Jumapili, Agosti 10
Rafiki wa kweli hupenda nyakati zote naye ni ndugu ambaye amezaliwa kwa ajili ya nyakati za taabu.—Met. 17:17.
Wakristo huko Yudea walipokabili njaa kali, akina ndugu katika kutaniko la Antiokia “wakaamua kila mmoja kulingana na uwezo wake, watume msaada kwa akina ndugu walioishi Yudea.” (Mdo. 11:27-30) Ingawa akina ndugu waliokabili njaa waliishi eneo la mbali, Wakristo huko Antiokia waliazimia kuwasaidia. (1 Yoh. 3:17, 18) Leo, sisi pia tunaweza kuonyesha huruma tunapopata habari kwamba waabudu wenzetu wamepatwa na msiba. Tunaitikia upesi—labda kwa kuwauliza wazee ikiwa tunaweza kusaidia katika kazi ya kutoa msaada, kwa kutoa mchango kwa ajili ya kazi ya ulimwenguni pote, au kwa kusali kwa ajili ya wale walioathiriwa na msiba. Huenda ndugu na dada zetu wakahitaji pia msaada ili kupata mahitaji yao ya msingi. Mfalme wetu, Kristo Yesu, atakapokuja kutekeleza hukumu, tungependa atupate tukionyesha huruma, kisha atupatie mwaliko wa ‘kuurithi Ufalme.’—Mt. 25:34-40. w23.07 4 ¶9-10; 6 ¶12
Jumatatu, Agosti 11
Usawaziko wenu na ujulikane kwa watu wote.—Flp. 4:5.
Yesu aliiga usawaziko wa Yehova. Alitumwa duniani ili awahubirie “kondoo waliopotea wa nyumba ya Israeli.” Lakini alikuwa mwenye usawaziko alipokuwa akitimiza mgawo huo. Pindi moja, mwanamke asiye Mwisraeli alimsihi Yesu amponye binti yake ambaye alikuwa “anasumbuliwa kikatili na roho mwovu.” Kwa huruma, Yesu alifanya jambo ambalo mwanamke huyo alimwomba na akamponya binti yake. (Mt. 15:21-28) Fikiria mfano mwingine. Mwanzoni mwa huduma yake, Yesu alisema hivi: “Yeyote anayenikana . . . , mimi pia nitamkana.” (Mt. 10:33) Lakini je, alimkana Petro alipomkana mara tatu? Hapana. Yesu alijua kwamba Petro alitubu na alikuwa mwenye imani. Baada ya kufufuliwa, Yesu alimtokea Petro na inaelekea alimhakikishia kwamba amemsamehe na anampenda. (Luka 24:33, 34) Yehova Mungu na Yesu Kristo ni wenye usawaziko. Namna gani sisi? Yehova anatarajia tuwe wenye usawaziko. w23.07 21 ¶6-7
Jumanne, Agosti 12
Kifo hakitakuwapo tena.—Ufu. 21:4.
Ni uhakikisho gani tunaoweza kushiriki na wale ambao wana shaka kwamba ahadi ya Mungu ya Paradiso itatimia? Kwanza, Yehova mwenyewe ndiye anayetoa ahadi hiyo. Kitabu cha Ufunuo kinasema: “Yule aliyeketi kwenye kiti cha ufalme akasema: ‘Tazama! Ninafanya vitu vyote kuwa vipya.’” Yeye ana hekima, nguvu, na tamaa ya kutimiza ahadi yake. Pili, utimizo wa ahadi hiyo ni hakika kabisa, hivi kwamba kwa maoni ya Yehova tayari mambo hayo yametukia. Ndiyo sababu anasema: “Maneno haya ni ya uaminifu na ya kweli. . . . Yametimia!” Tatu, Yehova anapoanza kufanya jambo, anahakikisha linakamilika kwa mafanikio, kama inavyothibitishwa na maneno haya: “Mimi ndiye Alfa na Omega.” (Ufu. 21:6) Yehova atathibitisha kwamba Shetani ni mwongo na ameshindwa. Hivyo, mtu anaposema, “Ahadi hii haiwezi kutimia,” unaweza kusoma na kufafanua Ufunuo 21:5, 6. Mwonyeshe jinsi ambavyo Yehova ametoa uhakikisho wa ahadi yake, kwa kuitia saini yake mwenyewe kwa njia ya mfano.—Isa. 65:16. w23.11 7 ¶18-19