Jumatatu, Oktoba 6
Nilisali nipate mvulana huyu, naye Yehova akanipa nilichoomba.—1 Sam. 1:27.
Katika maono yenye kustaajabisha, mtume Yohana aliwaona wazee 24 mbinguni wakimwabudu Yehova. Walimsifu Mungu na kusema kwamba anastahili kupokea “utukufu na heshima na nguvu.” (Ufu. 4:10, 11) Pia, malaika waaminifu wana sababu nyingi za kumsifu na kumtukuza Yehova. Wanaishi pamoja naye mbinguni na wanamjua vizuri. Wanaona sifa zake kupitia mambo anayofanya. Wanapomwona Yehova akitenda, wanachochewa kumsifu. (Ayu. 38:4-7) Sisi pia tungependa kumsifu Yehova katika sala zetu, tukitaja mambo tunayopenda na kuthamini kumhusu. Unaposoma na kujifunza Biblia, jaribu kutambua sifa za Yehova ambazo hasa unavutiwa nazo. (Ayu. 37:23; Rom. 11:33) Kisha umwambie Yehova jinsi unavyohisi kuhusu sifa hizo. Pia, tunaweza kumsifu Yehova kwa sababu ya jinsi ambavyo ametusaidia na kuwasaidia ndugu na dada zetu wote Wakristo.—1 Sam. 2:1, 2. w23.05 3-4 ¶6-7
Jumanne, Oktoba 7
Mtembee kwa kumstahili Yehova.—Kol. 1:10.
Mwaka wa 1919, watu wa Mungu waliwekwa huru kutoka katika Babiloni Mkubwa. Mwaka huo, “mtumwa mwaminifu na mwenye busara” alianza kufanya kazi ili watu wenye mioyo minyoofu waanze kutembea katika ‘Njia hiyo mpya ya Utakatifu’ iliyofunguliwa. (Mt. 24:45-47; Isa. 35:8) Kazi iliyofanywa na “watengeneza-barabara” waliotangulia, iliwasaidia wale walioanza kutembea katika barabara hiyo kuu wajifunze mengi zaidi kumhusu Yehova na makusudi yake. (Met. 4:18) Pia, wangeweza kupatanisha maisha yao na viwango vya Yehova. Yehova hakutarajia watu wake wafanye marekebisho yote yaliyohitajika kwa wakati mmoja. Badala yake, amekuwa akiwasafisha watu wake hatua kwa hatua. Tutafurahi sana wakati ambapo tutaweza kumfurahisha Mungu wetu katika kila jambo tunalofanya! Kila barabara inahitaji kudumishwa kwa ukawaida. Tangu mwaka wa 1919, kazi ya kutengeneza “Njia ya Utakatifu” imekuwa ikiendelea, ili kufanya iwezekane kwa watu wengi zaidi kuondoka katika Babiloni Mkubwa. w23.05 17 ¶15; 19 ¶16
Jumatano, Oktoba 8
Sitakuacha kamwe.—Ebr. 13:5.
Washiriki wa Baraza Linaloongoza wamekuwa wakiwazoeza kibinafsi wasaidizi katika halmashauri mbalimbali za Baraza Linaloongoza. Kwa sasa wasaidizi hao wanashughulikia majukumu mazito kwa uaminifu. Wako tayari kabisa kuendeleza kazi ya kuwatunza kondoo wa Kristo. Watiwa-mafuta wa mwisho watakapochukuliwa na kwenda mbinguni mwishoni mwa ile dhiki kuu, ibada safi itaendelea hapa duniani. Kwa sababu ya uongozi mzuri wa Yesu Kristo, waabudu wa Mungu hawatakosa chochote. Ni kweli kwamba wakati huo tutakuwa tukishambuliwa na Gogu wa Magogu, muungano wa mataifa yenye chuki. (Eze. 38:18-20) Lakini shambulizi hilo fupi halitafaulu; halitawafanya watu wa Mungu waache kumwabudu Yehova. Bila shaka atawaokoa! Katika maono, mtume Yohana aliona “umati mkubwa” wa kondoo wengine wa Kristo. Yohana aliambiwa kwamba ‘umati huo mkubwa’ unatoka “katika ile dhiki kuu.” (Ufu. 7:9, 14) Naam, tuna uhakika kwamba watakuwa salama! w24.02 5-6 ¶13-14