Kutangaza Ukweli Katika Misafa ya Milima Mirefu ya Austria
AUSTRIA ina haki ya kujulikana sana kwa yale majani mabichi-mabichi ya misafa ya milima mirefu ya huko, ile Miitu ya Vienna, na kwa Danube ule mto wa kupendeza wenye maji buluu. Miono hiyo na mingine inayojulikana sana inavutia watu wenye kuzuru kutoka sehemu zote za ulimwengu ili waje kwenye nchi ndogo hii iliyo katikati ya Ulaya.
Majira ya utalii yalipokuwa katika kilele Agosti uliopita, kikundi kimoja cha watu karibu mia moja wenye kuzuru kutoka nchi 17 za kigeni kilikuja kuona kitu tofauti kabisa. Wao walikuja Vienna kuhudhuria kuwekwa wakfu kwa ile afisi ya tawi la Austria iliyo mpya, ya Sosaiti ya Mnara wa Mlinzi, ambayo inaelekeza kazi ya kuhubiri Ufalme ya Mashahidi wa Yehova katika Austria.
Kutoka Mwanzo Mdogo
Afisi ya tawi ya Sosaiti iliyo ya kwanza katika Austria ilianzishwa Vienna katika 1923, Hiyo ilikuwa chini ya miaka kumi baada ya ziara ya kwanza kufanywa kwa waandikishaji wanne wa Mnara wa Mlinzi katika mji huo. Kufikia wakati huo hesabu ya watangazaji wa Ufalme ilikuwa imekua ikafika kama mia moja. Ndipo ilipokuja Vita ya Ulimwengu ya Pili na kuingia kwa Unazi, kipindi chenye majaribu na magumu makali kwa ndugu waaminifu. Lakini wao walivumilia, na kufikia mwisho wa vita hiyo hesabu yao ilikuwa imekua ikawa zaidi ya 700.
Katika 1957 jengo moja lilinunuliwa kule Gallgasse 44 ili kutunza kazi hiyo yenye kupanuka. Kadiri miaka ilivyopita, marekebisho kadhaa yalifanywa kwenye jengo hilo ili kuupatia nafasi ukuzi wa kazi ya Ufalme uliozidi kutokea barani. Kufikia 1973 hesabu ya wahubiri wa Ufalme ilipita ile alama ya 10,000. Hivyo, katika miaka ya mwanzo-mwanzo wa 1980, ramani zilitayarishwa za mpanuko. Mwishowe vizuizi vya kisheria viliondolewa, na nyanja zilizo kando-kando ya tawi zilipatikana. Katika Machi 1983 shirika moja la nje lilianza kazi ya muundo wa nje wa jengo. Baada ya hapo, akina ndugu ndio waliosonga mbele na kazi wakamaliza jengo hilo.
“Kujenga Betheli Yetu”
Mashahidi kutoka sehemu zote za Austria walijitolea kwa ajili ya kazi ile. Shime yenye kutumika ilikuwa kwamba “sisi tunajenga Betheli yetu.” Wao walikuja wakiwa katika magari na mabasi, wakafika 190 katika mwisho-juma mmoja. Ilikadiriwa kwamba mmoja katika kila wahubiri watano nchini alikuwa na ushiriki katika kazi ile. Baadhi yao walikuwa wataalamu—wastadi wa ramani za mijengo, mafundi wa mabomba, na mambo kama hayo. Wengine waliandaa vifaa au wakajitolea ili vyumba vyao vya kikazi vitumiwe. Baadhi yao hata waliacha kazi zao wakaja kufanya kazi kipindi chote cha ujenzi.
Ndugu mmoja aliyetumia sehemu ya likizo lake akiwa kwenye uwanja wa ujenzi aliandika hivi: “Mimi ningependa kuwapigia tena asante kwa lile juma zuri ajabu la likizo. Ilikuwa kama kuwa katika kisiwa cha utulivu kilichozungukwa na bahari ya wanadamu wenye msuko-suko. Ilikuwa vizuri sana kufurahia burudisho hilo la kimwili na kiroho bila gharama.” Hata wadogo-wadogo walikuwa na ushiriki. Mtoto wa miaka minane aliandika hivi: “Mimi nimesikia kwamba mnahitaji pesa kwa ujenzi wa Betheli. Mimi ningependa kuwapelekea ninyi kiasi fulani cha pesa ambazo nimeokoa. Nimetia ndani ya bahasha hii shilingi 200 [dola zipatazo 16 za United States].” Wengine walioka mkate, wakachuma matunda ya beri, na kutayarishia wenye kujitolea majimaji ya kunywa. Wahubiri katika yale makundi 36 ya Vienna waliandaa viburudisho kila Jumamosi katika kile kipindi chote cha ujenzi.
Kuwa na Vifaa kwa Ajili ya Ongezeko Zaidi
Baada ya kutengenezwa upya kwa lile jengo la awali na kuongezwa kwa mijengo mipya yenye kulizunguka, sasa tawi lina ukubwa ulio mara tatu za vile lilivyokuwa, likiwa na nafasi ya sakafuni ya meta za mraba 5,400. Hiyo ni kutia ndani vyumba 38, jumba la kulia chakula kwa watu 80, jiko jipya, na mahali pa kufulia nguo. Jumba la Ufalme jipya liko pale pale nyuma ya lile jengo la awali. Afisi za usimamiaji kazi na idara nyingine mbalimbali ndizo zinachukua sehemu iliyobaki ya majengo hayo.
Agosti 22, 1987, ilikuwa ndiyo siku ya wakfu kwa majengo mapya ya tawi. Miongoni mwa wale wageni 282 walikuwamo watu 100 wenye kuzuru kutoka matawi 16 ya Ulaya na mmoja kutoka Korea. Waliokuwapo pia ni wazee-wa-kazi Waaustria wapatao mia moja ambao walikuwa wameokoka majaribu ya Vita ya Ulimwengu ya Pili. Aliye na umri mkubwa zaidi miongoni mwao alikuwa Maria Hack wa miaka 102 kutoka Graz. Hadhirina ya wasikilizaji 6,810 wakiwa katika sehemu nyingine saba waliisikia pia programu ya wakfu kupitia miunganisho ya kamba za simu.
Wasemaji wakuu katika programu ya wakfu walikuwa ni kutia ndani T. Jaracz na M. G. Henschel wa Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova katika Brooklyn, New York, U.S.A. Akihutubu juu ya kichwa “Matawi Ambayo Yanazaa Tunda kwa Utukufu wa Yehova,” Ndugu Jaracz alitumia Yohana 15:2 na 8 kuonyesha kwamba “matawi” yanatumikia kwa utukufu wa Yehova wakati yanapozaa tunda jingi. Yale majengo mapya ya tawi yatachangia sana kutokeza tunda kwa utukufu wa Yehova.
Katika hotuba ya wakfu, Ndugu Henschel alikazia kwamba Yehova ni Mungu wa kusudi. Si kwamba tu yeye amejulisha mapema kusudi lake bali pia ameonyesha kwamba yeye ana uwezo wa kulitekeleza. Ujapokuwako upinzani wa Shetani, sisi tunaweza kuwa na uhakika kwamba kusudi la Mungu litatimizwa.
Programu ilipokuwa ikifikia mwisho, wote wenye kuwapo walihisi wametiwa moyo kuendelea na kazi ya kuhubiri wakiwa na sulubu iliyofanywa upya. Kwa uwazi, majengo yale mapya mazuri yatawatayarisha kwa vifaa Mashahidi Waaustria watangaze habari njema za Ufalme kwa kadiri kubwa hata zaidi katika nchi hii yenye misafa mirefu ya milima, kwa utukufu na sifa ya yule Muumba Mtukufu, Yehova.
[Pictures on page 23]
Jengo jipya, linavyoonekana kutoka bustani
Jumba la Ufalme
Mwingilio mkuu
Jengo jipya, huku ule mjengo uliotengenezwa upya ukiwa upande wa kulia