Wanaonyesha Imani Yenye Nguvu!
1 Mitume wa Yesu walimsikiliza kwa uangalifu alipozungumza kuhusu kuwako kwake na siku za mwisho za ulimwengu huu. Matukio yenye kuvuruga, kama vile vita, upungufu wa chakula, matetemeko ya dunia, na magonjwa, yangewapata wanadamu. Kisha, Yesu alisema kwamba watu wangechukia wafuasi wake, na kuwatesa, na hata kuwaua. Manabii wa uongo wangetokea na kudanganya wengi. Upendo wa watu wengi ungepoa.
2 Kwa kufikiria matukio hayo, mitume walipaswa kushangaa Yesu aliposema kisha hapo kwamba habari njema ya Ufalme ingehubiriwa katika dunia yote inayokaliwa. (Mt. 24:3-14) Leo tunaona jinsi unabii huo wenye kuvutia unatimia kwa namna yenye kutokeza. Ijapokuwa tunaishi nyakati za hatari, Mashahidi wa Yehova wanatangaza kwa bidii habari njema. Upendo wa watu wa ulimwengu unapopoa, upendo wetu unazidi kuongezeka. Hata ikiwa tunachukiwa na “mataifa yote,” tunahubiri karibu katika inchi zote.
3 Ni jambo lenye kutia moyo kabisa kuchunguza utendaji wa Mashahidi wa Yehova wa mwaka wa utumishi uliopita kama inavyoonyeshwa katika kisanduku kwenye ukurasa wa 3 mpaka wa 6. Miaka 16 iliyopita, wahubiri wamepitisha zaidi ya saa bilioni moja kila mwaka katika kazi ya kuhubiri na kufanya wanafunzi. Hilo linaonyesha kwamba Mashahidi wa Yehova wana imani yenye nguvu kabisa. Kulikuwa ongezeko la asilimia 5.8 (5.8%) la mapainia, ongezeko la 3.1% la wahubiri, na ongezeko la 4.4% la mafunzo ya Biblia. Kuhusu hesabu ya waliobatizwa, kulikuwa ongezeko la 20.1% la zaidi kwa kulinganisha na mwaka wa utumishi uliopita. Ni jambo lenye kufurahisha kuona kwamba karibu watu milioni saba wanamtumikia Yehova kwa uaminifu leo; ni watu wengi sana kwa kulinganisha na wakati mwingine wowote katika historia ya mwanadamu. Unapochunguza kisanduku, ni jambo gani linalokutia moyo zaidi?
4 Ijapokuwa hesabu hizo ni kubwa, tukumbuke kwamba ni alama ya watu walioonyesha imani yao. Tufikirie mfano mmoja. Guillermo alikomalia katika inchi ya Bolivia. Alizaliwa mwaka wa 1935; alipokuwa na miaka 9, akaanza kutumika katika shamba kubwa la mimea ya coca. Tangu utoto wake alikuwa na zoezi la kutafuna majani ya coca ili kutuliza taabu ya kufanya kazi ngumu. Baadaye alianza kulewa pombe na kuvuta tumbako. Alipoanza kujifunza yale ambayo Mungu anataka afanye, Guillermo aliacha kuvuta tumbako na kisha akaacha kulewa pombe. Tatizo kubwa lilikuwa kuachana na zoezi la tangu utoto la kutafuna majani ya coca. Alisali bila kuchoka na akaachana na zoezi hilo. Alipoachana na mambo yote hayo, akabatizwa. Anasema hivi: “Sasa, mimi ni safi na mwenye furaha nyingi.”
5 Yehova anapendezwa kwelikweli na watu. Anapenda wote watubu. (2 Pet. 3:9) Hiyo ni nia yetu pia. Basi, mioyo yetu ituchochee kufanya yote tuwezayo ili kuendelea kusaidia watu wenye kufuatia haki kumjua na kumpenda Yehova kama sisi.
[Maulizo ya funzo]
1. Ni matukio gani yenye kuvuruga ambayo Yesu alitabiri?
2. Kwa nini ni jambo lenye kushangaza kwamba habari njema inatangazwa ulimwenguni pote?
3. Ni hesabu gani zenye kutia moyo ambazo unaona kwenye ripoti ya ulimwenguni pote?
4. Ni matatizo gani mtu mmoja alishindana nayo alipokuwa akijikaza ili abatizwe?
5. Nia yako ni nini?