Jumapili, Septemba 28
Maadui wangu watakimbia siku nitakayoomba msaada. Nina hakika kuhusu jambo hili: Mungu yuko upande wangu.—Zab. 56:9.
Mstari huo unafunua njia iliyomsaidia Daudi kushinda woga wake. Ingawa uhai wake ulikuwa hatarini, alitafakari mambo ambayo Yehova angemfanyia wakati ujao. Daudi alijua kwamba Yehova angemwokoa kwa wakati unaofaa. Isitoshe, Yehova alikuwa ametangaza kwamba Daudi angekuwa mfalme anayefuata wa Israeli. (1 Sam. 16:1, 13) Daudi alikuwa na uhakika kwamba jambo lolote ambalo Yehova aliahidi lingetimia. Yehova ameahidi atakufanyia nini? Hatutarajii kwamba atukinge kutokana na matatizo yote. Lakini kumbuka kwamba majaribu yoyote ambayo huenda ukakabili katika mfumo huu wa mambo, Yehova atayaondoa katika dunia mpya inayokuja. (Isa. 25:7-9) Bila shaka Muumba wetu ana nguvu za kufufua wafu, kutuponya, na kuondoa wapinzani wote.—1 Yoh. 4:4. w24.01 6 ¶12-13
Jumatatu, Septemba 29
Mwenye furaha ni mtu ambaye amesamehewa kosa lake, ambaye dhambi yake imefunikwa.—Zab. 32:1.
Fikiria kuhusu wakfu na ubatizo wako. Ulichukua hatua hizo kwa sababu ulitaka kusimama upande wa Yehova. Kumbuka mambo ambayo yalikusaidia kusadiki kwamba umepata kweli. Ulipata ujuzi sahihi kumhusu Yehova na ukaanza kumheshimu na kumpenda akiwa Baba yako wa mbinguni. Ulisitawisha imani na ukachochewa kutubu. Moyo wako ulikuchochea kuacha mazoea yasiyofaa na kuishi kulingana na mapenzi ya Mungu. Ulifarijika ulipotambua kwamba Mungu amekusamehe. (Zab. 32:2) Ulihudhuria mikutano ya Kikristo na ukaanza kuwaambia wengine kuhusu mambo mazuri uliyokuwa unajifunza. Sasa ukiwa Mkristo aliyejiweka wakfu na kubatizwa, unatembea kwenye barabara ya uzima ukiwa umeazimia kuendelea kutembea katika barabara hiyo. (Mt. 7:13, 14) Na usimame imara na thabiti katika ujitoaji wako kwa Yehova na sikuzote uendelee kutii amri zake. w23.07 17 ¶14; 19 ¶19
Jumanne, Septemba 30
Mungu ni mwaminifu, naye hatawaacha mjaribiwe kupita mnavyoweza kuhimili, bali pamoja na majaribu hayo ataifanya pia njia ya kutokea ili mweze kuyavumilia.—1 Kor. 10:13.
Ukitafakari sala uliyotoa ulipojiweka wakfu kwa Yehova, utapata nguvu za kushinda kishawishi chochote. Kwa mfano, je, utamchezea kimapenzi mwenzi wa ndoa wa mtu mwingine? Bila shaka hapana! Tayari ulishamwahidi Yehova kwamba hutafanya jambo kama hilo. Ikiwa hutaruhusu tamaa mbaya zisitawi, hutahitaji kupambana baadaye ili kuzing’oa. ‘Utajiepusha’ na “kijia cha waovu.” (Met. 4:14, 15) Ukikumbuka azimio la Yesu la kumpendeza Baba yake, utakataa haraka na kwa uthabiti jambo lolote ambalo unajua halitampendeza Mungu ambaye umejiweka wakfu kwake. (Mt. 4:10; Yoh. 8:29). Ukweli ni kwamba majaribu na vishawishi vinakupa nafasi ya kuonyesha kwamba umeazimia ‘kuendelea kumfuata’ Yesu. Unapofanya hivyo, unaweza kuwa na uhakika kwamba Yehova atakusaidia. w24.03 9-10 ¶8-10