Ijumaa, Oktoba 3
Mkiangalia, si faida zenu wenyewe, bali pia faida za wengine.—Flp. 2:4.
Akiongozwa na roho, mtume Paulo aliwatia moyo Wakristo waangalie faida za wengine. Tunaweza kutumiaje shauri hilo kwenye mikutano? Kwa kukumbuka kwamba kama sisi, wengine pia wanataka kutoka maelezo. Fikiria jambo hili. Unapokuwa na mazungumzo pamoja na rafiki zako, je, unazungumza sana hivi kwamba wanakosa nafasi ya kuzungumza? La hasha! Unataka washiriki katika mazungumzo. Vivyo hivyo, kwenye mikutano, tungependa kuwapa wengi iwezekanavyo fursa ya kutoa maelezo. Kwa kweli, mojawapo ya njia bora zaidi ya kuwatia moyo ndugu na dada zetu, ni kuwapa nafasi ya kueleza imani yao. (1 Kor. 10:24) Toa maelezo mafupi, na hivyo utawapa watu wengi zaidi muda wa kushiriki. Hata unapotoa maelezo mafupi, epuka kuzungumzia mambo mengi sana. Ukizungumzia kila jambo linalotajwa kwenye fungu, wengine watakosa jambo la kusema. w23.04 22-23 ¶11-13
Jumamosi, Oktoba 4
Ninafanya mambo yote kwa ajili ya habari njema, ili niishiriki pamoja na wengine.—1 Kor. 9:23.
Tunapaswa kukumbuka kwamba ni jambo muhimu kuendelea kuwasaidia wengine, hasa kupitia huduma yetu ya Kikristo. Katika huduma yetu, tunahitaji kunyumbulika. Tunakutana na watu wenye imani na mitazamo mbalimbali na wanaotoka katika malezi mbalimbali. Mtume Paulo alibadilikana kulingana na hali na tunaweza kuiga mfano wake. Yesu alimweka rasmi Paulo kuwa “mtume kwa mataifa.” (Rom. 11:13) Akiwa na jukumu hilo, Paulo aliwahubiria Wayahudi, Wagiriki, watu wenye elimu, wakulima, watu walioheshimiwa, na wafalme. Ili kugusa mioyo ya watu hao mbalimbali, Paulo alikuwa “mambo yote kwa watu wa namna zote.” (1 Kor. 9:19-22) Alizingatia utamaduni, malezi, na imani ya wasikilizaji wake, na kubadilisha njia yake ya kuhubiri ili iwafae. Sisi pia tunaweza kupata matokeo mazuri katika huduma ikiwa tutakuwa tayari kubadili mazungumzo yetu ili yalingane na mahitaji ya wasikilizaji wetu. w23.07 23 ¶11-12
Jumapili, Oktoba 5
Mtumwa wa Bwana hahitaji kupigana, bali anahitaji kuwa mpole kwa wote.—2 Tim. 2:24.
Sifa ya upole si udhaifu, bali inaonyesha kwamba mtu ana nguvu. Tunahitaji kuwa na nguvu za kujidhibiti ili kuendelea kuwa watulivu tunapokabili hali ngumu. Upole ni moja kati ya sifa za “tunda la roho.” (Gal. 5:22, 23) Neno fulani la Kigiriki ambalo lilitafsiriwa kuwa “upole,” wakati mwingine lilitumiwa kufafanua farasi wa mwituni ambaye alizoezwa na kuwa mnyama wa kufugwa. Wazia farasi wa mwituni ambaye anakuwa mpole. Mnyama huyo ni mpole lakini ana nguvu. Tukiwa wanadamu, tunawezaje kusitawisha sifa ya upole na wakati huohuo kuwa wenye nguvu? Hatuwezi kufanya hivyo kwa nguvu zetu. Tunahitaji kumwomba Mungu atupe roho yake na kumwomba atusaidie kusitawisha sifa hii maridadi. Mambo yaliyoonwa yanathibitisha kwamba hilo linawezekana. Mashahidi wengi wamejibu kwa upole wanapokabiliana na wapinzani na hilo limewafanya wengi wawe na maoni yanayofaa kutuhusu.—2 Tim. 2:24, 25. w23.09 15 ¶3