Jumanne, Agosti 19
Yehova atawapa nguvu watu wake. Yehova atawabariki watu wake kwa amani.—Zab. 29:11.
Unaposali, fikiria ikiwa huu ndio wakati wa Yehova wa kujibu ombi lako. Huenda tukahisi kwamba tunahitaji kupata jibu la sala zetu papo hapo. Lakini ukweli ni kwamba Yehova anajua wakati unaofaa wa kutusaidia. (Ebr. 4:16) Sala yetu isipojibiwa papo hapo, huenda tukahisi kwamba jibu la Yehova ni ‘Hapana.’ Lakini jibu la Yehova linaweza kuwa ‘Bado wakati haujafika.’ Kwa mfano, ndugu kijana aliomba aponywe ugonjwa wake mbaya. Lakini akaendelea kuugua. Ikiwa Yehova angemponya kimuujiza, Shetani angeweza kudai kwamba ndugu huyo anaendelea kumtumikia Yehova kwa sababu tu ameponywa. (Ayu. 1:9-11; 2:4) Isitoshe, tayari Yehova amepanga wakati wa kuponya magonjwa yote. (Isa. 33:24; Ufu. 21:3, 4) Na mpaka wakati huo ufike, hatuwezi kutarajia kuponywa kimuujiza. Hivyo, ndugu huyo anaweza kumwomba Yehova ampatie nguvu na amani ya akili ili avumilie ugonjwa wake na kuendelea kumtumikia Mungu kwa uaminifu. w23.11 24 ¶13
Jumatano, Agosti 20
Hajatutendea kulingana na dhambi zetu, wala hajatupa adhabu tuliyostahili kulingana na makosa yetu.—Zab. 103:10.
Samsoni alikuwa amefanya kosa zito lakini hakufa moyo. Alitafuta fursa ya kutimiza mgawo aliopewa na Mungu wa kupigana dhidi ya Wafilisti. (Amu. 16:28-30) Samsoni alimsihi hivi Yehova: “Acha niwalipize kisasi Wafilisti.” Mungu wa kweli alijibu ombi la Samsoni na kumrudishia nguvu zake za kipekee. Matokeo ni kwamba Samsoni aliwaua Wafilisti wengi zaidi pindi hiyo kuliko alivyofanya hapo awali. Ingawa Samsoni alipatwa na matokeo mabaya kwa sababu ya kosa lake, aliendelea kujitahidi kufanya mapenzi ya Yehova. Hata ikiwa tutafanya kosa na kuhitaji kukaripiwa au kupoteza pendeleo fulani, hatupaswi kufa moyo. Kumbuka kwamba Yehova yuko tayari kutusamehe. (Zab. 103:8, 9) Licha ya makosa yetu, Yehova anaweza kutupatia nguvu za kufanya mapenzi yake kama alivyomsaidia Samsoni. w23.09 6 ¶15-16
Alhamisi, Agosti 21
Uvumilivu [hutokeza] hali yenye kukubaliwa; nayo hali yenye kukubaliwa, tumaini.—Rom. 5:4.
Uvumilivu wako hukupatia kibali cha Yehova. Hilo halimaanishi kwamba Yehova anafurahi unapokabili majaribu au matatizo. Wewe ndiye anayekukubali. Uvumilivu wako hutokeza hali yenye kukubaliwa. Baraka bora sana! (Zab. 5:12) Kumbuka kwamba Abrahamu alivumilia majaribu na kufurahia kibali cha Mungu. Yehova alimwona Abrahamu kuwa rafiki Yake na akahesabiwa kuwa mwadilifu. (Mwa. 15:6; Rom. 4:13, 22) Inaweza kuwa hivyo kwetu pia. Mungu hatoi kibali chake kwa msingi wa kiasi cha kazi tunachofanya katika utumishi wake au mapendeleo tunayofurahia. Anatupatia kibali chake kwa sababu ya kuvumilia kwa uaminifu. Sisi sote tunaweza kuvumilia, licha ya umri, hali, au uwezo wetu. Je, kwa sasa unavumilia kwa uaminifu jaribu fulani? Ikiwa ndivyo, kumbuka kwamba una kibali cha Mungu. Kutambua kwamba tuna kibali cha Mungu kunaweza kuwa na matokeo makubwa sana kwetu. Kunaweza kuimarisha tumaini letu. w23.12 11 ¶13-14