Mwishowe, Nilipata Uhuru wa Kweli!
Maria Kilin anaeleza maisha yake
Musimamizi wa gereza alituambia kwa kucheka: “Hakuna mutu anayewauliza. Munaweza kubaki pale.” Namna gani sisi, tuliokuwa wafanyakazi wenye bidii na wenye amani wa familia ya Warusi, tulijikuta katika gereza huko Corée du Nord katika mwaka wa 1950, miaka mitano hivi kisha Vita ya Pili ya Ulimwengu?
KARATASI zangu za utambulisho, zinaonyesha kama nilizaliwa katika mwaka wa 1924. Ni wazi kwamba nilizaliwa katika kijiji cha Shmakovka, Mashariki ya Mbali ya Russie, karibu na mupaka wa Chine.
Siku moja, baba yangu na ndugu zangu wakubwa walichukuliwa na wanyanganyi na tangu siku hiyo mama hakuwaona tena. Mama aliachwa na watoto wengi ambao hakuwa na uwezo wa kulisha. Jirani yetu fulani alimuomba mama ruhusa ya kutupeleka kwenye makao ya mayatima ya kanisa la Ortodokse la Warusi na kusema huko kwamba Mama alituacha.
Mama alikubali mupango huo kwa sababu ikiwa angekataa, sisi watoto wake wachanga, tungekufa na njaa. Kwa sasa nina miaka 80 na kitu, na kwa hiyo, ninamushukuru mama kwa sababu alikubali kututuma kwenye makao hayo ya mayatima. Kufanya hivyo kuliokoa maisha yetu. Lakini, uamuzi wake wa kukubali tupelekwe kwenye makao ya mayatima unaendelea kuniumiza moyoni.
Katika mwaka wa 1941, nilihamia Corée na nikiwa huko niliolewa na mwanaume Murusi muzuri sana anayeitwa Ivan. Olya, binti yetu, alizaliwa mwaka wa 1942 huko Séoul, muji mukubwa wa Corée. Kolya, kijana wetu mwanaume alizaliwa pia huko Séoul mwaka wa 1945, na Zhora, mudogo yake alizaliwa mwaka wa 1948. Bwana yangu alisimamia duka la familia yetu, na mimi nilikuwa nashona nguo. Kwa sababu muji wa Séoul ulikaliwa na majeshi ya Japon, watoto wetu walizungumuza luga ya Kijapani walipokuwa wanakomaa, hata ikiwa tulizungumuza Kirusi nyumbani. Mupaka mwaka wa 1950, ilionekana kulikuwa amani katika muji wa Séoul kati ya Wasovieti, Waamerika, na Wakorea. Wote walikuwa wananunua vitu katika duka letu.
Tunakamatwa na Majeshi ya Corée du Nord
Kama mungurumo wa radi, kila kitu kilibadilika katika mwaka wa 1950. Majeshi ya Corée du Nord yalikamata muji wa Séoul. Kwa sababu tulishindwa kukimbia, tulifungwa pamoja na raia wa inchi zingine za kigeni. Kwa miaka mitatu na nusu, tulitembea pamoja na wafungwa wa vita wa Angleterre, Russie, Amérique, na wa France katika maeneo yote ya Corée du Nord. Tulikaa mahali popote palipokuwa nafasi ya kujificha, na hivyo tulijaribu kuepuka mabombe.
Wakati fulani, tuliishi katika nyumba yenye joto na tulipewa chakula cha kutosha. Hata hivyo, kwa kawaida chakula chetu kilikuwa tu mutama na tulilala katika nyumba zilizoachwa na zenye baridi. Wengi katika kikundi chetu walikufa kwa sababu ya kukosa chakula na kwa sababu ya kutohangaikiwa. Nilihuzunika sana watoto wangu walipoteseka. Katika inchi ya Corée du Nord majira ya baridi yanaanza mapema sana. Ninakumbuka wakati fulani nikiwa pembeni ya moto usiku muzima, nikipasha majiwe moto ili kuyatia chini ya mahali ambapo watoto wangu walikuwa wanalala ili wapate joto.
Majira ya joto yalipoanza, wakaaji fulani wa vijiji vya Corée walituonyesha mimea ya porini ambayo watu wanakula, na tulitafuta vitunguu na mboga za majani, mapera, zabibu, na uyoga. Ni wazi kwamba watu wa vijijini hawakutuchukia, lakini walitusikilia huruma kwa sababu ya hali yetu ngumu. Nilijifunza kunasa vyura ili kuongeza chakula chetu kilichokuwa kidogo. Niliumia moyoni niliposikia watoto wangu wakiomba-omba vyura kila mara.
Siku moja katika Mwezi wa 10, tuliamuriwa kutembea kwa miguu mupaka Manp’o. Tuliambiwa kwamba tutapewa magari ya kukokotwa kwa ajili ya wagonjwa na watoto wadogo. Olya na baba yake walikuwa wakitembea kwa miguu pamoja na kikundi cha watu wengine. Kwa siku nyingi, mimi na wadogo wake tulingojea sana magari ya kukokotwa yafike. Mwishowe, magari hayo yalifika.
Wafungwa waliokuwa wagonjwa walirundikwa kama mifuko ya maharagwe ndani ya magari yaliyokokotwa. Iliumiza sana moyoni kuona jambo hilo. Zhora akiwa kwenye mugongo wangu, nilijaribu kumutia Kolya ndani ya gari hilo, lakini alilalamika sana kwa kusema: “Mama, Mama, ninataka kuenda na wewe! Tafazali usiniache!”
Kolya alinifuata nyuma, alikuwa anakimbia akiwa amenishika kwenye nguo na mukono wake mudogo ili tusimuache. Wafungwa wengi walipigwa risasi wakati wa safari hiyo mbaya, ambayo ilidumu kwa siku nyingi. Vikundi vya watu vilifuata, na kukanyaga-kanyaga maiti za watu hao waliouawa na kuachwa. Mwishowe, tulikutana tena na bwana yangu na Olya. Tulilia na kukumbatiana. Usiku huo, nilibaki macho na kupasha majiwe moto. Sasa nilikuwa na amani ya moyoni kwa sababu watoto wangu wote walikuwa hapo na ningetia majiwe ya moto chini ya mahali ambapo wote walikuwa wanalala ili wapate joto.
Katika mwaka wa 1953, karibu na mupaka unaogawanya Corée du Nord na Corée du Sud, maisha yetu yalikuwa mazuri kidogo. Tulipewa nguo safi, viatu, mikate, na vitu vitamu vya kutafuna. Kisha muda mufupi, wafungwa Waingereza walifunguliwa, na baadaye, Wafaransa wakafunguliwa. Lakini sisi hatukutambuliwa kuwa raia wa inchi yoyote. Wafungwa wa mwisho walipoondoka, tulibaki peke yetu. Tulilia kwa sababu ya kuvunjika moyo na hatukuweza kula chakula. Ni wakati huo ndipo mukubwa fulani wa jeshi la Corée alituambia maneno yenye kuumiza, yanayotajwa mwanzoni mwa habari hii.
Maisha Mapya Huko États-Unis
Jambo la kushangaza ni kwamba kisha muda mufupi tulipelekwa huko Corée du Sud katika eneo lisilo na majeshi. Kisha kuulizwa maulizo na mukubwa wa jeshi la États-Unis, tuliruhusiwa kuhamia États-Unis. Tulisafiri kwa mashua mupaka San Francisco, Californie, ambako tulisaidiwa na shirika fulani la kutoa misaada. Kisha, tulihamia Virginie, na watu tuliojuana nao walitusaidia kuanza kushugulikia mahitaji yetu wenyewe. Mwishowe, tulihamia Maryland ili kuanza maisha mapya.
Tulishangazwa na vitu vidogo, kama vile mashini ya kuvuta vumbi. Kwa sababu tulikuwa wageni katika inchi mupya, tulifanya kazi kwa saa nyingi na kwa bidii. Lakini nilihuzunishwa kuona namna wageni ambao walikuwa wamekwisha kuzoea eneo walivyokuwa wakiwaonea wageni wapya. Muda mufupi kisha sisi kufika Maryland, tulikutana na padri Murusi wa kanisa la Ortodokse ambaye alisema hivi: “Muko sasa katika inchi iliyobarikiwa. Ikiwa munapenda kufanya maendeleo, musifanye urafiki na watu wa inchi yenu.” Niliumia moyoni na kushangazwa sana. Nilijiuliza, ‘Je, hatupaswe kusaidiana?’
Katika mwaka wa 1970, mwanaume mumoja anayeitwa Bernie Battleman, ambaye ni Shahidi wa Yehova, alitutembelea ili kuzungumuza na sisi habari fulani ya Biblia. Alikuwa mwenye nguvu, mutu anayesema mambo waziwazi kama sisi tu. Tulizungumuza kwa muda wa saa nyingi. Kwa sababu nilikomalia katika makao ya mayatima ya kanisa la Ortodokse, nilijua akilini mafundisho ya kanisa. Lakini sikuwa hata na wazo la kuwa na Biblia! Bernie alituletea Biblia moja na akatuambia hivi: “Biblia hii ni yenu kwa sababu ninawapenda.” Alitutambulisha kwa Ben, Shahidi wa Yehova aliyetoka Belarus ambaye alizungumuza luga ya Kirusi.
Ben na bibi yake walijibia kwa upole maulizo yangu kwa kutumia Biblia. Hata hivyo, nilikuwa na uhakika kwamba Mashahidi wa Yehova walibadilisha maandiko matakatifu. Nilikasirishwa zaidi kwa sababu vichapo vyao vilisema kwamba zaidi ya Yesu Maria alikuwa na watoto wengine, wakati kanisa halikutufundisha hivyo.
Nilimuita rafiki yangu mumoja Mupolonye na nikamuomba asome katika Biblia yake ya luga ya Kipolonye ili kuona inasema nini katika andiko la Mathayo 13:55, 56. Aliponisomea andiko hilo, nilishituka kujua kwamba kwa kweli Yesu alikuwa na ndugu wadogo! Rafiki yangu huyo alimuita pia rafiki yake anayetumika Washington D.C., katika nyumba kubwa ya vitabu vinavyosomwa na watu, ili achunguze andiko hilo katika tafsiri zote za Biblia zilizopatikana katika nyumba hiyo. Alisema kama tafsiri zote za Biblia zilisema jambo lilelile: Yesu alikuwa na ndugu na dada!
Nilikuwa na maulizo mengine mengi. Sababu gani watoto wanakufa? Sababu gani mataifa yanapigana? Sababu gani watu hawasikilizane hata ikiwa wanazungumuza luga moja? Majibu niliyopata kutoka katika Biblia yalinipendeza sana. Nilijua kwamba mateso yanayowapata watu si mapenzi ya Mungu. Nilifurahi sana kujua kama nitaweza tena kuwaona watu niliopenda ambao walikufa katika vita mbalimbali. Hatua kwa hatua, nilianza kumuona Yehova kuwa ni mutu kwelikweli.
Siku moja, nilikuwa ninasimama mbele ya sanamu zangu, nikimuomba Mungu amusaidie mutoto wangu aliyekuwa ametoka tu kwenye vita huko Vietnam na aliyekuwa mwenye kushuka moyo sana. Mara moja, nilitambua kwamba sala zangu hazikupaswa kuelekezwa kwa sanamu, lakini zilipaswa kuelekezwa kwa Yehova, Mungu anayeishi. Nilitia sanamu hizo pembeni na nikaona kwamba zilikuwa vitu bure kabisa. Nilizinunua kwenye kanisa, lakini usiku huo nilizitupa.
Haikuwa vyepesi kwangu kuachana na kanisa ambamo nilikomalia. Lakini niliona mambo ambayo Biblia inafundisha kuwa ya maana zaidi kuliko kitu kingine chochote. Kisha mwaka mumoja, mimi, binti yangu, na bwana yangu tulienda kumutembelea padri Murusi wa kanisa la Ortodokse. Nilikuwa na buku ndogo ambamo niliandika maulizo juu ya habari za Biblia na maandiko yanayojibu maulizo hayo. Niliposoma maandiko ya Biblia kwa sauti, padri alitikisa kichwa na kusema “Umepotea.” Alituambia tusisubutu kurudia kwake tena.
Mambo yaliyotokea tulipokutana na padri yalimushangaza binti yetu Olya, aliyekuwa na akili nyingi na hamu ya kujua mambo mengi. Yeye pia alianza kuchunguza Biblia kwa uangalifu na kisha akaanza kuhuzuria mikutano ya Mashahidi wa Yehova pamoja na mimi. Nilibatizwa katika mwaka wa 1972, na Olya alibatizwa mwaka uliofuata.
Azimio la Familia Yetu
Azimio letu limekuwa, Kazia akili mambo ya sasa, sahau mambo ya zamani. Kwa hiyo, hatukusita kufanya jambo lolote jipya ikiwa tulisadikishwa kwamba ni jambo nzuri. Mimi na binti yangu tulipoanza kuwa na uhusiano pamoja na Mungu, tulikuwa na hamu kubwa ya kuwatembelea watu nyumbani kwao ili kuwaambia mambo tuliyokuwa tunajifunza. Ninakubali kwamba mwanzoni sikuwa na busara nilipokuwa nikizungumuza na watu katika mahubiri, na yule aliyehubiri pamoja na mimi alipaswa kueleza mambo kwa njia ya busara na upendo. Lakini baada ya muda, nilijifunza kuzungumuza na watu wa inchi na desturi mbalimbali ambao, kama vile mimi, walikuja Amerika kutafuta maisha mazuri zaidi.
Katika miaka iliyofuata, mara nyingi mimi na binti yangu tulisema kwamba ikiwa Pazia la Chuma linaondolewa, tungeenda katika inchi ya Russie ili kusaidia watu kujifunza juu ya Mungu. Pazia hilo lilipoondolewa mwanzoni mwa miaka ya 1990, Olya alitimiza ndoto hiyo kwa ajili ya sisi wawili. Alihamia Russie na kwa miaka 14 alikuwa muhudumu wa wakati wote huko. Alijifunza Biblia na watu wengi na aliweza kusaidia kutafsiri vichapo vya Kiingereza katika luga ya Kirusi kwenye Biro ya tawi ya Mashahidi wa Yehova ya Russie.
Sasa siwezi kutoka ndani ya kitanda, na watoto wangu wanafanya yote wanayoweza ili maisha yangu yawe mazuri. Ninamushukuru Mungu kwa sababu mwanzoni mwa miaka ya ugonjwa wangu, nilipata maisha mazuri zaidi. Nimeona utimizo wa maneno ya zaburi ya Biblia iliyoandikwa na muchungaji Daudi inayosema hivi: ‘Mungu ananiongoza kando ya mahali pa kupumuzika palipo na maji ya kutosha. Anaiburudisha nafsi yangu. Ananiongoza katika mapito ya uadilifu kwa ajili ya jina lake.’—Zaburi 23:2, 3.a
[Maelezo ya chini]
a Maria Kilin alikufa tarehe 1 Mwezi wa 3, 2010, wakati habari hii ya kwanza ya maisha yake ilikuwa ikitayarishwa ili itolewe.
[Picha zimetolewa na]
Picha iliyokamatwa na jeshi la États-Unis
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 13]
HABARI YENYE KUVUTIA
Mwishoni mwa mwaka wa 1954, Maria Kilin aliandika habari yenye kuvutia juu ya maisha yake huko Corée du Nord. Habari hiyo ilitafsiriwa katika Kiingereza na mufanyakazi Murusi aliyetumika katika biro inayowakilisha inchi ya Russie huko Australie na habari hiyo ikauzishiwa gazeti fulani la États-Unis. Ilichapishwa katika sehemu 12, kuanzia tarehe 16 mupaka 28, Mwezi wa 1, 1955.
Sehemu ya kwanza ilianza kwa maneno haya: “Mimi si muandikaji. Labda siweze kuandika vizuri habari ya maisha yangu. Lakini ninaweza kuiandika yote na ninaweza kuiandika kwa uhakika.” Na Maria alifanya hivyo. Habari iliyo hapa pembeni inazungumuzia kwa kifupi maisha ya Maria, na pia mabadiliko makubwa yaliyotokea miaka mingi kisha Maria kufika huko États-Unis.
[Picha]
Maandishi ya habari ya maisha yangu yaliyoandikwa kwa mukono na sehemu ya kwanza ya habari hiyo katika gazeti hilo
[Picha katika ukurasa wa 13]
Kijiji cha Shmakovka, Primorskiy Kray, katika Mashariki ya Mbali ya Russie, mahali nilipozaliwa
[Picha katika ukurasa wa 14]
Mimi na Ivan tulipofunga ndoa, mwaka wa 1941
[Picha katika ukurasa wa 14]
Mimi, bwana yangu, na wawili kati ya watoto wetu, mwaka wa 1954
[Picha zimetolewa na]
Picha iliyokamatwa na jeshi la États-Unis
[Picha katika ukurasa wa 15]
Katika bustani ya nyumba yangu huko Maryland, États-Unis, mwaka wa 1990 hivi