Jumatatu, Septemba 15
Akina ndugu, fuateni mfano wa manabii waliopatwa na uovu na kuonyesha subira na ambao walisema katika jina la Yehova.—Yak. 5:10.
Biblia ina mifano mingi ya watu walioonyesha subira. Kwa nini usijiwekee lengo la kufanya utafiti kuhusu mifano ambayo watu hao walituwekea? Kwa mfano, ingawa Daudi alitiwa mafuta alipokuwa na umri mdogo ili awe mfalme wa wakati ujao wa Israeli, alisubiri kwa miaka mingi kabla ya kuanza kutawala akiwa mfalme. Simeoni na Ana walimwabudu Yehova kwa uaminifu walipokuwa wakimsubiri Masihi aliyeahidiwa. (Luka 2:25, 36-38) Unapochunguza masimulizi hayo, tafuta majibu ya maswali yafuatayo: Ni nini ambacho huenda kilimsaidia mtu huyo awe mwenye subira? Alinufaikaje kwa kuonyesha subira? Ninawezaje kumwiga? Huenda pia ukanufaika kwa kujifunza kutokana na wale ambao hawakuonyesha subira. (1 Sam. 13:8-14) Unaweza kujiuliza hivi: ‘Ni nini kilichofanya wakose subira? Walipatwa na matokeo gani mabaya?’ w23.08 25 ¶15
Jumanne, Septemba 16
Tumeamini na tumejua kwamba wewe ndiye Mtakatifu wa Mungu.—Yoh. 6:69.
Mtume Petro alikuwa mshikamanifu; hakuruhusu jambo lolote limzuie kuendelea kumfuata Yesu. Kwa mfano, pindi fulani alionyesha ushikamanifu wake Yesu aliposema jambo ambalo wanafunzi wake hawakuelewa. (Yoh. 6:68) Bila kusubiri ufafanuzi, wengi waliacha kumfuata Yesu. Lakini Petro hakuacha. Alitambua kwamba Yesu tu ndiye aliyekuwa na “maneno ya uzima wa milele.” Yesu alijua kwamba Petro na wale mitume wengine wangemwacha. Ingawa hivyo, Yesu alikuwa na uhakika kwamba Petro angerudi na kuendelea kuwa mwaminifu. (Luka 22:31, 32) Yesu alielewa kwamba “roho inataka, lakini mwili ni dhaifu.” (Marko 14:38) Hivyo, hata baada ya Petro kukana kwamba hamjui Yesu, Yesu hakumwacha mtume huyo. Baada ya kufufuliwa Yesu alimtokea Petro—inaonekana Petro alikuwa peke yake. (Marko 16:7; Luka 24:34; 1 Kor. 15:5) Hilo lilimwimarisha mtume huyo ambaye alikuwa amehuzunika sana! w23.09 22 ¶9-10
Jumatano, Septemba 17
Wenye furaha ni wale ambao matendo yao ya kuasi sheria yamesamehewa na ambao dhambi zao zimefunikwa.—Rom. 4:7.
Mungu anasamehe au kufunika dhambi za wale wanaoweka imani kwake. Anawasamehe kabisa na hatahesabu dhambi zao kamwe. (Zab. 32:1, 2) Yehova anawaona watu hao kuwa hawana hatia na waadilifu kwa msingi wa imani yao. Ingawa Abrahamu, Daudi, na waabudu wengine waaminifu wa Mungu walitangazwa kuwa waadilifu, bado walikuwa watenda dhambi wasio wakamilifu. Lakini kwa sababu ya imani yao, Mungu aliwaona kuwa wasio na hatia hasa alipowalinganisha na wale ambao hawakuwa na imani kwake. (Efe. 2:12) Kama mtume Paulo anavyoeleza waziwazi kwenye barua yake, ni lazima mtu awe na imani ili kuwa na uhusiano wa kibinafsi pamoja na Mungu. Ndivyo ilivyokuwa kwa Abrahamu na Daudi, na ni hivyo kwetu pia. w23.12 3 ¶6-7