UMUKARIBIE MUNGU
“Sifa Zake Ambazo Hazionekani, Zinaonekana Waziwazi”
Unamuamini Mungu? Ikiwa unajibu ndiyo, je, unaweza kuonyesha mambo fulani yanayohakikisha kwamba kuna Mungu? Ni kweli kwamba tunazungukwa na mambo yanayohakikisha kuwa kuna Muumbaji aliye mwenye hekima, nguvu, na upendo. Ni mambo gani hayo, na ni yenye kusadikisha kwa kadiri gani? Ili kupata jibu, fikiria maneno ya mutume Paulo katika barua yake kwa Wakristo wa Roma.
Paulo alisema hivi: “Sifa zake [Mungu] ambazo hazionekani, zinaonekana waziwazi tangu kuumbwa kwa ulimwengu na kuendelea, kwa sababu zinaeleweka kwa vitu vilivyofanywa, yaani, nguvu zake za milele na Uungu, hivi kwamba hawana sababu ya kujitetea.” (Waroma 1:20) Kama Paulo alivyosema, Muumbaji anatuonyesha kwamba yeye yuko kupitia vitu ambavyo aliumba. Acheni tuchunguze kwa uangalifu sana maneno ya mutume Paulo.
Paulo anasema kwamba sifa za Mungu zinaonekana “tangu kuumbwa kwa ulimwengu na kuendelea.” Katika andiko hilo, neno la Kigiriki lililotafsiriwa “ulimwengu” halimaanishe sayari yetu Dunia, lakini, linamaanisha wanadamu.a Kwa hiyo, Paulo anasema kwamba tangu wakati wanadamu waliumbwa, wangeweza kuona uhakikisho wa sifa za Muumbaji katika vitu alivyoumba.
Tunazungukwa na mambo yanayohakikisha kwamba kuna Mungu. Mambo hayo hayajifiche katika ulimwengu wetu lakini ‘yanaonekana waziwazi.’ Kuanzia kiumbe kikubwa zaidi mupaka kiumbe kilicho kidogo zaidi, uumbaji unaonyesha waziwazi kwamba kuna Muumbaji na kwamba ana sifa za ajabu sana. Vitu vilivyoumbwa ambavyo vinaonekana kila mahali vinatuonyesha kwamba vilifanywa kwa akili na Mungu mwenye hekima. Mbingu zenye kujaa nyota na mawimbi makubwa ya bahari vinatuonyesha nguvu zake. Aina mbalimbali za chakula kinachofurahisha ulimi wetu na uzuri ambao tunaona wakati jua linatokea na wakati linatua, mambo yote hayo yanaonyesha upendo wake kwa wanadamu.—Zaburi 104:24; Isaya 40:26.
Mambo hayo yanayohakikisha kwamba kuna Mungu yako wazi kadiri gani? Yako wazi sana hivi kwamba wale ambao hawayaone na hivyo wanakataa kuamini kwamba kuna Mungu “hawana sababu ya kujitetea.” Mutu mumoja mwenye elimu anaeleza jambo hilo kwa njia hii: Wazia muendeshaji wa motokari anayepuuza alama yenye kusema “Geuka—Uende Upande wa Kushoto.” Polisi anamusimamisha na anaanza kumuandikia kiasi cha feza za kulipia kosa lake. Muendeshaji wa motokari anajaribu kubishana na polisi huyo na kumuambia kwamba hakuona alama hiyo ya barabarani. Lakini polisi huyo hakubali maneno yake kwa sababu alama hiyo inaonekana waziwazi na muendeshaji huyo wa motokari ana macho yenye kuona vizuri. Zaidi ya hiyo, kwa sababu yeye ni muendeshaji wa motokari, anapaswa kuona na kutii alama hizo. Ni hivyo pia juu ya mambo ambayo yanaonekana kila mahali yanayohakikisha kwamba kuna Mungu. Mambo hayo yanaonekana waziwazi. Kwa sababu sisi ni viumbe wenye akili, tuna uwezo wa kuona mambo hayo. Mutu hana sababu ya kujitetea anapokataa kuona mambo hayo.
Muumbaji anatuonyesha kwamba yeye yuko kupitia vitu ambavyo aliumba
Bila shaka, uumbaji unaonyesha mambo mengi juu ya Muumbaji. Lakini pia kuna kitabu kinachoonyesha mambo mengi zaidi juu yake, kitabu hicho ni Biblia. Kupitia kitabu hicho tunaweza kupata jibu la ulizo hili la maana sana: Mungu ana kusudi gani juu ya dunia na juu ya watu wanaokaa duniani? Kujua jibu la ulizo hilo kunaweza kukusaidia umukaribie Mungu ambaye “sifa zake ambazo hazionekani, zinaonekana waziwazi” kupitia mambo yanayotuzunguka.
Tafazali, mwezi huu wa 7, soma maandiko haya katika Biblia:
a Pia, Biblia inasema kwamba “ulimwengu” una hatia ya zambi na kwa sababu hiyo unahitaji mwokozi. Hilo linaonyesha wazi kwamba katika maandiko hayo neno hilo ulimwengu linamaanisha wanadamu wala si dunia.—Yohana 1:29; 4:42; 12:47.