Ezekieli
38 Neno la Yehova likakuja tena kwangu, na kusema: 2 “Mwana wa binadamu, elekeza uso wako juu ya Gogu wa inchi ya Magogu,+ mukubwa wa wakubwa wa Mesheki na Tubali,+ na utoe unabii juu yake.+ 3 Useme, ‘Bwana Mwenye Mamlaka Makubwa Zaidi Yehova anasema hivi: “Angalia, nitapigana na wewe, Ee Gogu, mukubwa wa wakubwa wa Mesheki na Tubali. 4 Nitakugeuza na kutia kulabu* katika mataya* yako+ na kukupeleka inje pamoja na jeshi lako lote,+ farasi na wapanda-farasi, wote wakiwa wamevaa utukufu, kutaniko kubwa sana lenye ngao za mukubwa na ngao za kidogo,* wote wakiwa na panga; 5 Uajemi, Etiopia, na Putu+ wako pamoja nao, wote wakiwa na ngao ya kidogo na kofia ya chuma; 6 Gomeri na wanajeshi wake wote, nyumba ya Togarma+ kutoka sehemu za mbali zaidi za kaskazini, pamoja na wanajeshi wake wote—vikundi vingi vya watu viko pamoja na wewe.+
7 “‘“Ukuwe tayari, ujitayarishe, wewe pamoja na majeshi yenye yamekusanyika pamoja na wewe, na utakuwa kamanda* wao.
8 “‘“Utakaziwa uangalifu* kisha siku nyingi. Katika kipindi cha mwisho cha miaka utashambulia inchi yenye watu wake wamerudishwa kutoka kwenye uharibifu wa upanga, wenye walikusanywa pamoja kutoka katika vikundi vingi vya watu, na kuletwa kwenye milima ya Israeli, yenye kwa wakati murefu ilikuwa imeharibiwa. Wakaaji wa inchi hiyo walirudishwa kutoka katika vikundi vya watu, na wote wanakaa kwa usalama.+ 9 Utawashambulia kama zoruba, na utafunika inchi kama mawingu, wewe na wanajeshi wako wote na vikundi vingi vya watu vyenye kuwa pamoja na wewe.”’
10 “Bwana Mwenye Mamlaka Makubwa Zaidi Yehova anasema hivi: ‘Siku hiyo mawazo yataingia katika moyo wako, na utapanga mupango wa uovu. 11 Utasema: “Nitashambulia inchi yenye makao yenye hayana ulinzi.*+ Nitashambulia wale wenye kukaa kwa usalama, bila usumbufu, wote wenye kukaa katika makao yenye hayalindwe na kuta, mapingo,* wala milango mikubwa.” 12 Itakuwa vile ili kukamata vitu vingi vyenye vinachukuliwa katika vita na vitu vingi vyenye vinanyanganywa katika vita, ili kushambulia maeneo yenye yaliharibiwa ambayo sasa yanaikaliwa+ na watu wenye walikusanywa kutoka katika mataifa,+ wenye wanajikusanyia utajiri na mali,+ wale wenye kukaa katikati ya dunia.
13 “‘Sheba+ na Dedani,+ wafanyabiashara wa Tarshishi+ na wapiganaji-vita wake wote* watakuambia: “Je, unashambulia ili ukamate vitu vingi vyenye vinachukuliwa katika vita na vitu vingi vyenye vinanyanganywa katika vita? Je, umekusanya majeshi yako ili kubeba feza na zahabu, kukamata utajiri na mali, ili kuchukua vitu vingi sana katika vita?”’
14 “Kwa hiyo toa unabii, mwana wa binadamu, na umuambie Gogu, ‘Bwana Mwenye Mamlaka Makubwa Zaidi Yehova anasema hivi: “Siku yenye watu wangu Israeli watakuwa wanaishi kwa usalama, je, hautajua jambo hilo?+ 15 Utakuja kutoka mahali pako, kutoka sehemu za mbali zaidi za kaskazini,+ wewe na vikundi vingi vya watu vyenye kuwa pamoja na wewe, wote wakiwa wamepanda farasi, mukusanyiko mukubwa, jeshi kubwa sana.+ 16 Kama mawingu yenye kufunika inchi, utashambulia watu wangu Israeli. Katika kipindi cha mwisho cha zile siku, nitakuleta ushambulie inchi yangu+ ili mataifa yanijue wakati nitajitakasa mwenyewe kupitia wewe mbele ya macho yao, Ee Gogu.”’+
17 “Bwana Mwenye Mamlaka Makubwa Zaidi Yehova anasema hivi: ‘Je, wewe hauko uleule mwenye nilisema kumuhusu katika siku za zamani kupitia watumishi wangu manabii wa Israeli, wenye walitoa unabii kwa miaka mingi kwamba utaletwa ili kuwashambulia?’
18 “‘Siku hiyo, siku yenye Gogu atashambulia inchi ya Israeli,’ ni vile Bwana Mwenye Mamlaka Makubwa Zaidi Yehova anasema, ‘kasirani yangu kali itawaka.+ 19 Katika bidii yangu, katika moto wa kasirani yangu kali, nitasema; na siku hiyo kutakuwa tetemeko kubwa la inchi katika inchi ya Israeli. 20 Kwa sababu yangu, samaki wa bahari, ndege wa anga, wanyama wa pori, wanyama wote wenye kutambaa chini, na wanadamu wote wenye kuwa juu ya uso wa dunia watatetemeka,+ na milima itaangushwa chini, na miteremuko mikali itaanguka, na kila ukuta utaanguka chini.’
21 “‘Nitaita upanga juu yake kwenye milima yangu yote,’ ni vile Bwana Mwenye Mamlaka Makubwa Zaidi Yehova anasema. ‘Upanga wa kila mutu utakuwa juu ya ndugu yake mwenyewe.+ 22 Nitaleta hukumu juu yake* kwa ugonjwa wa kuambukiza+ na umwangaji wa damu; na nitanyesha mvua kubwa yenye kufurika na mvua ya majiwe+ na moto+ na kiberiti+ juu yake na juu ya wanajeshi wake na juu ya vikundi vingi vya watu vyenye kuwa pamoja naye.+ 23 Na hakika nitajitukuza na kujitakasa na kujijulisha mwenyewe mbele ya macho ya mataifa mengi; nao watalazimika kujua kwamba mimi ni Yehova.’