-
Watiwa Nguvu na Mjumbe Kutoka Kwa MunguSikiliza Unabii wa Danieli!
-
-
‘MTU APENDWAYE SANA’ ATIWA NGUVU
14. Danieli alihitaji msaada gani ili kupokea ujumbe kutoka kwa malaika?
14 Malaika wa Yehova alikuwa amemletea Danieli ujumbe mzito na wenye kuhusisha mambo mengi. Kabla ya Danieli kuupokea, alihitaji msaada ili kupata nafuu kutokana na msononeko wake wa kimwili na kiakili. Yaonekana kwamba kwa kuwa malaika alijua hilo, alimsaidia Danieli kwa upendo na kumtia moyo. Acheni tusome simulizi la Danieli mwenyewe juu ya jambo lililotokea.
15. Malaika alifanya nini ili kumsaidia Danieli?
15 “Niliposikia sauti ya maneno yake, ndipo nikashikwa na usingizi mzito, na uso wangu umeielekea nchi.” Huenda hofu na woga ulimfanya Danieli azimie. Malaika huyo alifanya nini ili kumsaidia? “Tazama,” akasema Danieli, “mkono ukanigusa, ukaniweka juu ya magoti yangu, na vitanga vya mikono yangu.” Tena, malaika huyo akamtia moyo nabii huyo kwa kumwambia: “Ee Danieli, mtu upendwaye sana, yafahamu maneno nikuambiayo, ukasimame kiwima-wima; maana kwako nimetumwa sasa.” Mkono wenye kusaidia na maneno yenye kuliwaza yalimwamsha Danieli. Ingawa alikuwa ‘akitetemeka,’ Danieli ‘alisimama.’—Danieli 10:9-11.
16. (a) Twawezaje kusema kwamba Yehova hujibu sala za watumishi wake haraka? (b) Kwa nini malaika alikawia kuja kumsaidia Danieli? (Tia ndani sanduku.) (c) Malaika huyo alikuwa na ujumbe gani wa kumwarifu Danieli?
16 Malaika alitaja waziwazi kwamba kusudi lake la kuja lilikuwa kumtia nguvu Danieli. “Usiogope, Danieli,” akasema malaika huyo, “kwa maana tangu siku ile ya kwanza ulipotia moyo wako ufahamu, na kujinyenyekeza mbele za Mungu wako, maneno yako yalisikiwa; nami nimekuja kwa ajili ya maneno yako.” Kisha malaika akamweleza kwa nini alikuwa amekawia. Alisema hivi: “Lakini mkuu wa ufalme wa Uajemi alinipinga siku ishirini na moja; bali, tazama, huyo Mikaeli, mmoja wa hao wakuu wa mbele, akaja kunisaidia; nami nikamwacha huko pamoja na wafalme wa Uajemi.” Akisaidiwa na Mikaeli, malaika huyo aliweza kutimiza utume wake, wa kumwendea Danieli akiwa na ujumbe huu muhimu: “Sasa nimekuja kukufahamisha mambo yatakayowapata watu wako katika siku za mwisho; maana maono hayo ni ya siku nyingi bado.”—Danieli 10:12-14.
17, 18. Danieli alisaidiwaje mara ya pili, na hilo lilimwezesha kufanya nini?
17 Badala ya Danieli kuchochewa na tazamio la kupokea ujumbe wenye kusisimua kama huo, yaonekana kwamba mambo aliyosikia yalikuwa yamemwathiri sana. Simulizi lataarifu hivi: “Alipokwisha kusema nami maneno hayo, nikauelekeza uso wangu chini, nikawa bubu.” Lakini malaika huyo mjumbe alikuwa tayari kutoa msaada wenye upendo—mara ya pili. Danieli alisema hivi: “Kumbe, mmoja mfano wa wanadamu akanigusa midomo yangu; ndipo nikafumbua kinywa changu, nikanena.”b—Danieli 10:15, 16a.
18 Danieli alitiwa nguvu malaika alipoigusa midomo yake. (Linganisha Isaya 6:7.) Kwa kuwa angeweza kusema tena, Danieli aliweza kumweleza malaika mjumbe magumu aliyokuwa akiyavumilia. Danieli alisema hivi: “Ee Bwana wangu, kwa sababu ya maono haya huzuni zangu zimenipata tena; hata sikusaziwa nguvu. Maana, mtumishi wa Bwana wangu huyu atawezaje kusema na Bwana wangu huyu? kwa maana kwangu mimi, mara hazikusalia nguvu ndani yangu, wala pumzi haikusalia ndani yangu.”—Danieli 10:16b, 17.
19. Danieli alisaidiwaje mara ya tatu, na tokeo likawa nini?
19 Danieli hakuwa akilalamika wala kutoa udhuru. Alikuwa akitaja tu mashaka yake, naye malaika huyo alikubali taarifa yake. Kwa hiyo, Danieli akasaidiwa na malaika mjumbe mara ya tatu. “Mmoja mfano wa mwanadamu akanigusa tena, akanitia nguvu,” akasema nabii huyo. Baada ya kumgusa na kumtia nguvu, mjumbe huyo alisema maneno haya yenye kuliwaza: “Ee mtu upendwaye sana, usiogope; amani na iwe kwako, uwe na nguvu, naam, uwe na nguvu.” Mguso huo wenye upendo na maneno hayo yenye kujenga yaonekana ndiyo mambo tu aliyohitaji Danieli. Ikawaje? Danieli akatangaza hivi: “Aliposema nami nikapata nguvu, nikasema, Ee Bwana wangu, na aseme Bwana wangu; kwa maana umenitia nguvu.” Sasa Danieli alikuwa tayari kwa ajili ya mgawo mwingine mgumu.—Danieli 10:18, 19.
20. Kwa nini malaika mjumbe alihitaji kujitahidi ili atimize mgawo wake?
20 Baada ya kumtia Danieli nguvu na kumsaidia apate nafuu katika uwezo wake wa kiakili na kimwili, malaika huyo alitaja tena kusudi la utume wake. Alisema hivi: “Je! unajua sababu hata nikakujia? na sasa nitarudi ili nipigane na mkuu wa Uajemi; nami nitakapotoka huku, tazama, mkuu wa Uyunani [“Ugiriki,” NW] atakuja. Lakini nitakuambia yaliyoandikwa katika maandiko ya kweli; wala hapana anisaidiaye juu ya hao ila huyo Mikaeli, mkuu wenu.”—Danieli 10:20, 21.
21, 22. (a) Kutokana na mambo yaliyompata Danieli, twaweza kujifunza nini kuhusu njia ya Yehova ya kushughulika na watumishi wake? (b) Danieli alitiwa nguvu kwa ajili ya nini sasa?
21 Yehova ni mwenye upendo na fadhili kama nini! Sikuzote yeye hushughulika na watumishi wake kulingana na uwezo na udhaifu wao mbalimbali. Kwa upande mmoja, yeye huwapa migawo kulingana na ajuayo wanaweza kutimiza, hata ingawa huenda nyakati nyingine wakahisi vinginevyo. Kwa upande mwingine, yuko tayari kuwasikiliza na kuwaandalia kinachohitajiwa ili kutimiza migawo yao. Na tumwige Baba yetu wa kimbingu, Yehova, kwa kuwatia moyo na kuwatia nguvu waabudu wenzetu kwa upendo.—Waebrania 10:24.
22 Ujumbe wa malaika wenye kufariji ulimtia Danieli moyo sana. Ijapokuwa alikuwa mzee, Danieli alikuwa ametiwa nguvu na alikuwa tayari kupokea na kurekodi unabii zaidi wenye kutokeza kwa manufaa yetu.
-
-
Watiwa Nguvu na Mjumbe Kutoka Kwa MunguSikiliza Unabii wa Danieli!
-
-
b Ingawa huenda malaika huyohuyo aliyekuwa akiongea na Danieli akawa aligusa midomo yake na kumwamsha, maneno yanayotumiwa hapa yaweza kumaanisha pia kwamba malaika mwingine, huenda Gabrieli, ndiye aliyemgusa. Hata hivyo, Danieli alitiwa nguvu na malaika mjumbe.
-