NYONGEZA
Mambo Ambayo Biblia Inafundisha Kuhusu Kuvunja Ndoa na Kutengana
Yehova anataka bibi na bwana waliooana waendelee kutimiza kiapo cha ndoa yao, ni kusema, kuendelea kuwa waaminifu mupaka kifo. Yehova alipounganisha mwanaume na mwanamuke wa kwanza, alisema hivi: ‘Mwanaume atashikamana na muke wake, nao wawili watakuwa mwili mumoja.’ Baadaye, Yesu Kristo alirudilia tena maneno hayo na akaongeza: ‘Kwa hiyo, kile ambacho Mungu ameunganisha mutu yeyote asikitenganishe.’ (Mwanzo 2:24; Mathayo 19:3-6) Basi, Yehova na Yesu wanaona ndoa kuwa muungano wa maisha yote, ambao unaweza kuvunjika wakati tu mumoja anakufa. (1 Wakorintho 7:39) Kwa kuwa ndoa ni mupango mutakatifu, kuvunja ndoa si jambo la muchezo. Yehova anachukia talaka (ao kuvunja ndoa) bila sababu zisizo kuwa za Biblia.—Malaki 2:15, 16.
Sasa Biblia inasema ni nini inaweza kuwa sababu ya kuvunja ndoa? Yehova anachukia uzinifu na uasherati. (Mwanzo 39:9; 2 Samweli 11:26, 27; Zaburi 51:4) Kwa kweli, anaona uasherati kuwa jambo lenye kuchukiza sana, na kwa hiyo anakubali sababu hiyo kuwa musingi wa kuvunja ndoa. (Neno uasherati linafasiriwa kirefu katika Sura ya 9, fungu la 7.) Yehova anamupatia yule asiyekuwa na kosa, kati ya bwana na bibi, haki ya kuamua ikiwa ataendelea kuishi na yule aliyefanya uasherati ao kuvunja ndoa. (Mathayo 19:9) Kwa hiyo, ikiwa yule asiyekuwa na kosa anaamua kuvunja ndoa, Yehova hatachukizwa na uamuzi huo. Hata hivyo, kutaniko la Kikristo halitamutia mutu moyo aombe serikali ivunje ndoa yake. Kwa kweli, hali fulani zinaweza kufanya yule asiyekuwa na kosa aendelee kubaki na mwenzi wake wa ndoa aliyefanya uasherati, hasa ikiwa mwenzi huyo aliomba kabisa musamaha. Lakini, yule aliye na sababu ambayo Biblia inakubali ili kuvunja ndoa anapaswa kuchukua uamuzi huo yeye mwenyewe na kukubali matokeo yoyote ambayo uamuzi huo unaweza kuleta.—Wagalatia 6:5.
Katika hali zingine zenye kupita kiasi, Wakristo fulani waliamua kutengana na bwana zao ao bibi zao ao kuvunja ndoa hata ikiwa hakukuwa sababu ya uasherati. Katika hali kama hiyo, Biblia inasema kwamba yule anayeamua kumuacha bibi yake ao bwana yake akae bila kuoa ao kuolewa kama sivyo apatane tena na bibi yake ao bwana yake. (1 Wakorintho 7:11) Mukristo aliye katika hali hiyo hawezi kuoana na mutu mwengine. (Mathayo 5:32) Acha tuone sasa hali za kupita kiasi ambazo wengine waliona kuwa sababu za kutengana na wenzi wao wa ndoa.
Kukataa kimakusudi kuwapatia watu wa familia mahitaji yao. Familia inaweza kuwa masikini sana, na kukosa mambo ya lazima ya maisha, kwa sababu baba, hata ikiwa ana uwezo, anakataa kimakusudi kuwapatia mahitaji yao. Biblia inasema hivi: ‘Ikiwa yeyote hawaandalii [ao hawatimizie] mahitaji washiriki wa nyumba yake, ameikana imani naye ni mubaya kuliko mutu asiye na imani.’ (1 Timotheo 5:8) Ikiwa mutu huyo anakataa kubadilisha mwenendo wake, bibi anaweza kuomba serikali watengane, ili aweze kujilinda na kulinda watoto. Kwa kweli, Mukristo yeyote akishitakiwa kwamba anakataa kimakusudi kutimizia familia yake mahitaji yao, wazee wa kutaniko wanapaswa kuchunguza kabisa jambo hilo kwa uzito. Mutu anaweza kutengwa kwa kukataa kutimizia watu wa familia yake mahitaji yao.
Kumutesa bibi ao bwana kimwili kupita kiasi. Mutu anaweza kumutendea mwenzi wake wa ndoa kinyama kiasi cha kufanya afya yake na uzima wake uwe katika hatari. Ikiwa mwenzi anayetenda hivyo ni Mukristo, wazee wa kutaniko wanapaswa kufanya uchunguzi kuhusu jambo hilo. Mutu anaweza kutengwa kwa sababu ya milipuko ya hasira na kuzoea kumupiga mwenzi wake wa ndoa.—Wagalatia 5:19-21.
Ikiwa hali ya kiroho iko katika hatari kabisa. Labda bwana ao bibi anaweza mara kwa mara kumuzuia mwenzake asimuabudu Yehova ao labda anaweza hata kumufanya avunje amri za Mungu kwa kinguvu. Katika hali kama hiyo, yule anayeteswa anaweza kuamua kwamba kutengana kisheria ndio njia ya kuonyesha kwamba ‘anamutii Mungu kuwa mutawala kuliko wanadamu.’—Matendo 5:29.
Katika hali zote ambazo tumezungumuzia hapo juu, hakuna mutu anayepaswa kumutia moyo mutu anayepatikana katika moja ya hali hizo, ili atengane na bwana yake ao bibi yake ao aendelee kuishi naye. Hata ikiwa marafiki wenye kukomaa kiroho ao wazee wanaweza kumutegemeza na kumutolea mashauri, hakuna anayeweza kujua kabisa-kabisa kile kinachotendeka kati ya bibi na bwana. Ni Yehova peke yake anayejua hilo. Kwa kweli, bwana ao bibi anayefanya matatizo yao ya ndoa yaonekane kuwa makubwa kuliko yalivyo, kwa sababu tu anatafuta kutengana na mwenzake, anakosa kumuheshimu Mungu na pia mupango wa ndoa. Yehova anaona mipango hiyo ya udanganyifu, hata ikiwa mutu anajaribu kuificha namna gani. Kwa kweli, “vitu vyote viko uchi navyo vimefunuliwa wazi machoni pake yeye ambaye tunatoa hesabu kwake.” (Waebrania 4:13) Hata hivyo, ikiwa hali mbaya ya kupita kiasi inaendelea, hakuna mutu anayepaswa kumusema-sema vibaya Mukristo anayefikia uamuzi wa kutengana na mwenzi wake wa ndoa ikiwa alijaribu kila njia ili kuepuka jambo hilo. Kwa vyovyote, ‘sisi wote tutasimama mbele ya kiti cha hukumu cha Mungu.’—Waroma 14:10-12.