Alhamisi, Septemba 25
Alitusamehe kwa fadhili makosa yetu yote.—Kol. 2:13.
Baba yetu wa mbinguni anaahidi kwamba atatusamehe ikiwa tutatubu. (Zab. 86:5) Hivyo, ikiwa tumetubu dhambi zetu kikweli, tunaweza kuwa na uhakika kwamba jambo ambalo Yehova ametuahidi ni la kweli, naye ametusamehe. Kumbuka kwamba Yehova ana usawaziko na ni mwenye kunyumbulika. Kamwe hatarajii tufanye mengi zaidi ya yale tunayoweza kutimiza. Anathamini jambo lolote tunalofanya kwa ajili yake maadamu tumempa kilicho bora kulingana na uwezo wetu. Pia, tafakari kuhusu watu katika Biblia ambao walimtumikia Yehova kwa moyo wote. Mfikirie mtume Paulo. Kwa miaka mingi alifanya kazi kwa bidii, akisafiri umbali wa maelfu ya kilomita na kuanzisha makutaniko mengi. Hata hivyo, hali zake zilipobadilika na akashindwa kutimiza mengi zaidi katika kazi yake ya kuhubiri, je, alipoteza kibali cha Yehova? Hapana. Aliendelea kufanya yote aliyoweza, na Yehova alimbariki. (Mdo. 28:30, 31) Vivyo hivyo, wakati mwingine mambo tunayomtolea Yehova yanaweza kutofautiana. Lakini jambo muhimu kwake ni nia yetu. w24.03 27 ¶7, 9
Ijumaa, Septemba 26
Asubuhi na mapema, [Yesu] akaenda mahali pasipo na watu, naye akaanza kusali.—Marko 1:35.
Kupitia sala alizotoa kwa Yehova, Yesu aliwawekea wanafunzi wake mfano. Katika huduma yake yote, Yesu alisali mara nyingi. Alihitaji kutenga muda wa kusali kwa sababu mara nyingi alikuwa na shughuli nyingi na alizungukwa na watu wengi. (Marko 6:31, 45, 46) Aliamka asubuhi na mapema ili awe na muda wa kusali akiwa peke yake. Katika pindi moja, alisali usiku kucha kabla ya kufanya uamuzi muhimu. (Luka 6:12, 13) Na Yesu alisali tena na tena usiku wa kabla ya kifo chake alipokuwa akikazia fikira kutimiza sehemu ngumu zaidi ya mgawo wake duniani. (Mt. 26:39, 42, 44) Mfano wa Yesu unatufundisha kwamba hata tuwe na shughuli nyingi kadiri gani, tunahitaji kutenga muda wa kusali. Kama Yesu, tunahitaji kupanga muda wa kusali—tunaweza kuamka asubuhi na mapema ili kusali au tunaweza kusali usiku. Tunapofanya hivyo, tunamwonyesha Yehova kwamba tunathamini zawadi hii ya pekee. w23.05 3 ¶4-5
Jumamosi, Septemba 27
Upendo wa Mungu umemiminwa ndani ya mioyo yetu kupitia roho takatifu, ambayo tulipewa.—Rom. 5:5
Ona neno “umemiminwa” ambalo limetumiwa kwenye andiko la leo. Kitabu kimoja cha marejeo kinalinganisha neno “umemiminwa” na kijito cha maji, yaani, kinachotiririka maji mengi. Mfano huo unaonyesha jinsi Yehova anavyowapenda sana watiwa-mafuta! Watiwa-mafuta wanajua kwamba “wanapendwa na Mungu.” (Yuda 1) Mtume Yohana alieleza hisia zao alipoandika hivi: “Oneni upendo ambao Baba ametuonyesha, kwamba tunapaswa kuitwa watoto wa Mungu!” (1 Yoh. 3:1) Je, Yehova anawapenda tu watiwa-mafuta? La, Yehova amethibitisha upendo wake kwetu sisi sote. Ni nini kinachotuhakikishia zaidi kwamba Yehova anatupenda? Fidia—wonyesho mkubwa zaidi wa upendo katika ulimwengu wote!—Yoh. 3:16; Rom. 5:8. w24.01 28 ¶9-10