Jumapili, Oktoba 5
Mtumwa wa Bwana hahitaji kupigana, bali anahitaji kuwa mpole kwa wote.—2 Tim. 2:24.
Sifa ya upole si udhaifu, bali inaonyesha kwamba mtu ana nguvu. Tunahitaji kuwa na nguvu za kujidhibiti ili kuendelea kuwa watulivu tunapokabili hali ngumu. Upole ni moja kati ya sifa za “tunda la roho.” (Gal. 5:22, 23) Neno fulani la Kigiriki ambalo lilitafsiriwa kuwa “upole,” wakati mwingine lilitumiwa kufafanua farasi wa mwituni ambaye alizoezwa na kuwa mnyama wa kufugwa. Wazia farasi wa mwituni ambaye anakuwa mpole. Mnyama huyo ni mpole lakini ana nguvu. Tukiwa wanadamu, tunawezaje kusitawisha sifa ya upole na wakati huohuo kuwa wenye nguvu? Hatuwezi kufanya hivyo kwa nguvu zetu. Tunahitaji kumwomba Mungu atupe roho yake na kumwomba atusaidie kusitawisha sifa hii maridadi. Mambo yaliyoonwa yanathibitisha kwamba hilo linawezekana. Mashahidi wengi wamejibu kwa upole wanapokabiliana na wapinzani na hilo limewafanya wengi wawe na maoni yanayofaa kutuhusu.—2 Tim. 2:24, 25. w23.09 15 ¶3
Jumatatu, Oktoba 6
Nilisali nipate mvulana huyu, naye Yehova akanipa nilichoomba.—1 Sam. 1:27.
Katika maono yenye kustaajabisha, mtume Yohana aliwaona wazee 24 mbinguni wakimwabudu Yehova. Walimsifu Mungu na kusema kwamba anastahili kupokea “utukufu na heshima na nguvu.” (Ufu. 4:10, 11) Pia, malaika waaminifu wana sababu nyingi za kumsifu na kumtukuza Yehova. Wanaishi pamoja naye mbinguni na wanamjua vizuri. Wanaona sifa zake kupitia mambo anayofanya. Wanapomwona Yehova akitenda, wanachochewa kumsifu. (Ayu. 38:4-7) Sisi pia tungependa kumsifu Yehova katika sala zetu, tukitaja mambo tunayopenda na kuthamini kumhusu. Unaposoma na kujifunza Biblia, jaribu kutambua sifa za Yehova ambazo hasa unavutiwa nazo. (Ayu. 37:23; Rom. 11:33) Kisha umwambie Yehova jinsi unavyohisi kuhusu sifa hizo. Pia, tunaweza kumsifu Yehova kwa sababu ya jinsi ambavyo ametusaidia na kuwasaidia ndugu na dada zetu wote Wakristo.—1 Sam. 2:1, 2. w23.05 3-4 ¶6-7
Jumanne, Oktoba 7
Mtembee kwa kumstahili Yehova.—Kol. 1:10.
Mwaka wa 1919, watu wa Mungu waliwekwa huru kutoka katika Babiloni Mkubwa. Mwaka huo, “mtumwa mwaminifu na mwenye busara” alianza kufanya kazi ili watu wenye mioyo minyoofu waanze kutembea katika ‘Njia hiyo mpya ya Utakatifu’ iliyofunguliwa. (Mt. 24:45-47; Isa. 35:8) Kazi iliyofanywa na “watengeneza-barabara” waliotangulia, iliwasaidia wale walioanza kutembea katika barabara hiyo kuu wajifunze mengi zaidi kumhusu Yehova na makusudi yake. (Met. 4:18) Pia, wangeweza kupatanisha maisha yao na viwango vya Yehova. Yehova hakutarajia watu wake wafanye marekebisho yote yaliyohitajika kwa wakati mmoja. Badala yake, amekuwa akiwasafisha watu wake hatua kwa hatua. Tutafurahi sana wakati ambapo tutaweza kumfurahisha Mungu wetu katika kila jambo tunalofanya! Kila barabara inahitaji kudumishwa kwa ukawaida. Tangu mwaka wa 1919, kazi ya kutengeneza “Njia ya Utakatifu” imekuwa ikiendelea, ili kufanya iwezekane kwa watu wengi zaidi kuondoka katika Babiloni Mkubwa. w23.05 17 ¶15; 19 ¶16