Jumatano, Agosti 27
Ninaona ndani ya mwili wangu sheria nyingine ikipigana na sheria ya akili yangu na kunichukua mateka kwa sheria ya dhambi iliyo ndani ya mwili wangu.—Rom. 7:23.
Ukihisi umevunjika moyo kwa sababu ya mwelekeo wako wa kutenda dhambi, kufikiria kuhusu ahadi uliyomwahidi Yehova ulipojiweka wakfu kwake kutaimarisha azimio lako la kupambana dhidi ya kishawishi. Jinsi gani? Unapojiweka wakfu kwa Yehova, unajikana mwenyewe. Hilo linamaanisha kukataa tamaa na malengo ya kibinafsi ambayo hayampendezi Yehova. (Mt. 16:24) Hivyo, unapokabili jaribu huhitaji kutumia muda mwingi kufikiria cha kufanya. Tayari utakuwa umeamua cha kufanya—kuwa mwaminifu kwa Yehova. Utashikamana na azimio lako la kumpendeza Yehova. Kwa njia hiyo, utakuwa kama Ayubu. Hata ingawa alikabili majaribu makali sana, alisema hivi kwa uhakika: “Sitaukana utimilifu wangu!”—Ayu. 27:5. w24.03 9 ¶6-7
Alhamisi, Agosti 28
Yehova yuko karibu na wote wanaomwitia, wote wanaomwitia yeye katika ukweli.—Zab. 145:18.
Yehova, “Mungu wa upendo,” yuko pamoja nasi! (2 Kor. 13:11) Anapendezwa nasi kibinafsi. Tunasadiki kwamba “[tumezungukwa] na upendo Wake mshikamanifu.” (Zab. 32:10) Kadiri tunavyotafakari jinsi ambavyo ameonyesha upendo wake kwetu, ndivyo anavyokuwa halisi zaidi kwetu, na tunahisi yuko karibu zaidi nasi. Tunaweza kumkaribia kwa uhuru na kumweleza jinsi tunavyohitaji sana upendo wake. Tunaweza kumweleza mahangaiko yetu yote, tukiwa na uhakika kwamba anatuelewa na kwamba yuko tayari kutusaidia. (Zab. 145:19) Kama tunavyovutiwa kuota moto katika siku yenye baridi, ndivyo tunavyovutiwa na upendo mwororo wa Yehova. Ingawa upendo wa Yehova ni wenye nguvu, ni mwororo pia. Kwa hiyo, uruhusu upendo mwororo wa Yehova maishani mwako. Kwa sababu Yehova anatupenda, acheni sisi sote tuseme hivi kwa sauti: “Ninampenda Yehova”!—Zab. 116:1. w24.01 31 ¶19-20
Ijumaa, Agosti 29
Nimewajulisha jina lako.—Yoh. 17:26.
Yesu alifanya mengi zaidi ya kuwaambia tu watu kwamba jina la Mungu ni Yehova. Wayahudi ambao Yesu aliwafundisha tayari walilijua jina la Mungu. Lakini Yesu ndiye aliyekuwa mstari wa mbele akiwa yule ‘aliyeeleza kumhusu.’ (Yoh. 1:17, 18) Kwa mfano, Maandiko ya Kiebrania yanafunua kwamba Yehova ni mwenye rehema na huruma. (Kut. 34:5-7) Yesu alifafanua kweli hiyo hata zaidi aliposimulia kuhusu mfano wa mwana mpotevu na baba yake. Tunaposoma kuhusu jinsi baba huyo anavyomwona mwana wake aliyetubu “akiwa mbali,” anavyokimbia ili kukutana naye, anavyomkumbatia, na kumsamehe kutoka moyoni, tunapata picha kamili zaidi ya rehema na huruma ya Yehova. (Luka 15:11-32) Yesu aliwasaidia wengine waelewe vizuri kabisa utu wa Baba yake. w24.02 10 ¶8-9