Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Karibu
Hiki ni kifaa cha utafiti katika machapisho ya Mashahidi wa Yehova ya lugha mbalimbali.
Ikiwa ungependa kupakua machapisho, tafadhali tumia anwani jw.org.
  • Leo

Ijumaa, Oktoba 10

Kumwogopa Yehova ndio mwanzo wa hekima.—Met. 9:10.

Tukiwa Wakristo, tunapaswa kufanya nini ikiwa picha ya ponografia itatokea bila kutarajia kwenye kifaa chetu cha kielektroni? Tunapaswa kuacha mara moja kutazama picha hiyo. Itakuwa rahisi kufanya hivyo ikiwa tutakumbuka kwamba uhusiano wetu pamoja na Yehova ndilo jambo lenye thamani zaidi kwetu. Hata baadhi ya picha ambazo hazionwi kuwa za ponografia zinaweza kuchochea hamu ya ngono. Kwa nini tunapaswa kuziepuka? Kwa sababu hatungependa hata kuwazia kufanya uasherati katika moyo wetu. (Mt. 5:​28, 29) David, mzee wa kutaniko anayeishi nchini Thailand, anasema hivi: “Mimi hujiuliza: ‘Ingawa picha hizo si ponografia, je, nitamfurahisha Yehova ikiwa nitaendelea kuzitazama?’ Kufikiria kwa njia hiyo hunisaidia kutenda kwa hekima.” Tutatenda kwa hekima ikiwa tutasitawisha woga unaofaa kwa kuepuka kufanya jambo linalomchukiza Yehova. Kumwogopa Mungu ndio “mwanzo,” au msingi, “wa hekima.” w23.06 23 ¶12-13

Kuyachunguza Maandiko Kila Siku—2025

Jumamosi, Oktoba 11

Nendeni, watu wangu, ingieni katika vyumba vyenu vya ndani.—Isa. 26:20.

Huenda ‘vyumba vya ndani’ vinarejelea makutaniko yetu. Wakati wa dhiki kuu, tutapata ulinzi ambao Yehova ametuahidi ikiwa tutadumisha umoja na waabudu wenzetu. Kwa hiyo, tunapaswa kujitahidi sasa, si kuwavumilia tu ndugu na dada zetu, bali kuwa na upendo mwingi kuwaelekea. Huenda wokovu wetu utategemea jambo hilo! “Ile siku kuu ya Yehova” itawasababishia wanadamu taabu. (Sef. 1:​14, 15) Watu wa Yehova pia watapatwa na mateso. Lakini ikiwa tutajitayarisha sasa tutafaulu kuendelea kuwa watulivu na kuwasaidia wengine. Tutavumilia matatizo yoyote ambayo tutakabili. Waabudu wenzetu wakiteseka, tutajitahidi kuwasaidia kwa kuwaonyesha huruma na kwa kuwaandalia mahitaji yao. Na tutakaa karibu na ndugu na dada zetu ambao tayari tumesitawisha upendo kuwaelekea. Kisha Yehova atatuthawabisha kwa kutupatia uzima wa milele katika ulimwengu ambao hautakuwa na msiba wala dhiki yoyote.—Isa. 65:17. w23.07 7 ¶16-17

Kuyachunguza Maandiko Kila Siku—2025

Jumapili, Oktoba 12

[Yehova] atawafanya muwe imara, atawatia nguvu, atawapa msingi imara.—1 Pet. 5:10.

Mara nyingi, Neno la Mungu huwafafanua wanaume waaminifu kuwa wenye nguvu. Lakini hata wale waliokuwa na nguvu zaidi miongoni mwao hawakuhisi kwamba wana nguvu sikuzote. Kwa mfano, pindi fulani Mfalme Daudi alihisi kwamba alikuwa “imara kama mlima,” lakini katika pindi nyingine ‘aliogopa.’ (Zab. 30:7) Ingawa Samsoni alikuwa na nguvu nyingi zisizo za kawaida alipochochewa na roho ya Mungu, alitambua kwamba bila kupata nguvu zinazotoka kwa Mungu, angekuwa dhaifu kama wanadamu wengine wote. (Amu. 14:​5, 6; 16:17) Wanaume hao waaminifu walikuwa na nguvu kwa sababu tu Yehova aliwapa nguvu. Mtume Paulo alisema kwamba yeye pia alihitaji nguvu kutoka kwa Yehova. (2 Kor. 12:​9, 10) Alipambana na matatizo ya kiafya. (Gal. 4:​13, 14) Pia, wakati mwingine ilikuwa vigumu kwake kufanya mambo yaliyo sawa. (Rom. 7:​18, 19) Na wakati mwingine alikuwa na wasiwasi na hakuwa na uhakika kuhusu mambo ambayo yangempata. (2 Kor. 1:​8, 9) Ingawa hivyo, Paulo alipokuwa dhaifu, alikuwa mwenye nguvu. Jinsi gani? Yehova alimpa Paulo nguvu alizohitaji. Alimwimarisha Paulo. w23.10 12 ¶1-2

Kuyachunguza Maandiko Kila Siku—2025
Karibu
Hiki ni kifaa cha utafiti katika machapisho ya Mashahidi wa Yehova ya lugha mbalimbali.
Ikiwa ungependa kupakua machapisho, tafadhali tumia anwani jw.org.
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki