Jumanne, Oktoba 21
Yule atakayevumilia mpaka mwisho ndiye atakayeokolewa.—Mt. 24:13.
Fikiria manufaa ya kuonyesha subira. Tunapoonyesha subira, tunakuwa wenye furaha na watulivu zaidi. Hivyo, subira inaweza kutusaidia tuwe na hali nzuri kiakili na kimwili. Tunapowaonyesha wengine subira, tunakuwa na uhusiano mzuri zaidi pamoja nao. Kutaniko letu linakuwa na umoja zaidi. Ikiwa mtu fulani atatuudhi, hatutakasirika upesi na hivyo tutazuia hali isiwe mbaya zaidi. (Zab. 37:8, maelezo ya chini; Met. 14:29) Lakini jambo muhimu zaidi, tunamwiga Baba yetu wa mbinguni na kumkaribia hata zaidi. Subira ni sifa yenye kupendeza na ambayo inatunufaisha sana! Ingawa huenda isiwe rahisi sikuzote kuonyesha subira, kwa msaada wa Yehova tunaweza kuendelea kusitawisha sifa hiyo. Na tunapoendelea kuungoja ulimwengu mpya kwa subira, tunaweza kuwa na uhakika kwamba “jicho la Yehova linawalinda wale wanaomwogopa, wale wanaongojea upendo wake mshikamanifu.” (Zab. 33:18) Acheni sisi sote tuazimie kuendelea kujivika subira. w23.08 22 ¶7; 25 ¶16-17
Jumatano, Oktoba 22
Imani bila matendo imekufa.—Yak. 2:17.
Yakobo alionyesha kwamba huenda mtu akadai kwamba ana imani, lakini matendo yake hayathibitishi hilo. (Yak. 2:1-5, 9) Yakobo pia anamtaja mtu aliyemwona ‘ndugu au dada asiye na nguo au chakula’ lakini hakumsaidia. Hata ikiwa mtu huyo alidai kwamba ana imani, hakuionyesha kwa matendo; hivyo, imani yake ni bure. (Yak. 2:14-16) Yakobo alimrejelea Rahabu kuwa mfano mzuri wa mtu aliyeonyesha imani kwa matendo. (Yak. 2:25, 26.) Rahabu alikuwa amesikia kumhusu Yehova na alitambua kwamba alikuwa akiwategemeza Waisraeli. (Yos. 2:9-11) Rahabu alionyesha imani yake kwa matendo—aliwalinda wapelelezi wawili Waisraeli, maisha yao yalipokuwa hatarini. Kwa sababu hiyo, mwanamke huyo asiye Mwisraeli ambaye hakuwa mkamilifu, alitangazwa kuwa mwadilifu kama Abrahamu. Mfano alioweka unakazia umuhimu wa kuonyesha imani kwa matendo. w23.12 5-6 ¶12-13
Alhamisi, Oktoba 23
Iweni na mizizi na kuimarishwa juu ya ule msingi.—Efe. 3:17.
Tukiwa Wakristo, haturidhiki kujua mambo ya msingi tu kuhusu Biblia. Kwa msaada wa roho takatifu ya Mungu, tunatamani kujifunza “hata mambo mazito ya Mungu.” (1 Kor. 2:9, 10) Kwa nini usianze mradi wa kujifunza kibinafsi ambao utakusaidia kumkaribia Yehova hata zaidi? Kwa mfano, unaweza kuchunguza jinsi alivyowaonyesha upendo watumishi wake wa zamani na jinsi hilo linavyothibitisha kwamba anakupenda wewe pia. Unaweza kuchunguza mpango wa ibada ambao Yehova aliweka katika Israeli la kale na jinsi tunavyomwabudu leo tukiwa Wakristo. Au labda unaweza kujifunza kwa undani unabii mbalimbali ambao Yesu alitimiza wakati wa maisha na huduma yake hapa duniani. Unaweza kupata shangwe nyingi kwa kujifunza habari hizo kwa msaada wa Fahirisi au Mwongozo wa Utafiti wa Mashahidi wa Yehova. Kujifunza Biblia kwa kina kunaweza kuimarisha imani yako na kukusaidia upate “ujuzi kumhusu Mungu.”—Met. 2:4, 5. w23.10 18-19 ¶3-5