Jumanne, Septemba 23
Umestahimili kwa ajili ya jina langu.—Ufu. 2:3.
Tuna pendeleo kubwa sana kuwa sehemu ya tengenezo la Yehova katika siku hizi za mwisho zilizo ngumu. Hali za ulimwengu zinavyozidi kuzorota, Yehova anatupatia familia ya ndugu na dada iliyo na umoja. (Zab. 133:1) Anatusaidia tuwe na maisha ya familia yenye furaha. (Efe. 5:33–6:1) Na anatupatia ufahamu na hekima tunayohitaji ili tuwe na amani ya kweli ya moyoni na akilini. Hata hivyo, ni lazima tujitahidi ili tuendelee kumtumikia Yehova kwa uaminifu. Kwa nini? Kwa sababu nyakati nyingine tunaweza kukasirishwa na kutokamilika kwa wengine. Pia, tunaweza kuvunjika moyo kwa sababu ya makosa tunayofanya, hasa ikiwa tunarudia makosa yaleyale mara kwa mara. Tunahitaji kuendelea kumtumikia Yehova kwa uaminifu (1) mwabudu mwenzetu anapotukosea, (2) mwenzi wetu wa ndoa anapotuvunja moyo, na (3) tunapovunjika moyo kwa sababu ya makosa yetu. w24.03 14 ¶1-2
Jumatano, Septemba 24
Kwa kadiri ambavyo tumefanya maendeleo, na tuendelee kutembea kwa utaratibu katika mwendo huohuo.—Flp. 3:16.
Mara kwa mara, utasikia kuhusu mambo yaliyoonwa ya ndugu na dada ambao wamepanua utumishi wao mtakatifu. Labda walihudhuria Shule ya Waeneza-Injili wa Ufalme au walihamia maeneo yenye uhitaji mkubwa. Ikiwa hali zako zinakuruhusu, hilo ni lengo zuri sana la kujiwekea. Watu wa Yehova wanatafuta fursa mbalimbali za kupanua huduma yao. (Mdo. 16:9) Namna gani ikiwa hali zako za sasa hazikuruhusu kufanya hivyo? Usihisi kwamba wewe ni duni kuliko wale wanaofanya hivyo. (Mt. 10:22) Usisahau kwamba unamfurahisha sana Yehova unapofanya utumishi wake kwa bidii kulingana na uwezo na hali zako. Hiyo ni njia muhimu ya kuendelea kumfuata Yesu baada ya ubatizo.—Zab. 26:1. w24.03 10 ¶11
Alhamisi, Septemba 25
Alitusamehe kwa fadhili makosa yetu yote.—Kol. 2:13.
Baba yetu wa mbinguni anaahidi kwamba atatusamehe ikiwa tutatubu. (Zab. 86:5) Hivyo, ikiwa tumetubu dhambi zetu kikweli, tunaweza kuwa na uhakika kwamba jambo ambalo Yehova ametuahidi ni la kweli, naye ametusamehe. Kumbuka kwamba Yehova ana usawaziko na ni mwenye kunyumbulika. Kamwe hatarajii tufanye mengi zaidi ya yale tunayoweza kutimiza. Anathamini jambo lolote tunalofanya kwa ajili yake maadamu tumempa kilicho bora kulingana na uwezo wetu. Pia, tafakari kuhusu watu katika Biblia ambao walimtumikia Yehova kwa moyo wote. Mfikirie mtume Paulo. Kwa miaka mingi alifanya kazi kwa bidii, akisafiri umbali wa maelfu ya kilomita na kuanzisha makutaniko mengi. Hata hivyo, hali zake zilipobadilika na akashindwa kutimiza mengi zaidi katika kazi yake ya kuhubiri, je, alipoteza kibali cha Yehova? Hapana. Aliendelea kufanya yote aliyoweza, na Yehova alimbariki. (Mdo. 28:30, 31) Vivyo hivyo, wakati mwingine mambo tunayomtolea Yehova yanaweza kutofautiana. Lakini jambo muhimu kwake ni nia yetu. w24.03 27 ¶7, 9