea vitisho vya kumwua, pamoja na namna nyingine za upinzani. Mke wake akataka kumtaliki naye akashirikiana na adui zake, lakini msimamo wake ukabadilika siku moja. Mke huyo alipokuwa akisikiliza kutoka “chumba cha sala” nyumbani huku funzo la Biblia likiongozwa, alisikia Shahidi huyo akimshauri mume wake asiwe akimpiga. Wazia mshangao wa mume wake siku moja alipomkuta mke wake akimtolea ushuhuda kasisi! Si kwamba tu mume na mke waliunganishwa kama waabudu wa kweli, bali pia washiriki wengine watano wa jamaa walitumia subira ya Yehova kwa faida yao.

Mmojawapo wa watu hao wa ukoo alikuwa ni kijana mwanamume mwenye uwezo wa kufanya mambo aliyetumwa na kanisa “aokoe” mjomba wake. Baada ya mazungumzo ya saa tano pamoja na Shahidi huyo aliyeongoza funzo la Biblia pamoja na yule aliyekuwa mwinjilisti hapo kwanza, yajapokuwa hayo, mpwa huyo alipanga kisiri kwamba funzo la Biblia la kibinafsi liongozwe kila siku, mradi mjomba wake asingearifiwa juu ya jambo hilo. Walakini siri hiyo ilitobolewa wakati mjomba wake alipoingia wakati funzo lilipokuwa likiendelea. Lo! alifurahi kama nini kwamba mpwa wake alikuwa akijifunza! Baada ya ubatizo wao wa Kikristo, mwanamume huyo pamoja na mpwa wake wakawa mara moja mapainia wasaidizi na baada ya muda usio mrefu, wakawa mapainia wa kawaida (wahubiri wa Ufalme wa wakati wote). Tangu wakati huo wamehamia eneo lililo peke yake, ambapo wengine wa watu wao wa ukoo na wengine wamekuwa wenye kuitikia sana “habari njema.” Lo! ni furaha kama nini kwao kuona kundi jipya likianzishwa huko, kukiwa na zaidi ya watu 30 wenye kuhudhuria mikutano kwa ukawaida!

Katika kisa kingine, mwalimu wa shule ya msingi alisikia kwamba mwanamume fulani mjini alikuwa akilipinga fundisho la Utatu. Utafiti (kutaka kujua) wake uliamshwa, mwalimu huyo akaazimia kukutana na mtu huyo, na mazungumzo yaliyofanywa pamoja naye yaliongoza kwenye funzo la Biblia. Miezi minne baadaye, mwalimu huyo wa shule akawa ametambua kwamba alikuwa amekuwa sehemu ya taratibu ya kilimwengu ya dini ya uongo, ambayo alijitenga nayo mara moja, akifuatwa na washiriki wengine wawili wa jamaa yake.​—Ufu. 18:4.

Mwanamume huyo alipobatizwa kama shahidi wa Yehova, kanisa lake la hapo kwanza lilituma barua nchini pote kuonya washiriki wake juu yake. Walakini kuthamini uhusiano wake na Mungu kulimchochea awe painia msaidizi mara tu baada ya kubatizwa, kisha utumishi wa painia wa kawaida muda mfupi tu baadaye. Jambo hilo likatokeza badiliko lingine kubwa maishani mwake. Alilazimika kuacha cheo chake cha kufundisha chenye kuheshimiwa na kurudia maisha ya chini zaidi kama mkulima. Kwa kuwa Rwanda ina idadi kubwa ya watu waliosongamana na “asilimia” yapata 97 ya wakaaji wake wanashiriki katika ukulima, kazi za kilimwengu ni chache nazo zaonwa kuwa za thamani sana. Hata hivyo mwanamume huyo kijana alipata furaha nyingi zaidi kuliko hapo mbeleni, kutia ndani furaha ya kuona wanafunzi wake kadha wa kadha wa Biblia wakibatizwa.

Mwalimu mwingine, akiwa anaishi mwendo wa nusu siku kutoka kwenye mji ulio karibu zaidi, aliusikia ujumbe wa kweli alipokuwa akitembelea mji wa Rwanda wenye chuo kikuu. Kwa sababu ya kuwa peke yake na gharama kubwa ya kusafiri, ilikuwa lazima funzo la Biblia liongozwe kwa njia ya barua, likifanikishwa na ziara mbili tu za mtu binafsi katika miezi yote hiyo. Walakini hayo yalitosha kumchochea awaambie jirani, rafiki na baadhi ya wanafunzi wake “habari njema.” Muda si muda, mkewe akalikubali tumaini hilo pia.

Karibuni mtu huyo akakabiliwa na uamuzi: Acha kuhubiri au upoteze kazi yako. Uamuzi wake ulikuwa wazi; yeye angeendelea kuwaambia wengine juu ya ufalme wa Mungu. Wengine walimwonya kwamba angepungukiwa na chakula. Hata hivyo, si kwamba tu maisha ya jamaa na afya yake yalikuwa bora zaidi tu, bali vilevile anaendelea vizuri zaidi kiroho. Wengine kati ya watu wa ukoo wake wamekuwa raia za ufalme wa Mungu, pamoja na baadhi ya waliokuwa wanafunzi wake. Na kwa msaada wa painia wa pekee, kundi jipya limeanzishwa hivi karibuni katika eneo hilo. Kwa kuangalia nyuma, mtu anaweza kuona thamani kubwa ya funzo la Biblia kupitia kwa barua mahali ambako ziara za mtu binafsi haziwezekani.

VIZUIZI VYASHINDWA

Mitego ya kidini, upinzani, matatizo ya kazi na kuwa katika eneo lililo peke yake, yote hayo yameshindwa na wengi ambao wameitikia Ukristo wa kweli katika Rwanda. Matatizo mengine ambayo yameshindwa ni pamoja na uasherati, kuzoea sana tumbako na kulewa kupindukia. Ukabila ungali ni tatizo lingine ambalo Wakristo wamelazimika kushinda.

Halafu, pia, kuna ibada ya mababu waliokufa na sherehe kama hizo. Rugo (nyumba na uwanja wake ulio wa mviringo wa yai na kuzungukwa na boma la miti) ina kanyumba kadogo kalikotengezwa hasa kwa ajili ya mababu waliokufa. Watu wengi wangali wanatoa sadaka (matambiko) ambazo ni pamoja na damu na pombe. Vitendo vilivyo wazi zaidi vya ibada ya mashetani (mizimu) vinaonekana katika visa vinavyohusu mauti, magonjwa na matatizo ya mali. Kwa kawaida, mazoea hayo yanaachwa na wale wanaoikubali ibada safi ya Yehova.

Kwa mfano, mwanamume kijana mwenye jamaa aliachana na uchawi. Akiwa mwanafunzi mwenye bidii wa uchawi, alikuwa amekaribia kufikia hali ya kuwa mchawi. Karibu nusu ya malipo yake ya kila mwezi yalikuwa yakitumiwa kununua ngozi za chui, meno ya simba, nywele za ndovu (tembo), vinywaji na vitu vingine vingi vinavyohusiana na uchawi. Hata katika siku ya kufanya arusi kwa kujitoa sana aliomba mizimu (mashetani). Hata hivyo alipatwa na ugonjwa na baadaye hata na mkewe pia.

Baada ya kuonana kifupi na Mashahidi wa Yehova, mke wa mwanamume huyo alivutiwa sana na kuona jina “Yehova” katika Yeremia 16:21 katika Biblia yake ya Kinyarwanda na kwa hiyo akawaalika Mashahidi hao nyumbani mwao. Kupendezwa kuliamshwa, na siku moja wenzi hao wawili walihudhuria mkutano wa Kikristo ambao katika huo hotuba ilitolewa kuhusiana na uchawi na hali ya waliokufa. Habari hiyo ilimgusa moyo sana mwanamume huyo. Akaenda nyumbani, akakusanya vyombo vyake vyote vilivyohusiana na ibada ya mizimu​—vifaa vyenye thamani ya zaidi ya shilingi 1,750 (Z583)​—naye akavichoma moto, kazi ambayo ilimchukua saa tatu na nusu. (Linganisha Matendo 19:18, 19.) Wenzi hao walishangaa kama nini kuona afya yao ikiwa nzuri zaidi baada ya jambo hilo! Siku nyingine, mwanamke mmoja aliwatembelea na, baada ya kusikia “habari njema,” akajisikia huru baada ya miaka mingi ya kutawaliwa na mashetani. Naye akaanza kujifunza Biblia na kuhudhuria mikutano ya Kikristo pamoja na mume wake. Wakati wote huo, mwanamume yule kijana mwenye jamaa akawa amefanya mabadiliko mengine maishani mwake na kuonyesha kujiweka kwake wakf kwa Yehova, ambaye amemwonyesha subira na rehema hizo.

ROHO YA KUJINYIMA

Inachangamsha moyo kuona roho ya juhudi, kuthamini na nia ya kujinyima inayoonekana kati ya hao ambao wameanza kuonja hivi karibuni fadhili za upendo za Yehova. Mwanamume mmoja alikuwa na fedha zilizotosha tu kulipia nauli ya kwenda tu kwenye kusanyiko la mzunguko. Kwa hiyo akaanza kutembea. Baada ya kiliometre 65 (maili 40) alizotembea kwa miguu alifika nusu ya safari yake naye akapata njia ya kusafiri kwenye kusanyiko hilo. Lo! alikuwa mwenye furaha kama nini kuwa hapo!

Hata wakati njia za kusafiria zinapopatikana, mara nyingi motokaa hizo si starehe. Huenda mtu akalazimika kubebwa nyuma ya lori au juu ya mzigo wa makaa, kuni, sukari au vinywaji vilivyo ndani ya chupa. Kwa ujumla madereva wanahakikisha kwamba nafasi yote inatumiwa, wakisongamanisha watu 50 nyuma ya kagari kadogo kasikofunikwa juu​—ala, kwa malipo! Kuongezea kwa hayo kutupwa-tupwa huku na huku katika barabara ya mawe, pamoja na mvua inayonyesha pindi kwa pindi, nawe waweza kupiga picha akilini namna kusafiri kulivyo, katika visa vingi. Walakini Wakristo wamesafiri hivyo bila kulalamika ili wapate furaha nyingi na kuburudishwa kwenye makusanyiko yao ya mzunguko.

Kusafiri toka Rwanda kuja kwenye kusanyiko la mataifa yote la mwaka 1978 katika Nairobi, Kenya, lilikuwa jambo gumu sana. Wale wahudhuriaji 29 wa kusanyiko hilo​—watu wazima na watoto pia​—walizuiliwa karibu siku nzima na wanajeshi katika Uganda, ambayo wakati huo ilikuwa ikitawalwa na Idi Amin. Mwishowe wakafika Nairobi, yajapokuwa hayo, wahudhuriaji hao walithamini sana kuhudhuria kusanyiko lenye kuthawabisha kiroho pamoja na waamini wenzao kutoka nchi 28.

Kuthamini mwangaza wa kweli na fadhili zisizostahilika za Yehova pia kwaonekana wazi katika roho ya “upainia” ya wahubiri wengi wa Ufalme katika Rwanda. Kwa wastani, kila mhubiri asiyekuwa katika kazi ya kuhubiri wakati wote anatumia kati ya saa 20 na 25 kila mwezi akiwaambia wengine “habari njema” na kuongoza zaidi ya funzo moja la Biblia la kila juma pamoja na watu wenye kupendezwa. Na mara hii na nyingine imetokea kwamba mhubiri mpya ameripoti zaidi ya saa 50 za utendaji wa kiinjilisti na mafunzo ya Biblia matatu, manne au hata matano wakati wa mwezi mmoja!

Walakini kazi nyingi ya kuhubiri Ufalme ingali yabaki kufanywa katika nchi hii ndogo, inayopendeza ya Waafrika. Akiruka kwa ndege juu ya Rwanda, mtu huona nyumba nyingi zilizotapakaa. Isipokuwa tu nyanda zenye maji ya kutosha za Akagera National Park katika mashariki, watu wengi huishi kando ya mito yenye maji yaliyosimama mahali pamoja, juu ya vilima vya mviringo, karibu na mashamba ya michai ya chanikiwiti, kando-kando ya misitu ya milima yenye mvua, sehemu nyingi za ardhi zilizozungukwa na maziwa yenye kuvutia na juu ya pande za vilima vilivyoinuka, hata kufikia makao ya sokwe-mtu wakubwa wa milimani juu ya pande zenye misitu za volkeno za Virunga. Jitihada zinafanywa ili kufikia wengi wa watu hawa kama iwezekanavyo, kwa kuzuru nyumba zinazofikika na kwa kukutana nao wakati wa siku za soko.

Mashahidi wa Yehova hapa wanashukuru sana kwa ajili ya subira ya Mungu na kwa ajili ya nafasi zao za kusaidia wengine bado ili waitumie kwa faida yao. Subira ya Mungu kwa hakika yaweza ‘kuonwa kuwa wokovu’ kwa wengi, kama inavyoshuhudiwa na umati mkubwa wa waabudu wa Yehova katika Rwanda.​—2 Pet. 3:15.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki