Jumatatu, Septemba 29
Mwenye furaha ni mtu ambaye amesamehewa kosa lake, ambaye dhambi yake imefunikwa.—Zab. 32:1.
Fikiria kuhusu wakfu na ubatizo wako. Ulichukua hatua hizo kwa sababu ulitaka kusimama upande wa Yehova. Kumbuka mambo ambayo yalikusaidia kusadiki kwamba umepata kweli. Ulipata ujuzi sahihi kumhusu Yehova na ukaanza kumheshimu na kumpenda akiwa Baba yako wa mbinguni. Ulisitawisha imani na ukachochewa kutubu. Moyo wako ulikuchochea kuacha mazoea yasiyofaa na kuishi kulingana na mapenzi ya Mungu. Ulifarijika ulipotambua kwamba Mungu amekusamehe. (Zab. 32:2) Ulihudhuria mikutano ya Kikristo na ukaanza kuwaambia wengine kuhusu mambo mazuri uliyokuwa unajifunza. Sasa ukiwa Mkristo aliyejiweka wakfu na kubatizwa, unatembea kwenye barabara ya uzima ukiwa umeazimia kuendelea kutembea katika barabara hiyo. (Mt. 7:13, 14) Na usimame imara na thabiti katika ujitoaji wako kwa Yehova na sikuzote uendelee kutii amri zake. w23.07 17 ¶14; 19 ¶19
Jumanne, Septemba 30
Mungu ni mwaminifu, naye hatawaacha mjaribiwe kupita mnavyoweza kuhimili, bali pamoja na majaribu hayo ataifanya pia njia ya kutokea ili mweze kuyavumilia.—1 Kor. 10:13.
Ukitafakari sala uliyotoa ulipojiweka wakfu kwa Yehova, utapata nguvu za kushinda kishawishi chochote. Kwa mfano, je, utamchezea kimapenzi mwenzi wa ndoa wa mtu mwingine? Bila shaka hapana! Tayari ulishamwahidi Yehova kwamba hutafanya jambo kama hilo. Ikiwa hutaruhusu tamaa mbaya zisitawi, hutahitaji kupambana baadaye ili kuzing’oa. ‘Utajiepusha’ na “kijia cha waovu.” (Met. 4:14, 15) Ukikumbuka azimio la Yesu la kumpendeza Baba yake, utakataa haraka na kwa uthabiti jambo lolote ambalo unajua halitampendeza Mungu ambaye umejiweka wakfu kwake. (Mt. 4:10; Yoh. 8:29). Ukweli ni kwamba majaribu na vishawishi vinakupa nafasi ya kuonyesha kwamba umeazimia ‘kuendelea kumfuata’ Yesu. Unapofanya hivyo, unaweza kuwa na uhakika kwamba Yehova atakusaidia. w24.03 9-10 ¶8-10
Jumatano, Oktoba 1
Hekima inayotoka juu . . . [iko] tayari kutii.—Yak. 3:17.
Je, wakati mwingine ni vigumu kwako kutii? Mfalme Daudi alikabili changamoto hiyo naye alisali hivi kwa Mungu: “Chochea ndani yangu utayari wa kukutii.” (Zab. 51:12) Daudi alimpenda Yehova. Hata hivyo, wakati mwingine ilikuwa vigumu kwake kutii, na inakuwa hivyo pia kwetu. Kwa nini? Kwanza, tumerithi mwelekeo wa kutotii. Pili, sikuzote Shetani anajaribu kutuchochea tuasi, kama yeye alivyofanya. (2 Kor. 11:3) Tatu, tumezungukwa na ulimwengu huu wenye roho ya uasi, “roho ambayo sasa inafanya kazi katika wana wa kutotii.” (Efe. 2:2) Tunapaswa kujitahidi kushinda mwelekeo wetu wa kutenda dhambi na pia kupinga mkazo wa kutotii unaotoka kwa Ibilisi na ulimwengu huu. Tunapaswa kujitahidi kumtii Yehova na wale ambao amewapatia mamlaka. w23.10 6 ¶1