Jumapili, Septemba 21
Vilevile wanawake wanapaswa . . . wawe wenye kiasi katika mazoea, na waaminifu katika mambo yote.—1 Tim. 3:11
Tunastaajabishwa na jinsi mtoto anavyokua haraka na kuwa mtu mzima. Inaonekana ni kama watoto wanakua tu bila kufanya jitihada yoyote. Hata hivyo, jitihada inahitajika ili kuwa Mkristo mkomavu. (1 Kor. 13:11; Ebr. 6:1) Ili kufikia lengo hilo, tunahitaji kuwa na uhusiano wa karibu pamoja na Yehova. Pia, tunahitaji roho takatifu ili tusitawishe sifa zinazompendeza Yehova, tuwe na ustadi unaofaa, na tujitayarishe kwa ajili ya majukumu ya wakati ujao. (Met. 1:5) Yehova alimuumba mwanamume na mwanamke. (Mwa. 1:27) Ni wazi kwamba wanaume na wanawake wanatofautiana kimwili, lakini wanatofautiana kwa njia nyingine pia. Kwa mfano, Yehova aliwapatia wanaume na wanawake majukumu hususa, hivyo wanahitaji sifa na ustadi ili waweze kutimiza majukumu yao.—Mwa. 2:18. w23.12 18 ¶1-2
Jumatatu, Septemba 22
Fanyeni wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote, mkiwabatiza katika jina la Baba na la Mwana.—Mt. 28:19.
Je, Yesu alitaka wengine watumie jina la kibinafsi la Baba yake? Bila shaka. Huenda baadhi ya viongozi wa dini wa siku za Yesu waliamini kwamba jina la Mungu lilikuwa takatifu sana hivi kwamba halikupaswa kutamkwa, lakini Yesu hakuruhusu desturi hizo zisizo za kimaandiko zimzuie kuliheshimu jina la Baba yake. Fikiria wakati ambapo Yesu alimponya mwanamume mwenye roho waovu katika eneo la Wagerasene. Watu katika eneo hilo waliogopa na kumsihi Yesu aondoke, hivyo hakubaki katika eneo hilo. (Marko 5:16, 17) Lakini bado Yesu alitaka jina la Yehova lijulikane huko. Hivyo, alimwambia mwanamume aliyemponya awaambie watu mambo ambayo Yehova alikuwa amefanya, si mambo ambayo Yesu alikuwa amefanya. (Marko 5:19) Leo pia, anataka tufanye vivyo hivyo, yaani, tuwajulishe watu ulimwenguni pote kuhusu jina la Baba yake! (Mt. 24:14; 28:20) Tunapofanya sehemu yetu, tunamfurahisha Mfalme wetu, Yesu. w24.02 10 ¶10
Jumanne, Septemba 23
Umestahimili kwa ajili ya jina langu.—Ufu. 2:3.
Tuna pendeleo kubwa sana kuwa sehemu ya tengenezo la Yehova katika siku hizi za mwisho zilizo ngumu. Hali za ulimwengu zinavyozidi kuzorota, Yehova anatupatia familia ya ndugu na dada iliyo na umoja. (Zab. 133:1) Anatusaidia tuwe na maisha ya familia yenye furaha. (Efe. 5:33–6:1) Na anatupatia ufahamu na hekima tunayohitaji ili tuwe na amani ya kweli ya moyoni na akilini. Hata hivyo, ni lazima tujitahidi ili tuendelee kumtumikia Yehova kwa uaminifu. Kwa nini? Kwa sababu nyakati nyingine tunaweza kukasirishwa na kutokamilika kwa wengine. Pia, tunaweza kuvunjika moyo kwa sababu ya makosa tunayofanya, hasa ikiwa tunarudia makosa yaleyale mara kwa mara. Tunahitaji kuendelea kumtumikia Yehova kwa uaminifu (1) mwabudu mwenzetu anapotukosea, (2) mwenzi wetu wa ndoa anapotuvunja moyo, na (3) tunapovunjika moyo kwa sababu ya makosa yetu. w24.03 14 ¶1-2