Je, wewe unathamini uvumilivu wa Yehova?
1 Ikiwa Yehova hangekuwa mvumilivu kwa miaka 10, 20, au zaidi iliyopita, akiruhusu ushahidi wenye kupanuka utolewe, je, ungeweza kupata kujifunza kweli? Sisi ni wenye shukrani kama nini kuona kwamba ameruhusu watu wengine wengi “wafikie toba.” Hata hivyo, siku kubwa ya Yehova ya hukumu “itakuja kama mwizi.” (2 Pet. 3:9, 10) Kwa hiyo, uvumilivu wa Yehova haupaswi kuonwa kimakosa kuwa kuchelewa katika kuleta mwisho wa mfumo huu wa mambo.—Hab. 2:3.
2 Hurumia watu: Uvumilivu wa Yehova unapita kwa mbali uelewevu wetu. Hatupaswi kusahau kusudi lake. (Yona 4:1-4, 11) Yehova anaona hali yenye kuhuzunisha ya wanadamu, naye ni mwenye huruma kwa ajili yao. Yesu anahisi vivyo hivyo. Kwa kuwa alihurumia makutano makubwa ya watu ambayo alihubiria, alitaka kazi ya kueneza evanjeli ipanuke ili watu wengi zaidi wapate nafasi ya kupata uzima wa milele.—Mt. 9:35-38.
3 Wakati mambo ya huzuni na misiba inapotokea, je, mioyo yetu haisikii huruma kuelekea wale wasiojua kweli? Watu leo ni kama “kondoo wasio na mchungaji” kadiri wanavyojaribu kukabiliana na kuelewa hali ya machafuko katika ulimwengu. (Mk. 6:34) Kwa kuhubiri kwa bidii habari njema, tunafariji wale walio na mwelekeo mzuri wa moyo na tunaonyesha uthamini wetu kwa uvumilivu wa Yehova.—Mdo. 13:48.
4 Kazi yetu ni ya haraka: Mwaka jana watu 323,439 walibatizwa, na zaidi ya 14,000,000 walihudhuria Ukumbusho. Kuna uwezekano kama nini kwa wengine wengi kuokoka uharibifu wa mfumo huu mbovu! Hatujui “umati mkubwa” utakuwa mkubwa kadiri gani. (Ufu. 7:9) Hatujui utume wetu wa kuhubiri utaendelea kwa wakati gani. Lakini Yehova anajua. Habari njema itahubiriwa mpaka atakapotosheka, “na ndipo mwisho utakapokuja.”—Mt. 24:14.
5 Wakati unaobaki umepunguzwa, nayo siku ya Mungu inakaribia. (1 Kor. 7:29a; Ebr. 10:37) Hakuna shaka kwamba “wokovu wetu uko karibu zaidi kuliko tulipopata kuwa waamini.” (Rom. 13:11) Acheni tusikose kusudi la uvumilivu wa Mungu. Badala yake, acheni tuhubiri kwa haraka ili wengi walio na tamaa ya uadilifu wapate rehema kubwa ya Yehova.