Jumamosi, Septemba 6
[Iweni] vielelezo kwa kundi.—1 Pet. 5:3.
Upainia unamsaidia mwanamume kijana kujifunza jinsi ya kufanya kazi vizuri pamoja na watu mbalimbali. Pia, unamsaidia kupanga bajeti vizuri na kushikamana nayo. (Flp. 4:11-13) Njia nzuri ya kuanza utumishi wa wakati wote ni kufanya upainia msaidizi, jambo ambalo litakusaidia kuwa tayari kuanza upainia wa kawaida. Upainia unaweza kufungua mlango unaoongoza kwenye aina nyingine za utumishi wa wakati wote, kutia ndani kutumikia ukiwa mjenzi au Mwanabetheli. Wanaume Wakristo wanapaswa kuwa na lengo la kustahili kuwatumikia ndugu na dada zao wakiwa wazee wa kutaniko. Biblia inasema kwamba wanaume wanaojitahidi kufikia jukumu hilo ‘wanatamani kazi njema.’ (1 Tim. 3:1) Kwanza, ni lazima ndugu astahili kutumikia akiwa mtumishi wa huduma. Watumishi wa huduma wanawasaidia wazee kwa njia nyingi hususa. Wazee na watumishi wa huduma wanawatumikia kwa unyenyekevu ndugu na dada zao na kushiriki kwa bidii katika huduma. w23.12 28 ¶14-16
Jumapili, Septemba 7
Alipokuwa angali mvulana, alianza kumtafuta Mungu wa Daudi babu yake.—2 Nya. 34:3.
Mfalme Yosia alikuwa tineja alipoanza kumtafuta Yehova. Alitaka kujifunza kumhusu Yehova na kufanya mapenzi Yake. Hata hivyo, maisha hayakuwa rahisi kwa mfalme huyo kijana. Alihitaji kuchukua msimamo upande wa ibada safi wakati ambapo ibada ya uwongo ilikuwa imeenea. Na kwa kweli, alifanya hivyo! Kabla Yosia hajafikisha umri wa miaka 20, alianza kuondoa ibada ya uwongo katika taifa hilo. (2 Nya. 34:1, 2) Hata ikiwa wewe ni kijana, unaweza kuamua kumwiga Yosia kwa kumtafuta Yehova na kujifunza kuthamini sifa Zake. Ukifanya hivyo, utachochewa kujiweka wakfu kwake. Kujiweka wakfu kutaathirije maisha yako ya kila siku? Luke, ambaye alibatizwa akiwa na umri wa miaka 14, anasema hivi: “Kuanzia sasa na kuendelea, nitatanguliza kumtumikia Yehova maishani mwangu na nitajitahidi kumfurahisha.” (Marko 12:30) Wewe pia utapata baraka ikiwa unatamani kufanya hivyo! w23.09 11 ¶12-13
Jumatatu, Septemba 8
Waheshimuni wale wanaofanya kazi kwa bidii miongoni mwenu na wanaowasimamia katika Bwana.—1 The. 5:12.
Mtume Paulo alipoandika barua hiyo, mwaka mmoja haukuwa umepita tangu kutaniko la Thesalonike lilipoanzishwa. Inaonekana kwamba wanaume waliowekwa rasmi hawakuwa na uzoefu na huenda walifanya makosa. Ingawa hivyo, walistahili kuheshimiwa. Dhiki kuu inapokaribia, huenda tukategemea hata zaidi mwongozo kutoka kwa wazee wa kutaniko kuliko ilivyo sasa. Huenda tukapoteza mawasiliano na makao makuu ya ulimwenguni pote au ofisi ya tawi; basi, ni jambo muhimu kujifunza sasa kuwapenda na kuwaheshimu wazee wa kutaniko. Hata jambo gani litokee, acheni tuendelee kutunza akili zetu, tusikazie fikira udhaifu wao, bali tukazie fikira kwamba Yehova anawaongoza wanaume hao waaminifu kupitia Kristo. Kama vile kofia ya chuma ilivyolinda kichwa cha mwanajeshi, tumaini letu la wokovu hulinda mawazo yetu. Tunatambua kwamba mambo yaliyo katika ulimwengu huu hayana thamani yoyote. (Flp. 3:8) Tumaini letu linatusaidia kuendelea kuwa watulivu na thabiti. w23.06 11-12 ¶11-12