“Acheni mambo yenu yote yatendeke kwa upendo”
1 “Tunashangazwa na jinsi mnavyopanga mambo kwa hali ya juu, na utaratibu wenu. Hilo linastaajabisha na kuleta heshima.” Maneno hayo yalisemwa na mwanamume mmoja mwenye madaraka anayetumika katika ofisi moja ya waziri na ambaye alihudhuria mmoja wa mikusanyiko yetu ya wilaya. Inatia moyo kusikia sifa kama hizo kuhusu jinsi tunavyojiendesha katikati ya watu. Hilo laonyesha kwamba sisi, tukiwa kikundi, ‘tunaacha mambo yetu yote yatendeke kwa upendo.’ (1 Kor. 16:14) Wakati huohuo, kuna mambo fulani yenye kusumbua ambayo, ikiwa hayazungumziwi, yatapunguza sifa ya watu wa Mungu.
2 Tuonyeshe Upendo Wetu kwa Kujitolea: Mafanikio ya mkusanyiko hutegemea sana matayarisho. Kwa hiyo, tunataka mwonyeshe roho yenu ya kujipendea ili kushirikiana na halmashauri mbalimbali za mikusanyiko zinazowekwa rasmi katika eneo lenu. Tunataka kusifu wale wote wanaojitoa kwa kujitakia ili kusimamisha na kubomoa idara mbalimbali za mkusanyiko. Kwa kweli kuna mengi ya kufanya. Mara nyingi, inatuomba kusafisha mahali kikamili. Tunapaswa kupanga mambo ili ndugu fulani wachunge vitu tulivyosimamisha. Wakati wa mkusanyiko, wengine wanapaswa kuangalia ili vyoo vibaki safi.
3 Ripoti tunazopokea kutoka mahali mbalimbali zinaonyesha kwamba ni wachache tu kati ya akina ndugu na dada zetu ndio hujitoa kwa kujipendea kwa ajili ya matayarisho ya mikusanyiko. Wengine kati ya wale wanaojitoa huomba wategemezwe kifedha na kulishwa na Sosaiti. Wengine hutoa utumishi wao mbalimbali au vifaa vyao vya kazi huku wakiomba walipwe kwa utumishi uliotolewa. Hawatambui kwamba makusanyiko yetu matakatifu huwatolea nafasi bora ya kuchangia kwa kujipendea katika mpanuko wa ibada safi ya Yehova.—Zab. 110:3.
4 Katika nyakati za kibiblia, ujenzi wa hekalu na kuta za Yerusalemu zilikuwa nyakati zenye furaha kwa watumishi wa Yehova. Watu wa Mungu waliona hiyo kuwa nafasi ya kuonyesha shukrani yao kwa Yehova. Wanaume na wanawake walileta michango yao kila mtu kulingana na uwezo wake, na walijitoa kimwili katika kazi mbalimbali.—Ezra 2:64, 65, 69; 3:1, 3.
5 Tuna mengi ya kujifunza kutokana na mfano wao. Walikuwa wenye kujitoa na walitumika wote kwa kujipendea. Hali walimoishi hazikuwa zenye kufaa. Katika siku za Ezra, wale walioshiriki katika kazi za ujenzi walikuwa wapya katika mji. Walikuwa wameishi muda mrefu uhamishoni na iliwaomba wakati mwingi ili kustarehe na kujipanga upya kitengenezo. Zaidi ya hilo, walinyanyaswa na maadui wao ambao hawakutaka ibada ya kweli irudishwe Yerusalemu. Hivyo, hawakuwa na maisha rahisi. (Ezra 4:1-5) Ingawa walikuwa wapya katika mji, hawakuvunjika moyo na hawakuomba wategemezwe kifedha ati kwa sababu walishiriki katika ujenzi wa hekalu. Badala yake, walitumika bila ‘kulegea’ na Yehova aliwabariki.—Ezra 4:22.
6 Matayarisho ya mkusanyiko ni wakati wa furaha. (Kum. 16:15) Kila kutaniko, kila familia ya Kikristo, inapaswa kujisikia yenye kuhusika. Kupitia mfano wao na vitia-moyo vyao, wazee wanaweza kuchochea washiriki wa kutaniko lao. Mkusanyiko wa wilaya “Neno la Mungu la Kiunabii” ulipokaribia, wazee wa kutaniko moja katika nchi yetu walikusanya vijana wa kutaniko lao, na waliwaonyesha kaseti-vidio “ Unis grâce à l’enseignement divin ” ambayo inaeleza jinsi mahali pote ulimwenguni vijana na watu wazima hushiriki katika matayarisho ya mikusanyiko. Kwa sababu ya kaseti hiyo, vijana wa kutaniko hilo walijitoa kwa wingi wakiwa wenye kujipendea ili kusafisha kiwanja cha michezo ambako mkusanyiko ulipaswa kufanyika. Hata hali yetu iwe gani, acheni tutumike na kuchangia kwa furaha katika mafanikio ya mikusanyiko yetu ya wilaya inayopangwa mwaka huu.
7 Tushirikiane na Ndugu Wakati wa Mapumziko: Katika kusudi la kurahisisha mambo na kukomboa wakati, Sosaiti iliomba wahudhuriaji walete chakula chao kila siku. Ndugu wengi walifuata pendekezo hilo na waliona kwamba iliwezekana, wakati wa pumziko la saa sita, kukaa pamoja na washiriki wa familia zao ili kula kile walichokuwa wameleta. Wengi husema kwamba wanafaidika hivyo na wakati wa kiburudisho na kupitisha wakati mwingi zaidi pamoja na ndugu na dada zao. Kwa hiyo, inaomba watayarishe kimbele chakula na kinywaji na kukiweka katika mfuko mdogo au katika chombo cha kutia vinjwaji baridi, chombo kinachoweza kuwekwa chini ya kiti. Tunaomba wahudhuriaji wote wafanye hivyo. Hivi karibuni, ilionekana kwamba ndugu fulani waliondoka mahali pa mkusanyiko ili kwenda kununua chakula kando-kando. Tokeo ni kwamba wachuuzi wengi huonwa wakiingia mahali pa mkusanyiko. Wengine kati yao sasa wangetaka waruhusiwe kufungua meza zao za kuuzishia vitu na kupendekeza huduma zao kwa wahudhuriaji wa mkusanyiko. Ikiwa wangepewa ruhusa hiyo, watu wengi kutoka nje wangechanganyika nasi mchana. Tungeona tena mistari mirefu ya watu wenye kungojea mbele ya meza ya kuuzishia vyakula, jambo ambalo lingeharibu hali yenye kuburudisha ya mikusanyiko yetu. Ni kwa sababu hiyo tunaomba kila mtu alete kwenye mkusanyiko chakula chake na kinywaji chake cha kila siku. Watu wenye mwelekeo mzuri wanaokusindikiza wanapaswa kufanya vivyo hivyo. Vyombo vya bilauri vya kuwekea vyakula, na vinywaji vyenye alkoholi haviruhusiwi mahali pa mkusanyiko.
8 Tunatazamia kwa hamu kuhudhuria Mkusanyiko wa Wilaya “Watekelezaji wa Neno la Mungu.” Je, umekwisha kufanya matayarisho yako yote? Je, umepanga kutumikia ukiwa mwenye kujipendea? Mwenendo wetu kwenye hoteli na katika mji wa mkusanyiko na uonyeshe sikuzote kweli iliyo katika mioyo yetu na upendo wetu kwa Muumba wetu.