SURA YA 9
‘Kimbia Uasherati’
‘Kwa hiyo, viueni viungo vya mwili wenu vilivyo duniani kwa habari ya uasherati, uchafu, hamu ya ngono, tamaa yenye mazara [ao kuumiza], na kutamani, ambako ni ibada ya sanamu.’—WAKOLOSAI 3:5.
1, 2. Balaamu alifanya nini ili kuwanasa watu wa Yehova?
MUVUVI anaenda mahali ambapo anazoea kuvua samaki. Anafikiria aina ya samaki atavua, kwa hiyo anachagua chambo (ao chakula) ambacho samaki hao wanapenda; anatia chambo hicho kwenye ndoano, na kisha anatupa ndoano yake katika maji. Kisha muda mufupi, kamba ya ndoano inakokoteka na mupini wake unakunjama na muvuvi huyo anaanza kukokota samaki. Anafurahi kwa sababu alichagua chambo kinachofaa kabisa.
2 Mwaka wa 1473 mbele ya kuzaliwa kwa Yesu, mwanaume mumoja aliyeitwa Balaamu alifikiria sana mutego wa kuwanasa watu wa Mungu, ambao walikuwa wamepiga kambi katika inchi tambarare ya Moabu, kwenye mupaka na Inchi ya Ahadi. Balaamu alijidai kuwa nabii wa Yehova, lakini kwa kweli yeye alikuwa tu mutu mwenye pupa, na kwa hiyo, alihongwa ili kulaani Waisraeli. Lakini Yehova alibadilisha laana ya Balaamu kuwa baraka. Kwa sababu Balaamu alikuwa tu na tamaa ya malipo kama alivyoahidiwa, alifikiria njia ya kuwashawishi Waisraeli ili wafanye zambi nzito, na hivyo, Mungu wao aweze kuwalaani yeye mwenyewe. Kwa hiyo, Balaamu alifikiria chambo fulani: wanawake Wamoabu wenye kuvutia.—Hesabu 22:1-7; 31:15, 16; Ufunuo 2:14.
3. Je, mutego wa Balaamu ulifanikiwa?
3 Je, mutego wa Balaamu ulifanikiwa? Tunaweza kusema hivyo. Maelfu ya wanaume wa Israeli walianguka katika mutego kwa kufanya “uasherati na binti za Moabu.” Walianza hata kuabudu miungu ya Wamoabu, kama vile mungu Baali wa Peori mwenye kuchukiza, mungu wa uwezo wa kuzaa, ao ngono. Kwa sababu hiyo, Waisraeli 24 000 walikufa ijapokuwa walikuwa karibu kuingia katika Inchi ya Ahadi. Ilikuwa ni huzuni kubwa kabisa!—Hesabu 25:1-9.
4. Sababu gani maelfu ya Waisraeli walianguka katika mutego wa uasherati?
4 Ni nini iliyoongoza kwenye jambo hilo? Waisraeli wengi walikuwa tayari na moyo mubaya kwa sababu walikuwa wamejiondoa kwa Yehova, Mungu ambaye aliwaokoa kutoka Misri, aliyewalisha katika jangwa, na kuwalinda ili waingie katika Inchi ya Ahadi. (Waebrania 3:12) Kwa hiyo, mutume Paulo alitoa onyo hili: ‘Wala tusifanye uasherati, kama wengine wao walivyofanya uasherati, na kuanguka, 23 000 kati yao katika siku moja.’a—1 Wakorintho 10:8.
5, 6. Sababu gani habari inayozungumuziwa katika kitabu cha Hesabu juu ya Waisraeli ni ya maana sana kwetu leo?
5 Sisi watu wa Mungu, habari hiyo inatufundisha mambo mengi ya maana leo; sisi pia tuko kwenye mulango wa Inchi ya Ahadi iliyo nzuri zaidi. (1 Wakorintho 10:11) Kwa mufano, leo watu wa dunia wamejiingiza kabisa katika mambo ya uasherati kama Wamoabu, na hata kupita. Zaidi ya hilo, kila mwaka maelfu ya Wakristo wanaanguka katika mutego uleule wa uasherati kama Waisraeli. (2 Wakorintho 2:11) Leo katika kutaniko, kuna watu fulani wanaokusanyika na sisi, na hata Wakristo fulani, wanaoiga Zimri aliyeingiza waziwazi mwanamuke Mumidiani ndani ya hema lake katika kambi ya Waisraeli. Watu hao wana uvutano mubaya katika kutaniko la Kikristo.—Hesabu 25:6, 14; Yuda 4.
6 Je, unatambua kama leo hali yako ni kama ile ya Waisraeli waliokuwa katika inchi tambarare ya Moabu? Je, unaiona zawadi yako ambayo iko hapo milele, ni kusema, dunia mupya ambayo umengojea sana? Ikiwa ni hivyo, basi, fanya yako yote ili ubaki katika upendo wa Mungu kwa kufuata amri hii: ‘Kimbia uasherati.’—1 Wakorintho 6:18.
Kuangalia sehemu zingine tambarare za Moabu
UASHERATI NI NINI?
7, 8. “Uasherati,” ni nini, na namna gani wale wanaofanya uasherati wanavuna kile walichopanda?
7 Katika Biblia, neno “uasherati” (por·neiʹa katika Kigiriki) linamaanisha kufanya kitendo cha ndoa ao ngono yoyote inje ya ndoa inayokubaliwa na Biblia. Inatia ndani uzinzi, ukahaba, kitendo cha ndoa kati ya watu wasiooana, kufanya kitendo cha ndoa kupitia njia isiyo ya kawaida (kinywa ao mukundu) na pia kugusa-gusa viungo vya uzazi vya mutu mwengine asiye bwana yako ao bibi yako. Inatia ndani kulalana wanaume kwa wanaume ao wanawake kwa wanawake, mutu na munyama ao mutu kugusa-gusa viungo vya uzazi vya munyama ili kujitosheleza tamaa.b
8 Maandiko yako wazi: Watu wanaofanya uasherati hawawezi kuachiliwa wabaki katika kutaniko la Kikristo na hawatapata uzima wa milele. (1 Wakorintho 6:9; Ufunuo 22:15) Tena, hata leo watu hao wanajiletea maumivu makali kama vile kutoaminika tena na watu, kutojiheshimu, mugawanyiko katika ndoa, wanasumbuliwa na zamiri, wanabeba mimba zisizotakiwa, magonjwa, na hata kifo. (Wagalatia 6:7, 8) Sababu gani mutu ajiingize katika njia itakayomuletea matatizo mengi hivyo? Jambo la kuhuzunisha ni kwamba watu wengi hawawaze juu ya matokeo mabaya ya matendo yao wanapochukua hatua ya kwanza isiyofaa: hatua hiyo mara nyingi ni ponografia.
PONOGRAFIA NI HATUA YA KWANZA INAYOONGOZA KWENYE UASHERATI
9. Je, ni kweli kwamba ponografia haina hatari yoyote, kama watu wengine wanavyosema? Fasiria.
9 Katika inchi nyingi picha za mambo ya uasherati ao ponografia zinaonyeshwa wazi katika magazeti, kwenye televizyo, zinajaa kwenye internete, na maneno ya mambo ya uasherati yanajaa katika muziki.c Watu wengine wanasema kwamba ponografia haina hatari yoyote, je, ni kweli? Jibu ni hapana! Mara nyingi wale wanaotazama ponografia wanakuwa na mazoea ya kupiga punyeto (ao kugusa-gusa viungo vya uzazi ili kujitosheleza tamaa ya ngono) na wanakomalisha ‘hamu ya ngono yenye kufezehesha,’ mambo hayo yanaweza kumufanya mutu awe na pupa ya ngono, tamaa zenye kupotoka, matatizo makubwa katika ndoa na hata ndoa kuvunjika.d (Waroma 1:24-27; Waefeso 4:19) Muchunguzi mumoja alilinganisha mutumwa wa ngono na ugonjwa wa kansere. Alisema hivi: “Tamaa hiyo inakomaa na kuenea kila mahali. Mara nyingi haipunguke, na pia ni vigumu kuiponya ao kuitunza.”
Kutumikisha Internete kwa mipaka mahali kwenye watu wanaona katika nyumba ni jambo la hekima
10. Namna gani kanuni inayopatikana katika andiko la Yakobo 1:14, 15, inaweza kutusaidia? (Soma pia kisanduku “Namna Nilivyopata Nguvu za Kusafisha Maisha Yangu.”)
10 Fikiria sasa maneno yaliyo katika andiko la Yakobo 1:14, 15: ‘Kila mutu anajaribiwa kwa kuvutwa na kushawishiwa na tamaa yake mwenyewe. Kisha tamaa, wakati imetunga mimba, inazaa zambi; nayo zambi, wakati imetimizwa, inaleta kifo.’ Kwa hiyo, tamaa mbaya ikiingia katika akili yako, fanya nguvu ya kuiondoa mara moja! Kwa mufano, ikiwa unaona bila kukusudia picha za mambo ya uasherati, angalia pembeni kwa haraka, ao funga mara moja ordinatere yako, ao badilisha kipindi hicho unachofuata kwenye televizyo. Fanya yote ili ukimbize tamaa mbaya ya uasherati kabla haijatia mizizi katika moyo wako na kukutawala!—Mathayo 5:29, 30.
11. Namna gani tunaweza kuonyesha kwamba tunamutegemea Yehova tunapopambana na tamaa mbaya?
11 Kwa kuwa Mungu anatujua vizuri kuliko vile sisi wenyewe tunavyojijua, anajua sababu gani anatushauri hivi: ‘Viueni viungo vya mwili wenu vilivyo duniani kwa habari ya uasherati, uchafu, hamu ya ngono, tamaa yenye mazara [kuumiza], na kutamani, ambako ni ibada ya sanamu.’ (Wakolosai 3:5) Ni kweli kwamba labda inaweza kuwa vigumu kufanya hivyo. Lakini, usisahau kwamba Baba yetu wa mbinguni ni mwenye upendo na ni muvumilivu; tunaweza kumuomba musaada. (Zaburi 68:19) Basi, wakati unaanza kuingiliwa na mawazo mabaya, zungumuza naye haraka. Sali ili akupatie “nguvu zinazopita zile za kawaida,” na ulazimishe akili yako kuwaza mambo mengine.—2 Wakorintho 4:7; 1 Wakorintho 9:27; soma kisanduku “Ninaweza Kufanya Nini ili Niachane na Tabia Yangu Mbaya?”.
12. “Moyo” wetu ni nini, na sababu gani tunapaswa kuulinda?
12 Mwanaume mwenye hekima Sulemani aliandika hivi: “Linda moyo wako kuliko vitu vingine vyote vinavyopaswa kulindwa, kwa maana ndiko zinakotoka chemchemi za uzima.” (Methali 4:23) “Moyo” wetu ndio ule mutu wetu wa ndani, vile Yehova anavyotuona kabisa. Zaidi ya hilo, kupata ao kukosa uzima wa milele kutategemea vile Mungu anavyoona “moyo” wetu, wala si vile wengine wanavyotuona. Jambo hilo linapaswa kutufanya tufikiri sana. Ayubu, mwanaume mwaminifu, alifanya agano ao mapatano na macho yake ili asimutazame mwanamuke kwa tamaa mbaya. (Ayubu 31:1) Huo ni mufano muzuri kabisa wa kuiga! Mutunga-zaburi alikuwa pia na maoni kama hayo, basi alisali hivi: “Uyafanye macho yangu yapite ili yasione jambo lisilofaa.”—Zaburi 119:37.
DINA ALIFANYA UAMUZI MUBAYA
13. Dina alikuwa nani, na kwa nini tunaweza kusema kama alichagua marafiki wabaya?
13 Kama tulivyoona katika Sura ya 3, marafiki wetu wanaweza kutusaidia ao kutuharibisha. (Methali 13:20; 1 Wakorintho 15:33) Tuchukue mufano wa Dina, binti ya Yakobo. (Mwanzo 34:1) Ingawa wazazi wake walimufundisha vizuri tangu utoto, Dina alifanya jambo la upumbavu: alifanya urafiki na mabinti Wakanaani. Wamoabu na Wakanaani walikuwa watu wenye kupenda sana mambo ya uasherati. (Mambo ya Walawi 18:6-25) Wanaume wa Kanaani waliona kuwa Dina ni mwanamuke ambaye anaweza kukubali kwa urahisi kulala na mwanaume yeyote anayemupenda, hata Shekemu aliyekuwa “mwenye kuheshimiwa zaidi” katika nyumba ya baba yake alikuwa na mawazo hayo.—Mwanzo 34:18, 19.
14. Kwa kuwa Dina alichagua marafiki wabaya, jambo hilo lilileta magumu gani?
14 Hakika, Dina hakuwa na wazo la kulala na Shekemu alipomuona. Hata hivyo, Shekemu alifanya kile Wakanaani wengi waliona kuwa si vibaya kufanya wakati tamaa ya ngono inapoamuka. Labda Dina alijaribu kujiondoa katika kinywa cha simba, lakini hakuweza, kwa kuwa Biblia inasema, Shekemu ‘alimuchukua’ na ‘kumunajisi.’ Kisha hapo, Shekemu ‘alimupenda’ Dina, lakini hilo halikutengeneza hali, kwa sababu alikuwa amekwisha kumuharibisha. (Mwanzo 34:1-4) Na mwishowe, jambo hilo liliwaletea wengine matatizo, si Dina peke yake. Kwa sababu alichagua marafiki wabaya, jambo hilo lilianzisha mambo ambayo yalitukanisha familia yao nzima na kuiingiza katika taabu.—Mwanzo 34:7, 25-31; Wagalatia 6:7, 8.
15, 16. Namna gani tunaweza kupata hekima ya kweli? (Soma pia kisanduku “Maandiko ya Kufikiria Sana.”)
15 Dina alipata somo, dunia ilimufundisha. Wale wanaomupenda Yehova na kumutii si lazima wafundishwe na dunia. Kwa sababu wanamusikiliza Mungu, wanachagua ‘kutembea na watu wa hekima.’ (Methali 13:20a) Kwa kufanya hivyo, wanafikia kuelewa “njia yote ya yaliyo mema” na kuepuka matatizo na mateso ya bure.—Methali 2:6-9; Zaburi 1:1-3.
16 Kila mutu anayetafuta hekima ya Mungu anaweza kuipata, ikiwa anaendelea kusali na kujifunza kwa ukawaida Neno la Mungu na pia vitabu ambavyo mutumwa mwaminifu anatutolea. (Mathayo 24:45; Yakobo 1:5) Jambo lingine la maana ni unyenyekevu; sifa hiyo inaonekana wakati mutu anapotii mashauri ya Biblia. (2 Wafalme 22:18, 19) Kwa mufano, kila Mukristo anajua kwamba moyo ni mudanganyifu na hatari. (Yeremia 17:9) Lakini ikiwa anatenda jambo fulani bila kutumia hekima, je, atakuwa tayari kujinyenyekeza ili kukubali shauri na musaada anaotolewa?
17. Zungumuzia hali inayoweza kutokea katika familia, na namna gani baba anaweza kumusaidia binti yake.
17 Wazia hali hii. Baba fulani anamukataza binti yake kuenda kwenye matembezi pamoja na kijana fulani Mukristo wao wawili tu. Binti huyo anaweza kumuambia baba yake: “Sababu gani haunitumainie? Hatutafanya jambo lolote mbaya!” Labda binti huyo anamupenda Yehova na hana mawazo mabaya, lakini tunaweza kusema kweli kama “anatembea katika hekima” inayotoka kwa Mungu? Binti huyo ‘anakimbia kabisa uasherati’? Ao anaonyesha ujinga kwa ‘kuutegemea moyo’ wake? (Methali 28:26) Labda wewe pia unaweza kufikiria kanuni zingine zinazoweza kumusaidia baba huyo na binti yake katika jambo hilo.—Soma Methali 22:3; Mathayo 6:13; 26:41.
YOSEFU ALIKIMBIA UASHERATI
18, 19. Yosefu alishawishiwa namna gani, na alifanya nini?
18 Yosefu alikuwa kijana aliyemupenda Yehova na ambaye alikimbia uasherati. Alikuwa mudogo yake na Dina, lakini hawakuwa wa mama mumoja. (Mwanzo 30:20-24) Yosefu alipokuwa mutoto, alijionea matokeo mabaya ya mwenendo wa upumbavu wa dada yake. Bila shaka, kukumbuka mambo hayo na kutamani kubaki katika upendo wa Mungu, kulimusaidia Yosefu kisha miaka mingi alipojikuta huko Misri, wakati bibi ya bwana wake alikuwa anajaribu kumushawishi “siku baada ya siku.” Kwa sababu Yosefu alikuwa mutumwa, hangeweza kuomba aachishwe kazi! Kwa hiyo, kila siku ilimuomba ajiendeshe kwa hekima na ujasiri. Alifanya hivyo kwa kumuambia kila mara bibi ya Potifa kwamba yeye hapendi kufanya jambo hilo mbaya, na kisha alimukimbia.—Mwanzo 39:7-12.
19 Sasa waza kidogo: Ikiwa Yosefu alikuwa anamuwaza-waza mwanamuke huyo ao kuwaza-waza mambo ya ngono, je, angelibaki kweli mwaminifu? Jibu ni hapana. Maneno aliyomuambia bibi ya Potifa yanaonyesha wazi kwamba Yosefu hakuwa anawaza-waza mambo machafu; urafiki wake pamoja na Yehova ndilo lilikuwa jambo la maana sana kwake. Yeye alimuambia mwanamuke huyo hivi: ‘Bwana wangu hakunizuilia chochote ila wewe, kwa sababu wewe ni bibi yake. Basi ninaweza namna gani kufanya ubaya huu mukubwa na kwa kweli nimutendee Mungu zambi?’—Mwanzo 39:8, 9.
20. Namna gani Yehova alimusaidia Yosefu?
20 Wazia furaha ambayo Yehova alisikia alipoona namna kijana Yosefu alivyoendelea kubaki mwaminifu kila siku hata ikiwa alikuwa mbali na familia yao. (Methali 27:11) Kisha, Yehova alimusaidia Yosefu: Yosefu alifunguliwa na akawa waziri mukubwa wa Misri na pia musimamizi wa mambo ya chakula! (Mwanzo 41:39-49) Jambo hilo linaonyesha ukweli wa maneno ya andiko la Zaburi 97:10: ‘Enyi munaomupenda Yehova, muchukie yaliyo mabaya. Yeye anazilinda nafsi za washikamanifu wake; huwakomboa kutoka katika mukono wa waovu!’
21. Namna gani ndugu mumoja kijana katika inchi fulani ya Afrika alionyesha ujasiri?
21 Leo pia, watumishi wengi wa Mungu wanaonyesha kwamba ‘wanachukia yaliyo mabaya, na wanapenda yaliyo mema.’ (Amosi 5:15) Katika inchi fulani ya Afrika, ndugu mumoja kijana anakumbuka namna binti fulani aliyekuwa naye somo moja alimuambia bila hata haya kwamba atalala naye ikiwa atamusaidia wakati wa mashindano ya hesabu. Ndugu huyo anasema hivi: “Sikusita kumuambia mara moja sipendi. Kuendelea kuwa mwaminifu kulifanya niheshimiwe na nijiheshimu, hayo ni mambo yenye samani sana kuliko hata zahabu.” Ni kweli kwamba zambi inaweza kumupatia mutu ‘furaha ya muda,’ lakini mara nyingi raha hiyo ya muda mufupi inamuletea mutu mateso mengi. (Waebrania 11:25) Zaidi ya hilo, raha hiyo si kitu inapolinganishwa na furaha ya kudumu ambayo mutu anapata kwa kumutii Yehova.—Methali 10:22.
KUBALI MUSAADA WA MUNGU MWENYE REHEMA
22, 23. (a) Mukristo akianguka katika zambi nzito, kwa nini hilo halimaanishe kwamba hawezi kusimama tena? (b) Mutenda-zambi anaweza kupata musaada gani?
22 Sisi ni watu wasio wakamilifu, kwa hiyo, sisi wote tunajikaza kabisa ili kuzuia tamaa za mwili na kufanya yaliyo mema machoni pa Mungu. (Waroma 7:21-25) Yehova anajua hilo vizuri, ‘anakumbuka kwamba sisi ni mavumbi.’ (Zaburi 103:14) Hata hivyo, wakati fulani Mukristo pia anaweza kuanguka katika zambi nzito. Je, hilo linamaanisha kwamba hawezi kusimama tena? Anaweza! Ni kweli kwamba Mukristo huyo anaweza kuvuna matunda mabaya ya zambi zake, kama ilivyomufikia Mufalme Daudi. Lakini, sikuzote Mungu ‘iko tayari kuwasamehe’ wale wanaosikitika kabisa na ‘kuungama waziwazi’ zambi zao.—Zaburi 86:5; Yakobo 5:16; Methali 28:13.
23 Pia, kwa upendo Mungu amelipatia kutaniko la Kikristo “zawadi katika wanaume”, ni kusema, wachungaji wa kiroho wenye kukomaa, wanaostahili, na walio tayari kusaidia. (Waefeso 4:8, 12; Yakobo 5:14, 15) Kusudi lao ni kumusaidia mutenda-zambi ili arudilie urafiki wake pamoja na Mungu na, ‘kumupatia utambuzi wa moyo,’ kama Sulemani alivyosema, ili asirudilie tena zambi.—Methali 15:32.
‘JIPATIE MOYO’
24, 25. (a) Namna gani kijana anayezungumuziwa katika andiko la Methali 7:6-23 alionyesha kama alikuwa mutu ‘asiye na moyo’? (b) Namna gani tunaweza ‘kujipatia moyo’?
24 Biblia inasema kwamba kuna watu ‘wasio na moyo’ na kuna wale ‘wanaojipatia moyo.’ (Methali 7:7) Kukosa ukomavu wa kiroho na kukosa uzoefu katika kazi ya Mungu, kunaweza kumufanya mutu ‘asiye na moyo’ akose utambuzi na akili nzuri. Mutu huyo anaweza kuanguka katika zambi nzito kwa urahisi, kama yule kijana anayezungumuziwa katika Methali 7:6-23. Lakini, mutu ‘anayejipatia moyo’ anajifunza sana Neno la Mungu na kusali kwa ukawaida ili kutengeneza yule mutu wake wa ndani. Na hata ikiwa yeye ni mwanadamu asiye mukamilifu, anajikaza kadiri anavyoweza ili mawazo yake, tamaa zake, mielekeo yake, na miradi yake maishani, vipatane na mapenzi ya Mungu. Kwa kufanya hivyo, anaonyesha kama ‘anaipenda nafsi yake mwenyewe’ ao anajibariki, na “atapata mema.”—Methali 19:8.
25 Kwa hiyo ujiulize: ‘Je, ninaamini kabisa kwamba sheria za Mungu zinafaa? Je, ninaamini kabisa kwamba kuzitii kunaleta furaha nyingi?’ (Zaburi 19:7-10; Isaya 48:17, 18) Ikiwa bado una shaka fulani, uiondoe. Wazia juu ya matokeo mabaya ya kupuuza sheria za Mungu. Pia, ‘onja na uone ya kuwa Yehova ni mwema;’ ni kusema, ishi kulingana na kweli na jaza akili yako na mawazo yanayofaa: mambo yaliyo ya kweli, ya uadilifu (ao haki) yaliyo safi, yaliyo ya kupendeka, na yaliyo mema. (Zaburi 34:8; Wafilipi 4:8, 9) Jua kwamba, sikuzote ukifanya hivyo, upendo wako kwa Yehova utaongezeka, utapenda sana mambo anayopenda, na utachukia mambo anayochukia. Yosefu hakuwa malaika. Lakini, ‘alikimbia uasherati’ kwa sababu alimuacha Yehova amufinyange kwa muda wa miaka mingi, na kumusaidia atamani kumupendeza. Acha iwe hivyo pia kwako.—Isaya 64:8.
26. Ni jambo gani la lazima litakalozungumuziwa katika sura mbili zinazofuata?
26 Muumbaji wetu hakuumba viungo vya uzazi ili vichezewe ovyo-ovyo, lakini ili vipitishe uzima na kufanya bibi na bwana katika ndoa wafurahiane. (Methali 5:18) Mawazo ya Mungu juu ya ndoa yatazungumuziwa katika sura mbili zinazofuata.
a Hesabu inayotajwa katika kitabu cha Hesabu inatia ndani “vichwa [wakubwa] vya watu,” ambao inaonekana walikuwa wanaume 1000 waliouawa na waamuzi, na wale waliouawa na Yehova yeye mwenyewe.—Hesabu 25:4, 5.
b Maana ya uchafu na mwenendo mupotovu inazungumuziwa katika habari “Maulizo ya Wasomaji Wetu” katika Munara wa Mulinzi wa tarehe 15 Mwezi wa 7, 2006, uliochapishwa na Mashahidi wa Yehova.
c “Ponografia” inaweza kuwa picha, maneno ao maandishi yanayotumiwa ili kuamusha tamaa ya ngono. Inaweza kuwa picha ya mutu anayesimama ao kulala kwa namna ya kuamusha tamaa mbaya ao inaweza kuwa picha ya watu wawili ao wengi wanaofanya ngono ya uchafu kabisa na yenye kuchukiza.
d Kupiga punyeto kunazungumuziwa katika Nyongeza “Namna ya Kushinda Tabia.”