Jumamosi, Agosti 23
Siku ya Yehova inakuja kama vile mwizi anavyokuja usiku.—1 The. 5:2.
Biblia inapozungumza kuhusu “siku ya Yehova,” inarejelea wakati ambapo Yehova anawaharibu maadui wake na kuwaokoa watu wake. Zamani, pindi fulani, Yehova alileta hukumu juu ya mataifa. (Isa. 13:1, 6; Eze. 13:5; Sef. 1:8) Katika nyakati zetu, “siku ya Yehova” itaanza wakati ambapo Babiloni Mkubwa atashambuliwa na itakwisha katika vita vya Har–Magedoni. Ili tuokoke “siku” hiyo, tunahitaji kujitayarisha sasa. Yesu alitufundisha kwamba hatupaswi tu kuwa tayari kwa ajili ya “dhiki kuu” bali pia ‘tuendelee kuwa tayari.’ (Mt. 24:21; Luka 12:40) Katika barua yake ya kwanza iliyoongozwa na roho takatifu ambayo aliwaandikia Wathesalonike, mtume Paulo alitumia mifano kadhaa kuwasaidia Wakristo waendelee kuwa tayari kwa ajili ya siku kuu ya Yehova ya hukumu. Paulo alijua kamba siku ya Yehova haingefika wakati huo. (2 The. 2:1-3) Ingawa hivyo, aliwahimiza ndugu zake wajitayarishe kwa ajili ya siku hiyo kana kwamba ingekuja kesho, na sisi pia tunahitaji kufuata shauri hilo. w23.06 8 ¶1-2
Jumapili, Agosti 24
Ndugu zangu wapendwa, iweni imara, thabiti.—1 Kor. 15:58.
Mwishoni mwa miaka ya 1970, jengo lenye ghorofa 60 lilijengwa hatua kwa hatua huko Tokyo, Japani. Watu walijiuliza jengo hilo lingewezaje kuhimili matetemeko ya ardhi yanayotokea mara kwa mara katika jiji hilo. Siri ilikuwa nini? Mainjinia walikuwa wamebuni jengo hilo liwe imara lakini lenye uwezo wa kunyumbulika ili lihimili mitikisiko ya tetemeko la ardhi. Wakristo ni kama ghorofa hilo refu. Jinsi gani? Mkristo anapaswa kudumisha usawaziko kati ya kuwa imara na kunyumbulika. Anapaswa kuwa imara na thabiti na kuazimia kuendelea kutii sheria na viwango vya Yehova. Anakuwa “tayari kutii” na halegezi msimamo wake. Kwa upande mwingine, anahitaji kuwa mwenye “usawaziko,” au mwenye kunyumbulika, ikiwa hali inaruhusu au hata anapohitajika kufanya hivyo. (Yak. 3:17) Mkristo ambaye amejifunza kuwa na maoni hayo yenye usawaziko ataepuka kushikilia sana maoni yake au kuendekeza mambo yasiyofaa. w23.07 14 ¶1-2
Jumatatu, Agosti 25
Mnampenda ingawa hamkumwona kamwe.—1 Pet. 1:8
Yesu alihitaji kusimama imara dhidi ya vishawishi vya Shetani Ibilisi, kutia ndani mashambulizi ya moja kwa moja ambayo yangeweza kufanya aache kuwa mshikamanifu kwa Mungu. (Mt. 4:1-11) Shetani alikuwa ameazimia kumfanya Yesu atende dhambi ili asiweze kulipia fidia. Wakati wa huduma yake duniani, Yesu alivumilia majaribu mengine pia. Maadui wake walimtesa na walijaribu kumuua. (Luka 4:28, 29; 13:31) Alihitaji kuvumilia udhaifu wa wafuasi wake. (Marko 9:33, 34) Alipokuwa akihukumiwa kifo, aliteswa na kudhihakiwa. Kisha aliuawa kwa njia ya kuaibisha na yenye maumivu makali sana. (Ebr. 12:1-3) Alipokuwa kwenye mti wa mateso alilazimika kuvumilia mateso makali, bila kuwa na ulinzi wa Yehova. (Mt. 27:46) Ni wazi kwamba Yesu alijidhabihu sana ili kutoa uhai wake kuwa fidia. Je, hatuchochewi kumpenda sana Yesu tunapotafakari jinsi alivyojidhabihu sana kwa hiari kwa ajili yetu? w24.01 10-11 ¶7-9