Jumapili, Septemba 7
Alipokuwa angali mvulana, alianza kumtafuta Mungu wa Daudi babu yake.—2 Nya. 34:3.
Mfalme Yosia alikuwa tineja alipoanza kumtafuta Yehova. Alitaka kujifunza kumhusu Yehova na kufanya mapenzi Yake. Hata hivyo, maisha hayakuwa rahisi kwa mfalme huyo kijana. Alihitaji kuchukua msimamo upande wa ibada safi wakati ambapo ibada ya uwongo ilikuwa imeenea. Na kwa kweli, alifanya hivyo! Kabla Yosia hajafikisha umri wa miaka 20, alianza kuondoa ibada ya uwongo katika taifa hilo. (2 Nya. 34:1, 2) Hata ikiwa wewe ni kijana, unaweza kuamua kumwiga Yosia kwa kumtafuta Yehova na kujifunza kuthamini sifa Zake. Ukifanya hivyo, utachochewa kujiweka wakfu kwake. Kujiweka wakfu kutaathirije maisha yako ya kila siku? Luke, ambaye alibatizwa akiwa na umri wa miaka 14, anasema hivi: “Kuanzia sasa na kuendelea, nitatanguliza kumtumikia Yehova maishani mwangu na nitajitahidi kumfurahisha.” (Marko 12:30) Wewe pia utapata baraka ikiwa unatamani kufanya hivyo! w23.09 11 ¶12-13
Jumatatu, Septemba 8
Waheshimuni wale wanaofanya kazi kwa bidii miongoni mwenu na wanaowasimamia katika Bwana.—1 The. 5:12.
Mtume Paulo alipoandika barua hiyo, mwaka mmoja haukuwa umepita tangu kutaniko la Thesalonike lilipoanzishwa. Inaonekana kwamba wanaume waliowekwa rasmi hawakuwa na uzoefu na huenda walifanya makosa. Ingawa hivyo, walistahili kuheshimiwa. Dhiki kuu inapokaribia, huenda tukategemea hata zaidi mwongozo kutoka kwa wazee wa kutaniko kuliko ilivyo sasa. Huenda tukapoteza mawasiliano na makao makuu ya ulimwenguni pote au ofisi ya tawi; basi, ni jambo muhimu kujifunza sasa kuwapenda na kuwaheshimu wazee wa kutaniko. Hata jambo gani litokee, acheni tuendelee kutunza akili zetu, tusikazie fikira udhaifu wao, bali tukazie fikira kwamba Yehova anawaongoza wanaume hao waaminifu kupitia Kristo. Kama vile kofia ya chuma ilivyolinda kichwa cha mwanajeshi, tumaini letu la wokovu hulinda mawazo yetu. Tunatambua kwamba mambo yaliyo katika ulimwengu huu hayana thamani yoyote. (Flp. 3:8) Tumaini letu linatusaidia kuendelea kuwa watulivu na thabiti. w23.06 11-12 ¶11-12
Jumanne, Septemba 9
Mwanamke mpumbavu ana kelele. Yeye ni mjinga.—Met. 9:13.
Wale wanaosikia sauti ya “mwanamke mpumbavu” wanahitaji kufanya uamuzi huu: Je, watakubali mwaliko wake au wataukataa? Tuna sababu nzuri sana zinazotuchochea tuepuke uasherati. “Mwanamke mpumbavu” anafafanuliwa kuwa anasema hivi: “Maji yaliyoibwa ni matamu.” (Met. 9:17) “Maji yaliyoibwa” ni nini? Biblia inalinganisha uhusiano wa kingono ambao watu waliofunga ndoa hufurahia na maji yenye kuburudisha. (Met. 5:15-18) Mume na mke waliofunga ndoa kisheria wanaweza kufurahia kufanya ngono. Hata hivyo, mambo ni tofauti kuhusu “maji yaliyoibwa.” Maji hayo yanarejelea uasherati. Watu hufanya uasherati kisiri kama mwizi anavyoiba kisiri. ‘Maji hayo yaliyoibwa’ huenda yakaonekana kuwa matamu hasa ikiwa wale wanaohusika wanafikiri kwamba hakuna mtu atakayejua jambo hilo. Kwa kweli wanajidanganya! Yehova anaona mambo yote. Ikiwa tutapoteza kibali cha Yehova, tutapatwa na uchungu mwingi sana na kwa kweli hilo si jambo ‘tamu’ au linalofurahisha.—1 Kor. 6:9, 10. w23.06 22 ¶7-9