Kisanduku Cha Maulizo
◼ Jinsi gani tunavyopaswa kushughulikia kazi mbalimbali za kutaniko tunazopewa?
Kutaniko la watu wa Yehova linafanya kazi kwa utaratibu. Jambo hilo linawezekana kupitia jitihada yenye umoja. (1 Kor. 14:33, 40) Fikiria mambo yote yanayoshughulikiwa kuhusiana tu na mkutano mmoja wa kutaniko. Zaidi ya programu yenyewe, kuna shughuli nyingi kabla na baada ya mkutano kwa kuwa ndugu na dada wanafanya kazi mbalimbali. Kazi nyingine ambazo zinafanywa bila kuonekana waziwazi na wengine ni za lazima pia. Namna gani kila mmoja wetu anaweza kutegemeza mpango huo?
Jitoe. Wale walio na roho ya kujitoa kwa hiari au kwa kujipendea watapata mambo mengi ya kufanya. (Zab. 110:3) Onyesha hangaiko lako kwa wagonjwa na walio wazeewazee. Saidia katika kusafisha Jumba la Ufalme. Tunaweza kufanya kazi nyingi zenye faida bila kungojea aliko fulani la pekee. Tunahitaji tu kuwa na nia ya kusaidia.
Tumikia kwa kiasi. Watu wenye kiasi ni wenye furaha wanapotumikia wengine. (Luka 9:48) Kuwa na kiasi kutatuzuia kukubali madaraka mengi kuliko yale tunayoweza kushughulikia kwa namna yenye kufaa. Zaidi, kuwa na kiasi kutatulinda tusivuke mipaka ya mamlaka yetu.—Met. 11:2.
Uwe mwenye kutegemeka. Musa alitiwa moyo kuchagua “wanaume wenye kutegemeka” ili wachukue vyeo vyenye madaraka katika Israeli ya kale. (Kut. 18:21) Sifa hiyo inahitajiwa leo. Shughulikia kwa makini kila mgawo unaotolewa. (Luka 16:10) Ikiwa hautakuwa na nafasi ya kushughulikia mgawo fulani, hakikisha kwamba mipango inayofaa imechukuliwa ili mtu mwingine aushughulikie wakati wewe haupo.
Toa yaliyo bora zaidi. Wakristo wanahimizwa kufanya kazi kwa nafsi yote hata katika mambo ya kimwili. (Kol. 3:22-24) Kuna sababu kubwa zaidi ya kufanya hivyo tunapofanya kazi ili kuendeleza ibada ya kweli. Hata ikiwa kazi fulani inaonekana kuwa yenye umaana mdogo, ni baraka kwa kutaniko wakati ambapo inafanywa vizuri.
Kila kazi tunayotolewa inatupatia nafasi ya kuonyesha upendo wetu kwa Yehova na kwa ndugu zetu. (Mt. 22:37-39) Na tushughulikie kwa uaminifu kazi yoyote ile tunayopewa.