Jumatatu, Agosti 18
Kwa sababu ya ahadi ya Mungu, . . . alikuwa mwenye nguvu kwa imani yake.—Rom. 4:20.
Njia moja ambayo Yehova anatupatia nguvu ni kupitia wazee wa kutaniko. (Isa. 32:1, 2) Basi unapohisi wasiwasi, waeleze wazee wa kutaniko mambo yanayokuhangaisha. Wanapokupatia msaada, usisite kuukubali. Kupitia kwao, Yehova anaweza kukupa nguvu. Tumaini letu linalotegemea Biblia la kupata uzima wa milele—iwe ni katika dunia Paradiso au katika Ufalme wa mbinguni—linaweza pia kutujaza nguvu. (Rom. 4:3, 18, 19) Tumaini letu linatutia nguvu ili tuendelee kuvumilia majaribu, tuhubiri habari njema, na tutimize migawo mbalimbali kutanikoni. (1 The. 1:3) Tumaini hilohilo lilimtia nguvu mtume Paulo. Alikuwa ‘amekandamizwa,’ ‘kufadhaishwa,’ ‘kuteswa,’ na ‘kuangushwa chini.’ Hata uhai wake ulikuwa hatarini. (2 Kor. 4:8-10) Paulo alipata nguvu za kuvumilia kwa kukazia fikira tumaini lake. (2 Kor. 4:16-18) Paulo alikazia fikira tumaini lake la wakati wake ujao la kuishi milele mbinguni. Paulo alitafakari kuhusu tumaini hilo. Na matokeo ni kwamba alihisi “anafanywa upya siku kwa siku.” w23.10 15-16 ¶14-17
Jumanne, Agosti 19
Yehova atawapa nguvu watu wake. Yehova atawabariki watu wake kwa amani.—Zab. 29:11.
Unaposali, fikiria ikiwa huu ndio wakati wa Yehova wa kujibu ombi lako. Huenda tukahisi kwamba tunahitaji kupata jibu la sala zetu papo hapo. Lakini ukweli ni kwamba Yehova anajua wakati unaofaa wa kutusaidia. (Ebr. 4:16) Sala yetu isipojibiwa papo hapo, huenda tukahisi kwamba jibu la Yehova ni ‘Hapana.’ Lakini jibu la Yehova linaweza kuwa ‘Bado wakati haujafika.’ Kwa mfano, ndugu kijana aliomba aponywe ugonjwa wake mbaya. Lakini akaendelea kuugua. Ikiwa Yehova angemponya kimuujiza, Shetani angeweza kudai kwamba ndugu huyo anaendelea kumtumikia Yehova kwa sababu tu ameponywa. (Ayu. 1:9-11; 2:4) Isitoshe, tayari Yehova amepanga wakati wa kuponya magonjwa yote. (Isa. 33:24; Ufu. 21:3, 4) Na mpaka wakati huo ufike, hatuwezi kutarajia kuponywa kimuujiza. Hivyo, ndugu huyo anaweza kumwomba Yehova ampatie nguvu na amani ya akili ili avumilie ugonjwa wake na kuendelea kumtumikia Mungu kwa uaminifu. w23.11 24 ¶13
Jumatano, Agosti 20
Hajatutendea kulingana na dhambi zetu, wala hajatupa adhabu tuliyostahili kulingana na makosa yetu.—Zab. 103:10.
Samsoni alikuwa amefanya kosa zito lakini hakufa moyo. Alitafuta fursa ya kutimiza mgawo aliopewa na Mungu wa kupigana dhidi ya Wafilisti. (Amu. 16:28-30) Samsoni alimsihi hivi Yehova: “Acha niwalipize kisasi Wafilisti.” Mungu wa kweli alijibu ombi la Samsoni na kumrudishia nguvu zake za kipekee. Matokeo ni kwamba Samsoni aliwaua Wafilisti wengi zaidi pindi hiyo kuliko alivyofanya hapo awali. Ingawa Samsoni alipatwa na matokeo mabaya kwa sababu ya kosa lake, aliendelea kujitahidi kufanya mapenzi ya Yehova. Hata ikiwa tutafanya kosa na kuhitaji kukaripiwa au kupoteza pendeleo fulani, hatupaswi kufa moyo. Kumbuka kwamba Yehova yuko tayari kutusamehe. (Zab. 103:8, 9) Licha ya makosa yetu, Yehova anaweza kutupatia nguvu za kufanya mapenzi yake kama alivyomsaidia Samsoni. w23.09 6 ¶15-16