Alhamisi, Oktoba 2
Lakini wewe umehifadhi divai nzuri mpaka sasa.—Yoh. 2:10.
Tunaweza kujifunza nini kutokana na muujiza wa Yesu wa kugeuza maji kuwa divai? Tunajifunza somo kuhusu unyenyekevu. Yesu hakujigamba kuhusu muujiza huo; kwa kweli, hakujigamba kamwe kuhusu mambo aliyotimiza. Kinyume chake, kwa unyenyekevu, tena na tena alimpa sifa na utukufu Baba yake. (Yoh. 5:19, 30; 8:28) Ikiwa tutamwiga Yesu kwa kuwa wanyenyekevu, hatutajigamba kuhusu mambo tunayotimiza. Acheni tujigambe si kujihusu sisi wenyewe, bali kumhusu Mungu mwenye kustaajabisha ambaye tuna pendeleo la kumtumikia. (Yer. 9:23, 24) Acheni tumpe sifa anazostahili. Isitoshe, hatuwezi kamwe kutimiza jambo lolote zuri bila msaada wa Yehova? (1 Kor. 1:26-31) Tunapokuwa wanyenyekevu, hatujitafutii sifa kwa mambo mazuri tunayowafanyia wengine. Tunaridhika kujua kwamba Yehova anaona na kuthamini mambo tunayofanya. (Linganisha Mathayo 6:2-4; Ebr. 13:16) Kwa kweli, tunamfurahisha Yehova tunapomwiga Yesu kwa kuonyesha unyenyekevu.—1 Pet. 5:6. w23.04 4 ¶9; 5 ¶11-12
Ijumaa, Oktoba 3
Mkiangalia, si faida zenu wenyewe, bali pia faida za wengine.—Flp. 2:4.
Akiongozwa na roho, mtume Paulo aliwatia moyo Wakristo waangalie faida za wengine. Tunaweza kutumiaje shauri hilo kwenye mikutano? Kwa kukumbuka kwamba kama sisi, wengine pia wanataka kutoka maelezo. Fikiria jambo hili. Unapokuwa na mazungumzo pamoja na rafiki zako, je, unazungumza sana hivi kwamba wanakosa nafasi ya kuzungumza? La hasha! Unataka washiriki katika mazungumzo. Vivyo hivyo, kwenye mikutano, tungependa kuwapa wengi iwezekanavyo fursa ya kutoa maelezo. Kwa kweli, mojawapo ya njia bora zaidi ya kuwatia moyo ndugu na dada zetu, ni kuwapa nafasi ya kueleza imani yao. (1 Kor. 10:24) Toa maelezo mafupi, na hivyo utawapa watu wengi zaidi muda wa kushiriki. Hata unapotoa maelezo mafupi, epuka kuzungumzia mambo mengi sana. Ukizungumzia kila jambo linalotajwa kwenye fungu, wengine watakosa jambo la kusema. w23.04 22-23 ¶11-13
Jumamosi, Oktoba 4
Ninafanya mambo yote kwa ajili ya habari njema, ili niishiriki pamoja na wengine.—1 Kor. 9:23.
Tunapaswa kukumbuka kwamba ni jambo muhimu kuendelea kuwasaidia wengine, hasa kupitia huduma yetu ya Kikristo. Katika huduma yetu, tunahitaji kunyumbulika. Tunakutana na watu wenye imani na mitazamo mbalimbali na wanaotoka katika malezi mbalimbali. Mtume Paulo alibadilikana kulingana na hali na tunaweza kuiga mfano wake. Yesu alimweka rasmi Paulo kuwa “mtume kwa mataifa.” (Rom. 11:13) Akiwa na jukumu hilo, Paulo aliwahubiria Wayahudi, Wagiriki, watu wenye elimu, wakulima, watu walioheshimiwa, na wafalme. Ili kugusa mioyo ya watu hao mbalimbali, Paulo alikuwa “mambo yote kwa watu wa namna zote.” (1 Kor. 9:19-22) Alizingatia utamaduni, malezi, na imani ya wasikilizaji wake, na kubadilisha njia yake ya kuhubiri ili iwafae. Sisi pia tunaweza kupata matokeo mazuri katika huduma ikiwa tutakuwa tayari kubadili mazungumzo yetu ili yalingane na mahitaji ya wasikilizaji wetu. w23.07 23 ¶11-12