Jumapili, Septemba 14
Kufahamu kikamili upana na urefu na kimo na kina.—Efe. 3:18.
Unapotaka kununua nyumba, ungependa kuichunguza kwa kina nyumba hiyo wewe mwenyewe. Tunaweza kufanya jambo kama hilo tunaposoma na kujifunza Biblia. Ikiwa utaisoma haraka-haraka, huenda ukajifunza habari za msingi tu, yaani, “mambo ya msingi ya maneno matakatifu ya Mungu.” (Ebr. 5:12) Badala yake, kama ilivyokuwa kwa ile nyumba, unapaswa kuingia “ndani” na kuichunguza Biblia kwa makini ili uielewe kikamili zaidi. Njia bora ya kujifunza Biblia ni kuona jinsi sehemu mbalimbali za ujumbe wake zinavyohusiana. Jitahidi kuelewa ni kweli gani ambazo unaamini na kwa nini unaamini kweli hizo. Ili kuelewa kikamili Neno la Mungu, tunapaswa kujifunza kweli zenye kina za Biblia. Mtume Paulo aliwahimiza ndugu na dada zake Wakristo wajifunze Neno la Mungu kwa bidii ili “[wafahamu] kikamili upana na urefu na kimo na kina” cha ile kweli, kisha wangekuwa na “mizizi na kuimarishwa” katika imani yao. (Efe. 3:14-19) Sisi tunahitaji kufanya hivyo pia. w23.10 18 ¶1-3
Jumatatu, Septemba 15
Akina ndugu, fuateni mfano wa manabii waliopatwa na uovu na kuonyesha subira na ambao walisema katika jina la Yehova.—Yak. 5:10.
Biblia ina mifano mingi ya watu walioonyesha subira. Kwa nini usijiwekee lengo la kufanya utafiti kuhusu mifano ambayo watu hao walituwekea? Kwa mfano, ingawa Daudi alitiwa mafuta alipokuwa na umri mdogo ili awe mfalme wa wakati ujao wa Israeli, alisubiri kwa miaka mingi kabla ya kuanza kutawala akiwa mfalme. Simeoni na Ana walimwabudu Yehova kwa uaminifu walipokuwa wakimsubiri Masihi aliyeahidiwa. (Luka 2:25, 36-38) Unapochunguza masimulizi hayo, tafuta majibu ya maswali yafuatayo: Ni nini ambacho huenda kilimsaidia mtu huyo awe mwenye subira? Alinufaikaje kwa kuonyesha subira? Ninawezaje kumwiga? Huenda pia ukanufaika kwa kujifunza kutokana na wale ambao hawakuonyesha subira. (1 Sam. 13:8-14) Unaweza kujiuliza hivi: ‘Ni nini kilichofanya wakose subira? Walipatwa na matokeo gani mabaya?’ w23.08 25 ¶15
Jumanne, Septemba 16
Tumeamini na tumejua kwamba wewe ndiye Mtakatifu wa Mungu.—Yoh. 6:69.
Mtume Petro alikuwa mshikamanifu; hakuruhusu jambo lolote limzuie kuendelea kumfuata Yesu. Kwa mfano, pindi fulani alionyesha ushikamanifu wake Yesu aliposema jambo ambalo wanafunzi wake hawakuelewa. (Yoh. 6:68) Bila kusubiri ufafanuzi, wengi waliacha kumfuata Yesu. Lakini Petro hakuacha. Alitambua kwamba Yesu tu ndiye aliyekuwa na “maneno ya uzima wa milele.” Yesu alijua kwamba Petro na wale mitume wengine wangemwacha. Ingawa hivyo, Yesu alikuwa na uhakika kwamba Petro angerudi na kuendelea kuwa mwaminifu. (Luka 22:31, 32) Yesu alielewa kwamba “roho inataka, lakini mwili ni dhaifu.” (Marko 14:38) Hivyo, hata baada ya Petro kukana kwamba hamjui Yesu, Yesu hakumwacha mtume huyo. Baada ya kufufuliwa Yesu alimtokea Petro—inaonekana Petro alikuwa peke yake. (Marko 16:7; Luka 24:34; 1 Kor. 15:5) Hilo lilimwimarisha mtume huyo ambaye alikuwa amehuzunika sana! w23.09 22 ¶9-10