Jumamosi, Oktoba 25
Shafani akaanza kukisoma mbele ya mfalme.—2 Nya. 34:18.
Alipokuwa na umri wa miaka 26, Mfalme Yosia alianza kazi ya kurekebisha hekalu. Kazi hiyo ilipokuwa ikiendelea, “kitabu cha Sheria ya Yehova kilichotolewa kupitia Musa” kilipatikana. Mfalme aliposikia kikisomwa, alichochewa kuchukua hatua na kutenda kulingana na mambo yaliyoandikwa humo. (2 Nya. 34:14, 19-21) Je, ungependa kusoma Biblia kwa ukawaida? Ikiwa tayari unafanya hivyo je, unafurahia? Je, unaweka kumbukumbu ya mistari ambayo inaweza kukusaidia kibinafsi? Yosia alipokuwa na umri wa miaka 39, alifanya uamuzi mbaya uliomsababishia kifo. Alijitegemea mwenyewe badala ya kumwomba Yehova mwongozo. (2 Nya. 35:20-25) Tunapata somo fulani hapa. Hata iwe tuna umri gani au tumekuwa tukijifunza Biblia kwa muda mrefu kadiri gani, tunapaswa kuendelea kumtafuta Yehova. Hilo linatia ndani kusali kwake kwa ukawaida ili kupata mwongozo, kujifunza Neno lake, na kusikiliza ushauri wa Wakristo wakomavu. Tukifanya hivyo, tutapunguza uwezekano wa kufanya makosa mazito na tutakuwa wenye furaha zaidi.—Yak. 1:25. w23.09 12 ¶15-16
Jumapili, Oktoba 26
Mungu huwapinga wenye majivuno, lakini huwapa wanyenyekevu fadhili zisizostahiliwa.—Yak. 4:6.
Biblia inawataja wanawake wengi wa pekee waliompenda Yehova na kumtumikia. Wanawake hao walikuwa “wenye kiasi katika mazoea” na “waaminifu katika mambo yote.” (1 Tim. 3:11) Kwa kuongezea, akina dada vijana wanaweza kupata katika kutaniko lao wanawake Wakristo wakomavu ambao ni mfano mzuri wa kuigwa. Akina dada vijana, je, mnaweza kutafuta kutanikoni wanawake Wakristo wakomavu ambao mnaweza kuiga mfano wao? Chunguzeni sifa zao zinazovutia; kisha mfikirie jinsi mnavyoweza kuonyesha sifa hizo. Sifa muhimu ya kuwa Mkristo mkomavu ni unyenyekevu. Ikiwa mwanamke ni mnyenyekevu, atafurahia uhusiano mzuri na Yehova na watu wengine pia. Kwa mfano, mwanamke anayempenda Yehova, kwa unyenyekevu anachagua kuunga mkono kanuni ya ukichwa ambayo Baba yake wa mbinguni alianzisha. (1 Kor. 11:3) Kanuni hiyo inatumika kwa njia hususa katika kutaniko na katika familia pia. w23.12 18-19 ¶3-5
Jumatatu, Oktoba 27
Waume wanapaswa kuwapenda wake zao kama miili yao wenyewe.—Efe. 5:28.
Yehova anatarajia mume ampende mke wake na kumtunza kimwili, kihisia, na kiroho. Kusitawisha uwezo wa kufikiri, kuwaheshimu wanawake, na kuwa mwenye kutegemeka, kutakusaidia ukiwa mwenzi wa ndoa. Baada ya kufunga ndoa, unaweza kuwa baba. Unaweza kujifunza nini kutoka kwa Yehova kuhusu kuwa baba mzuri? (Efe. 6:4) Yehova alimwambia waziwazi Mwana wake, Yesu, kwamba anampenda na kumkubali. (Mt. 3:17) Ikiwa utakuwa baba, hakikisha kuwa unawahakikishia kwa ukawaida watoto wako kwamba unawapenda. Wapongeze mara kwa mara kwa mambo mazuri wanayofanya. Akina baba wanaoiga mfano wa Yehova wanawasaidia watoto wao kuwa wanaume na wanawake Wakristo wakomavu. Unaweza kujitayarisha sasa kwa ajili ya jukumu hilo kwa kuwajali kwa upendo watu katika familia yenu na katika kutaniko na kwa kujifunza kuwaambia kwamba unawapenda na unawathamini.—Yoh. 15:9. w23.12 28-29 ¶17-18