Ijumaa, Septemba 26
Asubuhi na mapema, [Yesu] akaenda mahali pasipo na watu, naye akaanza kusali.—Marko 1:35.
Kupitia sala alizotoa kwa Yehova, Yesu aliwawekea wanafunzi wake mfano. Katika huduma yake yote, Yesu alisali mara nyingi. Alihitaji kutenga muda wa kusali kwa sababu mara nyingi alikuwa na shughuli nyingi na alizungukwa na watu wengi. (Marko 6:31, 45, 46) Aliamka asubuhi na mapema ili awe na muda wa kusali akiwa peke yake. Katika pindi moja, alisali usiku kucha kabla ya kufanya uamuzi muhimu. (Luka 6:12, 13) Na Yesu alisali tena na tena usiku wa kabla ya kifo chake alipokuwa akikazia fikira kutimiza sehemu ngumu zaidi ya mgawo wake duniani. (Mt. 26:39, 42, 44) Mfano wa Yesu unatufundisha kwamba hata tuwe na shughuli nyingi kadiri gani, tunahitaji kutenga muda wa kusali. Kama Yesu, tunahitaji kupanga muda wa kusali—tunaweza kuamka asubuhi na mapema ili kusali au tunaweza kusali usiku. Tunapofanya hivyo, tunamwonyesha Yehova kwamba tunathamini zawadi hii ya pekee. w23.05 3 ¶4-5
Jumamosi, Septemba 27
Upendo wa Mungu umemiminwa ndani ya mioyo yetu kupitia roho takatifu, ambayo tulipewa.—Rom. 5:5
Ona neno “umemiminwa” ambalo limetumiwa kwenye andiko la leo. Kitabu kimoja cha marejeo kinalinganisha neno “umemiminwa” na kijito cha maji, yaani, kinachotiririka maji mengi. Mfano huo unaonyesha jinsi Yehova anavyowapenda sana watiwa-mafuta! Watiwa-mafuta wanajua kwamba “wanapendwa na Mungu.” (Yuda 1) Mtume Yohana alieleza hisia zao alipoandika hivi: “Oneni upendo ambao Baba ametuonyesha, kwamba tunapaswa kuitwa watoto wa Mungu!” (1 Yoh. 3:1) Je, Yehova anawapenda tu watiwa-mafuta? La, Yehova amethibitisha upendo wake kwetu sisi sote. Ni nini kinachotuhakikishia zaidi kwamba Yehova anatupenda? Fidia—wonyesho mkubwa zaidi wa upendo katika ulimwengu wote!—Yoh. 3:16; Rom. 5:8. w24.01 28 ¶9-10
Jumapili, Septemba 28
Maadui wangu watakimbia siku nitakayoomba msaada. Nina hakika kuhusu jambo hili: Mungu yuko upande wangu.—Zab. 56:9.
Mstari huo unafunua njia iliyomsaidia Daudi kushinda woga wake. Ingawa uhai wake ulikuwa hatarini, alitafakari mambo ambayo Yehova angemfanyia wakati ujao. Daudi alijua kwamba Yehova angemwokoa kwa wakati unaofaa. Isitoshe, Yehova alikuwa ametangaza kwamba Daudi angekuwa mfalme anayefuata wa Israeli. (1 Sam. 16:1, 13) Daudi alikuwa na uhakika kwamba jambo lolote ambalo Yehova aliahidi lingetimia. Yehova ameahidi atakufanyia nini? Hatutarajii kwamba atukinge kutokana na matatizo yote. Lakini kumbuka kwamba majaribu yoyote ambayo huenda ukakabili katika mfumo huu wa mambo, Yehova atayaondoa katika dunia mpya inayokuja. (Isa. 25:7-9) Bila shaka Muumba wetu ana nguvu za kufufua wafu, kutuponya, na kuondoa wapinzani wote.—1 Yoh. 4:4. w24.01 6 ¶12-13