Watchtower—MAKTABA KU ENTERNETE
Watchtower
MAKTABA KU ENTERNETE
Kiswahili (Congo)
  • BIBLIA
  • VICHAPO
  • MIKUTANO
  • w13 15/6 uku. 17-21
  • Yehova Ni Mushikamanifu na Mwenye Kusamehe

Hakuna video juu ya habari yenye umechagua.

Pole, kulikuwa kosa fulani wakati video ilikuwa inajaribu kusoma.

  • Yehova Ni Mushikamanifu na Mwenye Kusamehe
  • Munara wa Mulinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2013
  • Vichwa Vidogo
  • Habari za Kufanana na Zile
  • YEHOVA NI MUSHIKAMANIFU
  • TUIGE USHIKAMANIFU WA YEHOVA
  • YEHOVA NI MWENYE KUSAMEHE
  • TUIGE SIFA YA YEHOVA YA KUSAMEHE
  • TUENDELEE KUPENDEZWA SANA NA SIFA ZA YEHOVA
  • Yehova Ni Mungu Mwenye Anasameheaka Sana
    Munara wa Mulinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Gazeti la Funzo)—2022
  • Musamaha wa Yehova Unakuletea Faida Gani
    Munara wa Mulinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Gazeti la Funzo)—2025
Munara wa Mulinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2013
w13 15/6 uku. 17-21
[Picha katika ukurasa wa 17]

Yehova Ni Mushikamanifu na Mwenye Kusamehe

‘Wewe, Ee Yehova, ni mwema na uko tayari kusamehe; na fazili zenye upendo ni nyingi kwa wale wote wanaokuitia.’​—ZAB. 86:5.

UNAWEZA KUELEZA?

  • Ni katika njia gani tunaweza kuiga ushikamanifu wa Yehova?

  • Namna gani tunaweza kuiga sifa ya Yehova ya kusamehe?

  • Sababu gani unataka kuendelea kupendezwa sana na sifa za Yehova?

1, 2. (a) Sababu gani tunapendezwa sana na marafiki walio washikamanifu na wanaosamehe? (b) Tutazungumuzia maulizo gani?

KWA maoni yako, rafiki wa kweli anapaswa kuwa mutu wa namna gani? Dada mumoja anayeitwa Ashley, anasema hivi: “Kwa maoni yangu, rafiki wa kweli ni mutu anayekutegemeza nyakati zote na anayekusamehe unapokosea.” Sisi wote tunapendezwa sana na rafiki walio washikamanifu na wanaosamehe. Rafiki hao wanatufanya tujisikie salama na wenye kupendwa.​—Met. 17:17.

2 Yehova ndiye rafiki yetu mushikamanifu na mwenye kusamehe kuliko rafiki zetu wote. Mutunga-zaburi alieleza jambo hilo hivi: ‘Wewe, Ee Yehova, ni mwema na uko tayari kusamehe; na fazili zenye upendo [ao upendo mushikamanifu] ni nyingi kwa wale wote wanaokuitia.’ (Zab. 86:5) Inamaanisha nini kuwa mushikamanifu na mwenye kusamehe? Namna gani Yehova anaonyesha sifa hizo nzuri? Na tunaweza kumuiga namna gani? Majibu ya maulizo hayo yatatusaidia tumupende zaidi rafiki yetu muzuri kuliko wote, Yehova. Pia, yatatia nguvu uhusiano wetu na ndugu na dada zetu.​—1 Yoh. 4:7, 8.

YEHOVA NI MUSHIKAMANIFU

3. Kuwa mushikamanifu kunamaanisha nini?

3 Ushikamanifu ni sifa nzuri inayotia ndani kujitoa, kuwa mwaminifu, na kutii kikamili. Mutu mushikamanifu si kigeugeu. Badala yake, anapenda sana mutu (ao kitu) fulani, anashikamana na mutu huyo (ao kitu hicho) hata katika hali ngumu. Kwa kweli, Yehova ndiye ‘mushikamanifu’ zaidi kuliko wote.​—Ufu. 16:5.

4, 5. (a) Namna gani Yehova anaonyesha ushikamanifu? (b) Namna gani kufikiria matendo ya ushikamanifu ya Mungu kunaweza kututia moyo?

4 Namna gani Yehova anaonyesha ushikamanifu? Yeye hawatupilie hata kidogo watumishi wake waaminifu. Mufalme Daudi alimusifu Yehova kwa sababu ya ushikamanifu wake. (Soma 2 Samweli 22:26.) Alipopambana na matatizo, Yehova hakumuacha, lakini alimuongoza, alimulinda, na alimukomboa. (2 Sam. 22:1) Daudi alijua kwamba Yehova haonyeshe ushikamanifu wake kwa maneno tu, lakini pia kwa matendo. Sababu gani Yehova alimutendea Daudi kwa ushikamanifu? Kwa sababu Daudi mwenyewe alikuwa ‘mutu mushikamanifu.’ Yehova anapendezwa sana na ushikamanifu wetu; na ikiwa tunataka awe mushikamanifu kwetu, sisi pia tunapaswa kuwa washikamanifu kwake.​—Met. 2:6-8.

5 Kufikiria matendo ya ushikamanifu ya Yehova kunaweza kututia moyo. Ndugu mumoja mwaminifu anayeitwa Reed alisema hivi: “Ninaposoma namna Yehova alivyomutegemeza Daudi wakati wa taabu, hilo linanisaidia kabisa. Hata alipokuwa akiishi ndani na inje ya mapango kwa sababu ya kumukimbia Mufalme Sauli, Yehova aliendelea kumutegemeza. Habari hiyo inanitia moyo sana! Na inanikumbusha kwamba hata hali iwe namna gani, hata ikiwa inaonekana kama hakuna tena tumaini, Yehova atanitegemeza ikiwa ninabaki mushikamanifu kwake.” Bila shaka, wewe pia unaamini hivyo.​—Rom. 8:38, 39.

6. Yehova anaonyesha ushikamanifu katika njia gani zingine, na hilo linawaletea watumishi wake faida gani?

6 Yehova anaonyesha ushikamanifu katika njia gani zingine? Habadili kanuni zake. Anatuhakikishia hivi: ‘Hata uzeeni mwa mutu mimi ni yuleyule.’ (Isa. 46:4) Siku zote maamuzi yake yanategemea kanuni zake zisizobadilika za mema na mabaya. (Mal. 3:6) Zaidi ya hilo, Yehova anaonyesha ushikamanifu wake kwa kutimiza ahadi yake. (Isa. 55:11) Kwa hiyo, waabudu wote waaminifu wa Yehova wanafaidika na ushikamanifu wake. Namna gani? Tunapojikaza kuishi kulingana na kanuni za Yehova, tuwe hakika kwamba atatimiza ahadi yake ya kutubariki.​—Isa. 48:17, 18.

TUIGE USHIKAMANIFU WA YEHOVA

7. Ni katika njia gani tunaweza kuiga ushikamanifu wa Mungu?

7 Namna gani tunaweza kuiga ushikamanifu wa Yehova? Njia moja ni kuwasaidia wale wanaopambana na hali ngumu. (Met. 3:27) Kwa mufano, je, unajua ndugu ao dada ambaye amevunjika moyo, labda kwa sababu ya magonjwa, kupingwa na watu wa familia, ao kwa sababu ya uzaifu wake mbalimbali? Sababu gani usichukue hatua ya kumutolea “maneno mema, maneno yenye kufariji?” (Zek. 1:13)a Ukifanya hivyo, utaonyesha kwamba wewe ni rafiki mushikamanifu na wa kweli, rafiki ‘anayeshikamana na mutu kwa ukaribu zaidi kuliko ndugu.’​—Met. 18:24.

8. Namna gani tunaweza kuiga ushikamanifu wa Yehova, kwa mufano katika ndoa?

8 Tunaweza pia kuiga ushikamanifu wa Yehova kwa kubaki waaminifu kwa wale tunaowapenda. Kwa mufano, ikiwa umeoa ao kuolewa, unajua kama unapaswa kubaki mwaminifu kwa bibi ao bwana yako. (Met. 5:15-18) Kwa hiyo, hautajaribu hata kidogo kufanya mambo yanayoweza kukuongoza kwenye uzinifu. (Mt. 5:28) Zaidi ya hayo, tunaonyesha kama tuko washikamanifu kwa ndugu na dada zetu kwa kutupilia mbali porojo ao kusingiziana, kwa kuepuka kueneza habari zisizojenga ao hata kuzisikiliza.​—Met. 12:18.

9, 10. (a) Tunataka kubaki washikamanifu kwa nani hasa? (b) Sababu gani si rahisi siku zote kutii amri za Yehova?

9 Zaidi ya yote, tunapenda kubaki washikamanifu kwa Yehova. Namna gani? Kwa kujikaza kuona mambo kama vile Yehova anavyoyaona, ni kusema, kupenda yale anayopenda na kuchukia yale anayochukia, na kisha kuishi kulingana na mapenzi yake. (Soma Zaburi 97:10.) Tukiendelea kujikaza ili mawazo yetu yapatane na mawazo ya Yehova, itakuwa rahisi kwetu kutii amri zake.—Zab. 119:104.

10 Ni kweli kwamba haitakuwa rahisi siku zote kutii amri za Yehova. Labda itaomba tufanye yote tunayoweza ili kubaki washikamanifu. Wakristo fulani waseja wangependa kuoa ao kuolewa, lakini hawajapata ndugu ao dada anayewafaa katika kutaniko. (1 Kor. 7:39) Dada ambaye hajaolewa anaweza kuvumbua kwamba wafanyakazi wenzake wasiokuwa mashahidi wanamuchochea afunge ndoa na mufanyakazi mwengine asiyekuwa shahidi. Labda dada huyo anapambana na jaribu la kukosa bwana. Lakini, anajikaza sana kubaki mushikamanifu kwa Yehova. Je, hatupendezwe sana kabisa na mifano mizuri ya ushikamanifu kama hiyo? Bila shaka, Yehova atawabariki wale wote wanaobaki waaminifu kwake ijapokuwa majaribu.​—Ebr. 11:6.

[Picha katika ukurasa wa 19]

‘Yuko rafiki anayeshikamana na mutu kwa ukaribu zaidi kuliko ndugu.’​—Met. 18:24 (Ona fungu la 7)

‘Musameheane kwa hiari.’​—Efe. 4:32 (Ona fungu la 16)

YEHOVA NI MWENYE KUSAMEHE

11. Kuwa mwenye kusamehe kunamaanisha nini?

11 Yehova ni Mungu aliye tayari kusamehe. Hiyo ni moja kati ya sifa zake zenye kuvutia sana. Kuwa mwenye kusamehe kunamaanisha nini? Kwa kweli, sifa hiyo inahusisha kumuhurumia mutu aliyekukosea ikiwa kuna sababu nzuri ya kufanya hivyo. Mutu mwenye kusamehe hafunge macho juu ya kosa ao kupunguza uzito wa kosa hilo. Lakini anaepuka kuweka kinyongo. Biblia inafundisha kwamba Yehova iko “tayari kusamehe” wale wanaotubu kikweli.​—Zab. 86:5.

12. (a) Yehova anasamehe namna gani? (b) Mutume Petro alimaanisha nini aliposema kwamba zambi za mutu zinaweza ‘kuvutwa’?

12 Namna gani Yehova anaonyesha sifa ya kusamehe? Anaposamehe, anafanya hivyo “kwa njia kubwa”; anasamehe kabisa na kusahau. (Isa. 55:7) Tunajua namna gani kwamba Yehova anasamehe kabisa? Fikiria uhakikisho anaotutolea katika andiko la Matendo 3:19. (Soma.) Mutume Petro alitia moyo wasikilizaji wake ‘watubu na wageuke.’ Wakati mutenda-zambi anatubu kikweli, anahuzunika sana kuhusu makosa aliyofanya, na anaazimia kutoyarudilia tena. (2 Kor. 7:10, 11) Tena, toba ya kweli inamuchochea ‘kugeuka,’ ni kusema, kuacha mwenendo wake muchafu na kufuata njia inayomupendeza Mungu. Ikiwa wasikilizaji wa Petro wangeonyesha toba hiyo ya kweli, matokeo yangekuwa nini? Petro alisema kama zambi zao ‘zingevutwa.’ Neno hilo linatokana na neno la Kigiriki linalomaanisha “kupanguza ao kuondoa.” Kwa hiyo, Yehova anaposamehe, ni kama vile anachukua kitambaa na kusafisha ubao. Anasamehe kabisa.​—Ebr. 10:22; 1 Yoh. 1:7.

13. Yehova anatuhakikishia nini anaposema, ‘zambi yao sitaikumbuka tena’?

13 Namna gani tunajua kama Yehova anasamehe na kusahau? Tufikirie unabii wa Yeremia kuhusu agano jipya, ambalo Yehova alifanya na Wakristo watiwa-mafuta, agano linalofanya iwezekane kwa wale walio na imani katika zabihu ya ukombozi wapate musamaha wa kweli. (Soma Yeremia 31:34.) Yehova anasema hivi: ‘Nitalisamehe kosa lao, na zambi yao sitaikumbuka tena.’ Kwa hiyo, Yehova anatuhakikishia kwamba anaposamehe, hawezi tena kututendea kulingana na makosa tuliyofanya zamani. Haendelee tena kufikiria zambi zetu ili kutushitaki ao kutuazibu tena na tena. Lakini, Yehova anasamehe zambi hizo na kusahau.​—Rom. 4:7, 8.

14. Namna gani tunaweza kufarijiwa tunapotafakari kuhusu sifa ya Yehova ya kusamehe? Toa mufano.

14 Kutafakari kuhusu sifa ya Yehova ya kusamehe kunaweza kutufariji. Fikiria mufano huu. Miaka fulani iliyopita, dada mumoja tutakayemwita Elaine alitengwa na kutaniko. Kisha miaka mingi, alirudishwa katika kutaniko. Dada Elaine anasema hivi: “Ijapokuwa nilifikiri na kuambia wengine kwamba Yehova alinisamehe, siku zote nilijisikia kwa kiasi fulani kwamba alikuwa mbali nami ao kwamba wengine walikuwa karibu zaidi naye na kwamba Mungu alikuwa halisi zaidi kwao.” Lakini, dada Elaine alifarijiwa aliposoma na kutafakari mifano fulani ya Biblia inayozungumuzia sifa ya Yehova ya kusamehe. Dada Elaine anasema hivi: “Nilitambua kwamba Yehova ananipenda na ananihangaikia kwa njia ambayo nilikuwa bado sijawazia.” Elaine alichochewa hasa na wazo hili: “Yehova anaposamehe zambi zetu, hatupaswe kufikiri kwamba tutabaki na alama ya zambi hiyo maisha yetu yote.”b Elaine anasema hivi: “Nilikuwa nikifikiri kama Yehova hangenisamehe kabisa, na nilifikiri kama nitabeba muzigo huo maisha yangu yote. Najua kama itachukua wakati, lakini nimeanza kusikia kama ninaweza kabisa kumukaribia Yehova, na ninajisikia kama sibebe tena muzigo huo.” Tuna pendeleo kabisa la kumutumikia Mungu mwenye upendo na mwenye kusamehe!​—Zab. 103:9.

TUIGE SIFA YA YEHOVA YA KUSAMEHE

15. Namna gani tunaweza kuiga sifa ya Yehova ya kusamehe?

15 Tunaweza kuiga sifa ya Yehova ya kusamehe kwa kusameheana wakati wowote ambapo tuna sababu nzuri ya kufanya hivyo. (Soma Luka 17:3, 4.) Kumbuka kwamba wakati Yehova anasamehe, anasahau zambi zetu katika maana ya kwamba haendelee kuzifikiria ili kutushitaki ao kutupatia malipizi. Tunapowasamehe wengine, sisi pia tunaweza kusahau kwa kuacha kufikiria-fikiria makosa waliyotutendea na kuepuka kuwakumbusha tena makosa hayo.

16. (a) Je, kuwasamehe wengine kunamaanisha kufunga macho juu ya makosa yao ao kuwaruhusu watutendee kwa namna isiyofaa? Eleza. (b) Ikiwa tunapenda Mungu atusamehe, tunapaswa kufanya nini?

16 Kuwa mwenye kusamehe hakumaanishe kama tutafunga macho juu ya makosa wala kuwaruhusu wengine watutendee kwa namna isiyofaa, kunamaanisha tu kwamba hatutaweka kinyongo. Lakini, tusisahau kwamba ili kusamehewa na Mungu, tunapaswa pia kuiga sifa yake ya kusamehe katika uhusiano wetu na wengine. (Mt. 6:14, 15) Kwa vyovyote, Yehova anatuelewa, na hilo linamufanya akumbuke kama “sisi ni mavumbi.” (Zab. 103:14) Kwa hiyo basi, je, kuelewa wengine hakupaswe kutuchochea kuvumilia uzaifu wao na kuwa tayari kuwasamehe kikweli?​—Efe. 4:32; Kol. 3:13.

[Picha katika ukurasa wa 21]

Sala zetu za kuomba musamaha zinapaswa kutoka moyoni (Ona fungu la 17)

17. Ni jambo gani linaloweza kutusaidia ikiwa ndugu ao dada yetu ametuumiza?

17 Bila shaka, si rahisi kusamehe. Inaonekana kama hata Wakristo watiwa-mafuta wa wakati wa mitume walishindwa kumaliza matatizo yao. (Flp. 4:2) Ikiwa ndugu ao dada yetu ametuumiza, ni jambo gani linaloweza kutusaidia? Kumbuka Ayubu. Aliumizwa sana wakati “marafiki” zake​—Elifazi, Bildadi na Sofari​—walimushitaki kwa uongo. (Ayu. 10:1; 19:2) Mwishowe, Yehova aliwakaripia washitaki hao wa uongo. Mungu aliwaambia waende kwa Ayubu na watoe zabihu kwa ajili ya zambi zao. (Ayu. 42:7-9) Lakini, Yehova pia alimuomba Ayubu afanye jambo fulani. Jambo gani hilo? Yehova alimwomba Ayubu asali kwa ajili ya washitaki hao. Ayubu alitenda kama Yehova alivyomwamuru, na Yehova alimubariki kwa sababu alikuwa na roho ya kusamehe wengine. (Soma Ayubu 42:10, 12, 16, 17.) Tunapata somo gani? Kusali kwa ajili ya mutu aliyetukosea kunaweza kutusaidia tusiweke kinyongo.

TUENDELEE KUPENDEZWA SANA NA SIFA ZA YEHOVA

18, 19. Namna gani tunaweza kuendelea kupendezwa sana na sifa zenye kuvutia za Yehova?

18 Bila shaka tumefurahia kuzungumuzia sifa fulani zenye kuvutia za Yehova. Tumejifunza kwamba yeye ni mwenye kukaribiwa kwa urahisi, hana ubaguzi, ni mukarimu, mwenye usawaziko, mushikamanifu, na mwenye kusamehe. Lakini, tumejifunza tu mambo machache kumuhusu Yehova. Tutakapopata uzima wa milele, tutafurahia kuendelea kujifunza mengi kumuhusu. (Mhu. 3:11) Bila shaka, tunakubaliana na maneno ya mutume Paulo, aliyeandika hivi: “Lo! Jinsi kilivyo kina cha utajiri wa Mungu na hekima na ujuzi!” Tunaweza kusema vivyo hivyo kuhusu sifa yake ya upendo na sifa zingine sita ambazo tumezungumuzia.​—Rom. 11:33.

19 Wengi kati yetu wanaendelea kupendezwa sana na sifa zenye kuvutia za Yehova. Ili kusamini sana sifa za Yehova, tunapaswa kuzijua, kufikiri sana juu ya sifa hizo, na kuzionyesha katika maisha yetu. (Efe. 5:1) Tunapofanya hivyo, tutaona kwamba maneno haya ya mutunga​-zaburi ni ya kweli: ‘Lakini mimi, kumukaribia Mungu ni kwema kwangu.’​—Zab. 73:28.

a Ili kupata mapendekezo yatakayokusaidia, soma habari “Je, Umetia Moyo Yeyote Karibuni?” katika Munara wa Mulinzi wa tarehe 15 Mwezi wa 1, 1995 na “Kuchochea Kwenye Upendo na Kazi Zilizo Bora​—Jinsi gani?” katika Munara wa Mulinzi wa tarehe 1 Mwezi wa 4, 1995.

b Soma kitabu Mkaribie Yehova, sura ya 26 fungu la 10.

    Vichapo vya Swahili (Congo) (1996-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili (Congo)
    • Tumia Wengine
    • Préférences
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Kanuni za Matumizi
    • Kanuni za Kutunza Siri
    • Paramètres Kuhusu Kutunza Siri
    • JW.ORG
    • Ingia
    Tumia Wengine