Jumatano, Oktoba 22
Imani bila matendo imekufa.—Yak. 2:17.
Yakobo alionyesha kwamba huenda mtu akadai kwamba ana imani, lakini matendo yake hayathibitishi hilo. (Yak. 2:1-5, 9) Yakobo pia anamtaja mtu aliyemwona ‘ndugu au dada asiye na nguo au chakula’ lakini hakumsaidia. Hata ikiwa mtu huyo alidai kwamba ana imani, hakuionyesha kwa matendo; hivyo, imani yake ni bure. (Yak. 2:14-16) Yakobo alimrejelea Rahabu kuwa mfano mzuri wa mtu aliyeonyesha imani kwa matendo. (Yak. 2:25, 26.) Rahabu alikuwa amesikia kumhusu Yehova na alitambua kwamba alikuwa akiwategemeza Waisraeli. (Yos. 2:9-11) Rahabu alionyesha imani yake kwa matendo—aliwalinda wapelelezi wawili Waisraeli, maisha yao yalipokuwa hatarini. Kwa sababu hiyo, mwanamke huyo asiye Mwisraeli ambaye hakuwa mkamilifu, alitangazwa kuwa mwadilifu kama Abrahamu. Mfano alioweka unakazia umuhimu wa kuonyesha imani kwa matendo. w23.12 5-6 ¶12-13
Alhamisi, Oktoba 23
Iweni na mizizi na kuimarishwa juu ya ule msingi.—Efe. 3:17.
Tukiwa Wakristo, haturidhiki kujua mambo ya msingi tu kuhusu Biblia. Kwa msaada wa roho takatifu ya Mungu, tunatamani kujifunza “hata mambo mazito ya Mungu.” (1 Kor. 2:9, 10) Kwa nini usianze mradi wa kujifunza kibinafsi ambao utakusaidia kumkaribia Yehova hata zaidi? Kwa mfano, unaweza kuchunguza jinsi alivyowaonyesha upendo watumishi wake wa zamani na jinsi hilo linavyothibitisha kwamba anakupenda wewe pia. Unaweza kuchunguza mpango wa ibada ambao Yehova aliweka katika Israeli la kale na jinsi tunavyomwabudu leo tukiwa Wakristo. Au labda unaweza kujifunza kwa undani unabii mbalimbali ambao Yesu alitimiza wakati wa maisha na huduma yake hapa duniani. Unaweza kupata shangwe nyingi kwa kujifunza habari hizo kwa msaada wa Fahirisi au Mwongozo wa Utafiti wa Mashahidi wa Yehova. Kujifunza Biblia kwa kina kunaweza kuimarisha imani yako na kukusaidia upate “ujuzi kumhusu Mungu.”—Met. 2:4, 5. w23.10 18-19 ¶3-5
Ijumaa, Oktoba 24
Zaidi ya mambo yote, pendaneni sana, kwa sababu upendo hufunika dhambi nyingi.—1 Pet. 4:8.
Neno linalotafsiriwa kuwa “sana” ambalo mtume Petro ametumia, kihalisi linamaanisha “kujinyoosha” au “kuvutika.” Sehemu ya pili ya mstari huo inafafanua matokeo ya kupendana sana. Tukiwapenda sana ndugu zetu tutafunika dhambi zao. Tunaweza kuwazia hali hiyo kwa njia hii: Tunaushika upendo wetu kwa mikono miwili, kana kwamba tumeshika kitambaa kinachovutika, na tunakivuta zaidi na zaidi hadi kinafunika, si dhambi moja au mbili, bali “dhambi nyingi.” Kufunika kunamaanisha kusamehe. Kama kitambaa kinavyoweza kufunika doa, upendo unaweza kufunika udhaifu na kutokamilika kwa wengine. Upendo wetu kwa wengine unapaswa kuwa na nguvu sana hivi kwamba tunaweza kusamehe kutokamilika kwa waabudu wenzetu—hata ikiwa ni vigumu kufanya hivyo. (Kol. 3:13) Tunapowasamehe wengine, tunaonyesha kwamba upendo wetu ni wenye nguvu na tunataka kumfurahisha Yehova. w23.11 11-12 ¶13-15