Somo 13
Namna Gani Unaweza Kuipata Ile Dini ya Kweli?
Je! dini zote zinamupendeza Mungu, au ni moja tu? (1)
Kwa nini kuna dini nyingi sana zinazojidai kuwa za Kikristo? (2)
Namna gani unaweza kuwatambua Wakristo wa kweli? (3-7)
1. Yesu alianzisha dini moja tu ya kweli ya Kikristo. Basi leo kunapaswa kuwa kikundi kimoja tu cha watu walio waabudu wa kweli wa Yehova. (Yoane 4:23, 24; Waefeso 4:4, 5) Biblia inafundisha kwamba ni watu wachache tu walio kwenye barabara nyembamba inayopeleka kwenye uhai.—Matayo 7:13, 14.
2. Biblia ilitangulia kueleza kimbele kwamba kisha kifo cha wale mitume, mafundisho yenye makosa na mazoea yasiyokuwa ya Kikristo yangekuja kuingia polepole katika kutaniko la Kikristo. Watu wangeweza kuvuta waamini ili kuwafuata wao badala ya kumufuata Kristo. (Matayo 7:15, 21-23; Matendo 20:29, 30) Hiyo ndiyo sababu tunaona dini nyingi tofauti zinazojidai kuwa za Kikristo. Namna gani sisi tunaweza kuwatambua Wakristo wa kweli?
3. Alama yenye kuonekana sana ya Wakristo wa kweli ni kwamba wao wanao upendo kati yao ulio wa kweli. (Yoane 13:34, 35) Hawafundishwi kufikiri kwamba wao ndio wazuri kuliko watu wenye rangi ya ngozi nyingine. Wala hawafundishwi kuchukia watu wanaotoka inchi zingine. (Matendo 10:34, 35) Kwa hiyo hawashiriki au kuingia katika vita mbalimbali. Wakristo wa kweli wanatendeana kama ndugu na dada.—1 Yoane 4:20, 21.
4. Alama nyingine ya dini ya kweli ni kwamba washiriki wayo wanaiheshimu sana Biblia. Wanaikubali kuwa Neno la Mungu na wanaamini kile inasema. (Yoane 17:17; 2 Timoteo 3:16, 17) Wanalichukua Neno la Mungu kuwa la lazima sana kuliko mawazo au desturi za binadamu. (Matayo 15:1-3, 7-9) Katika maisha yao ya kila siku wanajaribu kuishi kulingana na Biblia. Kwa hiyo hawahubiri jambo fulani na kuzoea lililo tofauti.—Tito 1:15, 16.
5. Dini ya kweli inapaswa pia kuliheshimu jina la Mungu. (Matayo 6:9) Yesu alifanya jina la Mungu, Yehova, lijulikane kwa wengine. Wakristo wa kweli wanapaswa kufanya hivyo hivyo. (Yoane 17:6, 26; Waroma 10:13, 14) Mahali unapoishi watu gani wanaelezea wengine juu ya jina la Mungu?
6. Wakristo wa kweli wanapaswa kuhubiri juu ya Ufalme wa Mungu. Yesu alifanya hivyo. Siku zote yeye alisema juu ya Ufalme. (Luka 8:1) Aliamuru wanafunzi wake kuhubiri ujumbe huuhuu duniani kote. (Matayo 24:14; 28:19, 20) Wakristo wa kweli wanaamini kwamba ni Ufalme wa Mungu peke yake utakaoleta amani ya kweli na usalama kwenye dunia hii.—Zaburi 146:3-5.
7. Wanafunzi wa Yesu si sehemu ya ulimwengu huu mwovu. (Yoane 17:16) Hawajiingizi katika ulimwengu wa mambo ya kisiasa na mabishano ya watu. Wanaepuka mwenendo, mazoea, na nia zinazoumiza ambazo zinafuatiliwa na watu wengi katika ulimwengu. (Yakobo 1:27; 4:4) Je! unaweza kutambua kikundi cha kidini mahali unapoishi kilicho na alama hizo za Ukristo wa kweli?
[Picha katika ukurasa wa 27]
Wakristo wa kweli wanapendana, wanaiheshimu Biblia, na wanahubiri juu ya Ufalme wa Mungu