Jumapili, Agosti 24
Ndugu zangu wapendwa, iweni imara, thabiti.—1 Kor. 15:58.
Mwishoni mwa miaka ya 1970, jengo lenye ghorofa 60 lilijengwa hatua kwa hatua huko Tokyo, Japani. Watu walijiuliza jengo hilo lingewezaje kuhimili matetemeko ya ardhi yanayotokea mara kwa mara katika jiji hilo. Siri ilikuwa nini? Mainjinia walikuwa wamebuni jengo hilo liwe imara lakini lenye uwezo wa kunyumbulika ili lihimili mitikisiko ya tetemeko la ardhi. Wakristo ni kama ghorofa hilo refu. Jinsi gani? Mkristo anapaswa kudumisha usawaziko kati ya kuwa imara na kunyumbulika. Anapaswa kuwa imara na thabiti na kuazimia kuendelea kutii sheria na viwango vya Yehova. Anakuwa “tayari kutii” na halegezi msimamo wake. Kwa upande mwingine, anahitaji kuwa mwenye “usawaziko,” au mwenye kunyumbulika, ikiwa hali inaruhusu au hata anapohitajika kufanya hivyo. (Yak. 3:17) Mkristo ambaye amejifunza kuwa na maoni hayo yenye usawaziko ataepuka kushikilia sana maoni yake au kuendekeza mambo yasiyofaa. w23.07 14 ¶1-2
Jumatatu, Agosti 25
Mnampenda ingawa hamkumwona kamwe.—1 Pet. 1:8
Yesu alihitaji kusimama imara dhidi ya vishawishi vya Shetani Ibilisi, kutia ndani mashambulizi ya moja kwa moja ambayo yangeweza kufanya aache kuwa mshikamanifu kwa Mungu. (Mt. 4:1-11) Shetani alikuwa ameazimia kumfanya Yesu atende dhambi ili asiweze kulipia fidia. Wakati wa huduma yake duniani, Yesu alivumilia majaribu mengine pia. Maadui wake walimtesa na walijaribu kumuua. (Luka 4:28, 29; 13:31) Alihitaji kuvumilia udhaifu wa wafuasi wake. (Marko 9:33, 34) Alipokuwa akihukumiwa kifo, aliteswa na kudhihakiwa. Kisha aliuawa kwa njia ya kuaibisha na yenye maumivu makali sana. (Ebr. 12:1-3) Alipokuwa kwenye mti wa mateso alilazimika kuvumilia mateso makali, bila kuwa na ulinzi wa Yehova. (Mt. 27:46) Ni wazi kwamba Yesu alijidhabihu sana ili kutoa uhai wake kuwa fidia. Je, hatuchochewi kumpenda sana Yesu tunapotafakari jinsi alivyojidhabihu sana kwa hiari kwa ajili yetu? w24.01 10-11 ¶7-9
Jumanne, Agosti 26
Wote walio na haraka kwa hakika watakuwa maskini.—Met. 21:5.
Kuwa wenye subira kunatusaidia tunaposhughulika na wengine. Hutusaidia kuwasikiliza wengine kwa makini wanapozungumza. (Yak. 1:19) Pia, subira huendeleza amani. Hutulinda dhidi ya kutenda haraka-haraka na kusema jambo lisilo la fadhili tunapokuwa na mkazo. Na ikiwa tuna subira, hatutakuwa wepesi wa hasira mtu fulani anapotukasirisha. Badala ya kulipiza kisasi, ‘tutaendelea kuvumiliana na kusameheana kwa hiari.’ (Kol. 3:12, 13) Pia, subira inaweza kutusaidia kufanya maamuzi mazuri. Badala ya kutenda haraka-haraka au kuongozwa na hisia, tutatumia muda kufanya utafiti na kuchanganua maamuzi mbalimbali tunayoweza kufanya. Kwa mfano, ikiwa tunatafuta kazi, huenda tukashawishiwa kukubali kazi ya kwanza ambayo tunapata. Hata hivyo, ikiwa tuna subira tutatumia muda kuchunguza jinsi kazi hiyo itakavyoathiri familia yetu na hali yetu ya kiroho. Tunapokuwa na subira, tunaweza kuepuka kufanya uamuzi mbaya. w23.08 22 ¶8-9