Je, Unaweza Kuhubiri Siku za Yenga?
1. Tunaweza kujifunza nini kutokana na jinsi Paulo na wenzake walivyotenda walipokuwa katika muji wa Filipi?
1 Siku ya Sabato ndiyo siku ambayo Wayahudi wengi katika muji wa Filipi walikuwa wanapumzika. Paulo na wenzake walitembelea muji huo katika safari moja kati ya safari zao za umisionari. Wangestahili pia kupumzika siku hiyo na kusimamisha kazi ya kuhubiri; na hakuna mutu ambaye angeweza kuwalaumu. Hata hivyo, walijua kwamba siku hiyo Wayahudi walikusanyika inje ya muji ili kusali, kwa hiyo walitumia nafasi hiyo ili kuwahubiria. Paulo na wenzake walifurahi sana Lidia alipowasikiliza na watu wote wa nyumbani mwake walipobatizwa! (Mdo. 16:13-15) Leo, kwa kuwa watu wengi wanapumzika Siku ya Yenga, kwa nini usitumie saa fulani siku hiyo ili kuwahubiria?
2. Ni matatizo gani ambayo watu wa Yehova wameshinda ili waweze kuhubiri Siku za Yenga bila kusumbuliwa?
2 Mapambano ili Kuhubiri Siku za Yenga: Katika mwaka wa 1927, watu wa Yehova walitiwa moyo wapitishe saa fulani katika mahubiri kila Siku ya Yenga. Kufanya hivyo kuliwaletea mara moja upinzani. Wengi walifungwa katika Marekani kwa kushtakiwa kwamba wanavunja sheria za Sabato ya Siku ya Yenga, kwamba wanavuruga amani ya watu, na kwamba wanauzisha vitabu bila vikaratasi vya serikali. Lakini watu wa Yehova hawakuacha kuhubiri. Katika miaka ya 1930, walipanga “kampanye za vikundi,” katika kampanye hizo wahubiri wa makutaniko yaliyo kandokando walijiunga pamoja ili kuhubiri katika eneo fulani. Wahubiri fulani walipofungwa, wengine wengi walifika mara moja hivi kwamba wenye mamlaka walishindwa kuwazuia. Je, unapendezwa kabisa na jinsi ndugu hao walivyojitoa hivi kwamba tunaweza sasa kuhubiri Siku za Yenga bila kusumbuliwa?
3. Ni nini kinachofanya Siku ya Yenga iwe siku nzuri kwa ajili ya mahubiri?
3 Siku Nzuri Zaidi kwa Ajili ya Mahubiri: Watu wengi hawaendi kazini Siku ya Yenga, kwa hiyo wanapatikana nyumbani. Kwa kawaida ni wenye kutulia zaidi. Watu fulani wanaoenda kanisani wanaweza kupenda kuzungumzia mambo ya Mungu siku hiyo. Ikiwa tunafanya mikutano Siku ya Yenga, tayari tutakuwa wenye kuvaa namna inayofaa kwa ajili ya mahubiri, basi kwa nini tusipange kuhubiri mbele ao kisha mikutano? Ikiwa inahitajiwa, tunaweza kubeba chakula chepesi.
4. Ni furaha gani tunayoweza kupata ikiwa tunahubiri saa fulani Siku ya Yenga?
4 Ikiwa tunatumia saa fulani Siku ya Yenga ili kuhubiri, bado tutabaki na wakati wa kutosha ili kupumzika. Na tutapumzika tukiwa wenye kutosheka ao kurizika kwa kuwa tulishiriki katika utumishi mtakatifu. (Met. 19:23) Tunaweza hata kuwa na furaha ya kumpata mutu fulani aliye kama Lidia!