Jumatano, Oktoba 1
Hekima inayotoka juu . . . [iko] tayari kutii.—Yak. 3:17.
Je, wakati mwingine ni vigumu kwako kutii? Mfalme Daudi alikabili changamoto hiyo naye alisali hivi kwa Mungu: “Chochea ndani yangu utayari wa kukutii.” (Zab. 51:12) Daudi alimpenda Yehova. Hata hivyo, wakati mwingine ilikuwa vigumu kwake kutii, na inakuwa hivyo pia kwetu. Kwa nini? Kwanza, tumerithi mwelekeo wa kutotii. Pili, sikuzote Shetani anajaribu kutuchochea tuasi, kama yeye alivyofanya. (2 Kor. 11:3) Tatu, tumezungukwa na ulimwengu huu wenye roho ya uasi, “roho ambayo sasa inafanya kazi katika wana wa kutotii.” (Efe. 2:2) Tunapaswa kujitahidi kushinda mwelekeo wetu wa kutenda dhambi na pia kupinga mkazo wa kutotii unaotoka kwa Ibilisi na ulimwengu huu. Tunapaswa kujitahidi kumtii Yehova na wale ambao amewapatia mamlaka. w23.10 6 ¶1
Alhamisi, Oktoba 2
Lakini wewe umehifadhi divai nzuri mpaka sasa.—Yoh. 2:10.
Tunaweza kujifunza nini kutokana na muujiza wa Yesu wa kugeuza maji kuwa divai? Tunajifunza somo kuhusu unyenyekevu. Yesu hakujigamba kuhusu muujiza huo; kwa kweli, hakujigamba kamwe kuhusu mambo aliyotimiza. Kinyume chake, kwa unyenyekevu, tena na tena alimpa sifa na utukufu Baba yake. (Yoh. 5:19, 30; 8:28) Ikiwa tutamwiga Yesu kwa kuwa wanyenyekevu, hatutajigamba kuhusu mambo tunayotimiza. Acheni tujigambe si kujihusu sisi wenyewe, bali kumhusu Mungu mwenye kustaajabisha ambaye tuna pendeleo la kumtumikia. (Yer. 9:23, 24) Acheni tumpe sifa anazostahili. Isitoshe, hatuwezi kamwe kutimiza jambo lolote zuri bila msaada wa Yehova? (1 Kor. 1:26-31) Tunapokuwa wanyenyekevu, hatujitafutii sifa kwa mambo mazuri tunayowafanyia wengine. Tunaridhika kujua kwamba Yehova anaona na kuthamini mambo tunayofanya. (Linganisha Mathayo 6:2-4; Ebr. 13:16) Kwa kweli, tunamfurahisha Yehova tunapomwiga Yesu kwa kuonyesha unyenyekevu.—1 Pet. 5:6. w23.04 4 ¶9; 5 ¶11-12
Ijumaa, Oktoba 3
Mkiangalia, si faida zenu wenyewe, bali pia faida za wengine.—Flp. 2:4.
Akiongozwa na roho, mtume Paulo aliwatia moyo Wakristo waangalie faida za wengine. Tunaweza kutumiaje shauri hilo kwenye mikutano? Kwa kukumbuka kwamba kama sisi, wengine pia wanataka kutoka maelezo. Fikiria jambo hili. Unapokuwa na mazungumzo pamoja na rafiki zako, je, unazungumza sana hivi kwamba wanakosa nafasi ya kuzungumza? La hasha! Unataka washiriki katika mazungumzo. Vivyo hivyo, kwenye mikutano, tungependa kuwapa wengi iwezekanavyo fursa ya kutoa maelezo. Kwa kweli, mojawapo ya njia bora zaidi ya kuwatia moyo ndugu na dada zetu, ni kuwapa nafasi ya kueleza imani yao. (1 Kor. 10:24) Toa maelezo mafupi, na hivyo utawapa watu wengi zaidi muda wa kushiriki. Hata unapotoa maelezo mafupi, epuka kuzungumzia mambo mengi sana. Ukizungumzia kila jambo linalotajwa kwenye fungu, wengine watakosa jambo la kusema. w23.04 22-23 ¶11-13