Alhamisi, Oktoba 9
Msiuzime moto wa roho.—1 The. 5:19.
Tunaweza kufanya nini ili tupokee roho takatifu? Tunaweza kusali ili tupate roho takatifu, kujifunza Neno la Mungu lililoongozwa na roho, na kushirikiana na tengenezo lake linaloongozwa na roho. Kufanya hivyo, kutatusaidia kusitawisha sifa za “tunda la roho.” (Gal. 5:22, 23) Mungu huwapa roho yake wale tu ambao wanadumisha mawazo safi na mwenendo safi. Hataendelea kutupatia roho yake ikiwa tutaendelea kuwa na mawazo yasiyo safi na kutenda kulingana na mawazo hayo. (1 The. 4:7, 8) Ili tuendelee kupokea roho takatifu, pia hatupaswi ‘kuutendea unabii kwa dharau.’ (1 The. 5:20) Hapa “unabii” unamaanisha ujumbe uliotokezwa na roho ya Mungu, kutia ndani ujumbe kuhusu siku ya Yehova na uhitaji wa kutenda haraka katika nyakati zetu. Hatuahirishi siku hiyo katika akili zetu na kufikiri kwamba Har–Magedoni haitakuja tukiwa hai. Badala yake, tunaiweka karibu akilini kwa kudumisha mwenendo unaofaa na kuendelea kuwa na bidii katika “vitendo vya ujitoaji-kimungu.”—2 Pet. 3:11, 12. w23.06 12 ¶13-14
Ijumaa, Oktoba 10
Kumwogopa Yehova ndio mwanzo wa hekima.—Met. 9:10.
Tukiwa Wakristo, tunapaswa kufanya nini ikiwa picha ya ponografia itatokea bila kutarajia kwenye kifaa chetu cha kielektroni? Tunapaswa kuacha mara moja kutazama picha hiyo. Itakuwa rahisi kufanya hivyo ikiwa tutakumbuka kwamba uhusiano wetu pamoja na Yehova ndilo jambo lenye thamani zaidi kwetu. Hata baadhi ya picha ambazo hazionwi kuwa za ponografia zinaweza kuchochea hamu ya ngono. Kwa nini tunapaswa kuziepuka? Kwa sababu hatungependa hata kuwazia kufanya uasherati katika moyo wetu. (Mt. 5:28, 29) David, mzee wa kutaniko anayeishi nchini Thailand, anasema hivi: “Mimi hujiuliza: ‘Ingawa picha hizo si ponografia, je, nitamfurahisha Yehova ikiwa nitaendelea kuzitazama?’ Kufikiria kwa njia hiyo hunisaidia kutenda kwa hekima.” Tutatenda kwa hekima ikiwa tutasitawisha woga unaofaa kwa kuepuka kufanya jambo linalomchukiza Yehova. Kumwogopa Mungu ndio “mwanzo,” au msingi, “wa hekima.” w23.06 23 ¶12-13
Jumamosi, Oktoba 11
Nendeni, watu wangu, ingieni katika vyumba vyenu vya ndani.—Isa. 26:20.
Huenda ‘vyumba vya ndani’ vinarejelea makutaniko yetu. Wakati wa dhiki kuu, tutapata ulinzi ambao Yehova ametuahidi ikiwa tutadumisha umoja na waabudu wenzetu. Kwa hiyo, tunapaswa kujitahidi sasa, si kuwavumilia tu ndugu na dada zetu, bali kuwa na upendo mwingi kuwaelekea. Huenda wokovu wetu utategemea jambo hilo! “Ile siku kuu ya Yehova” itawasababishia wanadamu taabu. (Sef. 1:14, 15) Watu wa Yehova pia watapatwa na mateso. Lakini ikiwa tutajitayarisha sasa tutafaulu kuendelea kuwa watulivu na kuwasaidia wengine. Tutavumilia matatizo yoyote ambayo tutakabili. Waabudu wenzetu wakiteseka, tutajitahidi kuwasaidia kwa kuwaonyesha huruma na kwa kuwaandalia mahitaji yao. Na tutakaa karibu na ndugu na dada zetu ambao tayari tumesitawisha upendo kuwaelekea. Kisha Yehova atatuthawabisha kwa kutupatia uzima wa milele katika ulimwengu ambao hautakuwa na msiba wala dhiki yoyote.—Isa. 65:17. w23.07 7 ¶16-17