Jumanne, Oktoba 14
Waliiacha nyumba ya Yehova.—2 Nya. 24:18.
Somo moja ambalo tunaweza kujifunza kutokana na uamuzi mbaya wa Mfalme Yehoashi ni kwamba tunahitaji kuchagua marafiki ambao watatuchochea kufanya mambo mazuri—marafiki ambao wanampenda Yehova na wanaotaka kumfurahisha. Hatuhitaji kuchagua tu marafiki wenye umri kama wetu. Kumbuka kwamba Yehoashi alikuwa na umri mdogo sana kuliko rafiki yake, Yehoyada. Jiulize hivi kuhusu marafiki unaochagua: ‘Je, wananisaidia kuimarisha imani yangu kwa Yehova? Je, wananitia moyo kuishi kulingana na viwango vya Mungu? Je, wanazungumza kumhusu Yehova na kweli zake zenye thamani? Je, wanaheshimu viwango vya Mungu? Je, wananiambia tu mambo ambayo ninapenda kusikia au je, wana ujasiri wa kunirekebisha ninapokosea?’ (Met. 27:5, 6, 17) Kwa kweli, ikiwa rafiki zako hawampendi Yehova, huwahitaji. Lakini ikiwa una marafiki ambao wanampenda Yehova, shikamana nao—watakusaidia kufanya mambo yanayofaa!—Met. 13:20. w23.09 9-10 ¶6-7
Jumatano, Oktoba 15
Mimi ndiye Alfa na Omega.—Ufu. 1:8.
Herufi alfa ndiyo ya kwanza katika alfabeti ya Kigiriki, na herufi omega ndiyo ya mwisho. Kwa kusema kwamba yeye ndiye “Alfa na Omega,” Yehova anatusaidia kuelewa kwamba anapoanza kufanya jambo fulani, lazima alikamilishe kwa mafanikio. Baada ya kuwaumba Adamu na Hawa, Yehova alisema hivi: “Zaeni, muwe wengi, muijaze dunia na kuitiisha.” (Mwa. 1:28) Wakati huo ni kama Yehova alikuwa akisema “Alfa.” Alieleza waziwazi kusudi lake kwamba wakati utafika ambapo dunia itajaa wazao wa Adamu na Hawa walio wakamilifu na watiifu, ambao wataigeuza dunia kuwa paradiso. Wakati huo ujao, kusudi lake litakapotimia, ni kana kwamba atasema “Omega.” Baada ya kukamilisha uumbaji wa “mbingu na dunia na kila kitu kilichomo,” Yehova alitoa uhakikisho huu. Alitoa uhakikisho kwamba atatimiza kusudi lake kwa ajili ya wanadamu na dunia. Lingetimizwa kikamili mwishoni mwa ile siku ya saba.—Mwa. 2:1-3. w23.11 5 ¶13-14
Alhamisi, Oktoba 16
Fungueni njia ya Yehova! Tengenezeni barabara kuu iliyonyooka inayopitia jangwani kwa ajili ya Mungu wetu.—Isa. 40:3.
Safari ngumu kutoka Babiloni kwenda Israeli ingechukua miezi minne hivi, lakini Yehova aliahidi kwamba kizuizi chochote ambacho kingeonekana kuwa kinazuia safari hiyo kingeondolewa. Wayahudi waaminifu walijua kwamba ikiwa wangerudi katika nchi ya Israeli wangepata baraka nyingi kuliko jambo lolote ambalo wangedhabihu. Baraka kuu zaidi ilihusiana na ibada yao. Hakukuwa na hekalu la Yehova katika jiji la Babiloni. Hakukuwa na madhabahu ambayo Waisraeli wangetoa dhabihu zilizotajwa katika Sheria ya Musa, na hakukuwa na mpango wa makuhani ambao wangetoa dhabihu hizo. Isitoshe watumishi wa Yehova walikuwa wachache kwa kulinganishwa na idadi kubwa sana ya watu ambao waliabudu miungu ya uwongo, na ambao hawakumheshimu Yehova na viwango vyake. Basi, maelfu ya Wayahudi waliomwogopa Mungu, walitazamia kwa hamu kurudi katika nchi yao ambako wangerudisha ibada safi. w23.05 14-15 ¶3-4