Watchtower—MAKTABA KU ENTERNETE
Watchtower
MAKTABA KU ENTERNETE
Kiswahili (Congo)
  • BIBLIA
  • VICHAPO
  • MIKUTANO
  • w14 15/6 uku. 8-11
  • Namna ya Kusaidia Ndugu na Dada Ambao Ndoa Zao Zimevunjika

Hakuna video juu ya habari yenye umechagua.

Pole, kulikuwa kosa fulani wakati video ilikuwa inajaribu kusoma.

  • Namna ya Kusaidia Ndugu na Dada Ambao Ndoa Zao Zimevunjika
  • Munara wa Mulinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2014
  • Vichwa Vidogo
  • Habari za Kufanana na Zile
  • KUJISIKIA MWENYE KUVURUGIKA
  • KUJIKAZA ILI KUPATA NGUVU TENA
  • KUJISIKIA KUWA PEKEE NA MWENYE KUKATALIWA
  • Kuendelea na Maisha Kisha Ndoa Kuvunjika
    Munara wa Mulinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2013
Munara wa Mulinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2014
w14 15/6 uku. 8-11

Namna ya Kusaidia Ndugu na Dada Ambao Ndoa Zao Zimevunjika

Mwanamuke anayemufariji dada ambaye ndoa yake ilivunjika

Pengine unajua mutu fulani ao watu wengi ambao ndoa zao zimevunjika. Ni hivyo kwa sababu limekuwa jambo la kawaida kuvunja ndoa. Kwa mufano, utafiti uliofanywa katika inchi ya Polandi unaonyesha kwamba watu walio na miaka 30 ambao wameoana kumepita tatu mupaka sita wanaelekea kuvunja ndoa; si hao tu ndio walio katika hali hiyo.

Shirika la Mambo ya Familia la Hispania, linasema hivi: “Hesabu zinaonyesha kwamba katika Ulaya nusu ya watu ambao wameoana watavunja ndoa zao.” Katika inchi nyingine tajiri, mambo yako hivyohivyo.

KUJISIKIA MWENYE KUVURUGIKA

Ni jambo gani linalohusika katika hali hiyo inayotokea kwa ukawaida? Mushauri mumoja mwenye uzoefu wa mambo ya familia katika Ulaya Mashariki alisema hivi: “Kuvunja ndoa kunaonyesha waziwazi jambo ambalo lilikuwa tayari limetokea—kuvunjika kwa uhusiano na kutengana, jambo lenye kumuumiza sana moyoni.” Aliongezea hivi: “Kisha ndoa kuvunjika, kuna hali ya huzuni nyingi inayoumiza sana moyoni, hasira, kujuta, kuvunjika moyo, kukosa tumaini na kusikia haya.” Wakati fulani, hali hiyo inaweza kuleta mawazo ya kutaka kujiua. “Wakati tribinale inakubali kuvunjika kwa ndoa, hatua ingine inaanza. Kila wakati mutu anajisikia kuwa amebakia peke yake na kutengwa na wengine. Yeye anaweza kujiuliza hivi: ‘Sasa ndoa yangu imevunjika, ninakuwa nani sasa? Maisha yangu yana kusudi gani?’”

Wakati anakumbuka namna alivyojisikia katika miaka iliyopita, Ewa anasema hivi: “Nilisikia haya sana wakati ndoa yetu ilivunjika, majirani wangu na wafanya kazi wenzangu waliniita ‘mutu ambaye ndoa yake imevunjika.’ Nilisikia hasira sana. Nilibaki na watoto wangu wawili na kulazimishwa kuwa baba na mama yao.”a Adam, aliyekuwa muzee wa kutaniko mwenye kuheshimiwa kwa muda wa miaka 12, anasema hivi: “Nilipoteza sana heshima yangu mwenyewe na wakati fulani nilisikia hasira sana, na nilipenda kujitenga na kila mutu.”

KUJIKAZA ILI KUPATA NGUVU TENA

Wanapoendelea kusumbuka kwa sababu ya huzuni, watu fulani ambao ndoa zao zimevunjika, wamejikaza kupata tena nguvu hata kisha miaka mingi kupita. Wanaweza kuona kwamba wengine hawawahangaikie. Zaidi ya hilo, mwandishi mumoja wa habari alisema kwamba wanapaswa sasa “kubadili tabia zao na kujifunza wenyewe namna ya kupambana na matatizo yao.”

Stanisław anasema hivi: “Ndoa yetu ilipovunjika, bibi yangu wa zamani alinizuia ao alikataa niwaone binti zangu wawili wadogo. Hilo lilifanya nijisikie kuwa hakuna hata mutu mumoja aliyenihangaikia na kuwaza kwamba pengine Yehova pia alikuwa ameniacha. Sikuwa tena na hamu ya kuishi. Kisha muda fulani, nilitambua kwamba nilikuwa nimeingiwa na mawazo mabaya sana.” Pia, Wanda ambaye ndoa yake ilikuwa imevunjika alikuwa na wasiwasi alipofikiria maisha yake ya wakati ujao. Alisema hivi: “Nilifikiri kabisa kwamba muda mufupi kisha ndoa yangu kuvunjika, watu kutia ndani Mashahidi wenzangu, hawangenihangaikia hata kidogo mimi na watoto wangu. Hata hivyo, sasa ninaweza kuona kwamba ndugu walitutegemeza sana na kunisaidia nilipoendelea kujaribu kuwalea watoto wangu ili wamutumikie Yehova.”

Maneno hayo yanaweza kukusaidia uelewe kwamba kisha ndoa kuvunjika watu fulani wanasumbuliwa na maoni yasiyofaa. Wanaweza kujiona kuwa wana sifa mbaya, kwamba hawafae kitu hata kidogo na hawastahili kuhangaikiwa. Tena, wanaweza kuanza kusema vibaya juu ya ndugu na dada walio karibu yao. Kwa hiyo, wanaweza kuanza kufikiri kwamba ndugu na dada katika kutaniko hawana upendo na hawawahangaikie. Lakini, mufano wa Stanisław na Wanda unaonyesha kwamba ndugu na dada fulani ambao ndoa zao zimevunjika wanaweza kufikia kutambua kwamba ndugu na dada zao wanawahangaikia kabisa. Bila shaka, Wakristo wenzao wamewahangaikia kwa njia ya pekee, hata kama musaada ambao walitoa haukupokewa vizuri hapo mbele.

KUJISIKIA KUWA PEKEE NA MWENYE KUKATALIWA

Kumbuka kwamba hata kama tunajikaza kusaidia ndugu na dada ambao ndoa zao zimevunjika, wanaweza kujisikia mara kwa mara kuwa peke yao. Zaidi sana dada ambao ndoa zao zimevunjika wanaweza kufikiri kwamba ni watu wachache tu ndio wanawahangaikia. Alicja anasema hivi: “Kumepita miaka munane kisha ndoa yangu kuvunjika. Lakini, ningali ninajisikia kuwa mutu wa bure wakati fulani. Ninapojisikia hivyo, nina amua kujitenga na wengine na kuanza kulia na kuhuzunika.”

Hata kama ndugu na dada fulani ambao ndoa zao zimevunjika hawajisikie hivyo, Biblia inawashauria waepuke kujitenga na wengine. Ikiwa hawafuate shauri hilo, wanaweza kukataa “hekima inayotumika.” (Met. 18:1) Hata hivyo, yule anayejisikia kuwa peke yake, anapaswa kutenda kwa hekima kwa kuepuka kutafuta kila mara shauri ao faraja kwa mutu fulani wa jinsia tofauti. Kufanya hivyo kutamusaidia asianze kuvutiwa kimapenzi na mutu huyo asiyekuwa bibi ao bwana yake.

Ndugu na dada zetu ambao ndoa zao zimevunjika wanaweza kupatwa na matatizo mengi ya moyoni kama vile kuwa na wasiwasi kuhusu wakati wao ujao, kujisikia kuwa peke yao, ao kutengwa na wengine. Tunapoelewa kwamba ni kawaida kujisikia hivyo na wakati huohuo pia ni vigumu kupambana na hali hiyo, tunapaswa kumuiga Yehova kwa kuwategemeza kwa uaminifu ndugu na dada hao. (Zab. 55:22; 1 Pet. 5:6, 7) Tunaweza kuwa hakika kwamba watapendezwa sana na musaada wowote ambao tutawatolea. Bila shaka, watapata marafiki wazuri katika kutaniko wanaoweza kuwasaidia!—Met. 17:17; 18:24.

a Majina fulani yamebadilishwa.

Maoni Yenye Kufaa Kuhusu Kuvunja Ndoa

Sisi watumishi wa Yehova tunaheshimu ndoa sana. Tunafanya hivyo kwa sababu mawazo yetu yanategemea yale ambao Maandiko yanasema kuhusu ndoa. Kwa mufano, kwenye Malaki 2:16, tunasoma maneno ya Mungu yanayosema hivi: “[Mungu] Anachukia talaka [ao kuvunja ndoa].” Sababu moja ya Maandiko inayoweza kufanya ndoa ivunjike ni kama bibi ao bwana anafanya uzinifu. Kwa hiyo, ni kosa kubwa kabisa mutu kuanza kuwa na mawazo ya kuvunja ndoa bila sababu ya maandiko pengine ukiwa tayari unafikiria kuoa ao kuolewa na mutu mwengine.—Mwa. 2:22-24; Kum. 5:21; Mt. 19:4-6, 9.

Lakini ndoa inapovunjika, kwa sababu Mukristo mumoja amekosa uaminifu, ndugu na dada katika kutaniko wanategemeza yule anayeumizwa. Wanamuiga Yehova kwa kufanya yote wanayoweza ili kusaidia watumishi waaminifu hao “waliopondwa roho.”—Zab. 34:15, 18; Isa. 41:10.

UNAWEZA KUTOA MUSAADA FULANI?

Unaweza kumutegemeza kabisa yule anayehitaji musaada? Unaweza kufanya nini ili kusaidia mutu fulani anayejisikia kama wale wanaozungumuziwa mwanzoni mwa habari hii? Chunguza yale ambayo Biblia inasema, na uone namna gani Wakristo fulani waaminifu wametoa musaada unaofaa. •

Sikiliza kwa uangalifu. (Met. 16:20, 23)

Jua kwamba kisha ndoa kuvunjika, mutu hawezi kufurahia kueleza mambo yote yaliyofanya ndoa yake ivunjike. Na ukweli ni kwamba kumukaza mutu aseme hakuwezi kuwa na matokeo mazuri na hakuwezi kupunguza mahangaiko yake. (Met. 12:25; Rom. 12:15) Michał, aliyemusaidia Adam kwa muda murefu, anaonyesha kwamba unaweza kujitia pa nafasi ya mutu huyo, kumusikiliza kwa uangalifu bila kukazia kila jambo analosema. Michał anasema hivi: “Nilijikaza kumusaidia Adam aelewe kwamba wakati anakuwa zaifu kwa sababu ya kujisikia vibaya moyoni, bila kufikiri anaweza kusema jambo fulani ambalo atahuzunikia baadaye.” Kwa hiyo Michał alimuambia Adam waziwazi kwamba hakutafuta kujua kila jambo. Lakini, alisikiliza kama rafiki wa kweli. Tunaweza kupata wakati wa kutosha ili kuzungumuza nao hata mbele ao kisha mikutano ya Kikristo kwa kusema tu maneno rahisi kama haya: “Namna gani sasa? Inaonekana kwamba una shida fulani siku hizi. Ninaweza kukusaidia.”

Onyesha mutu kwamba unamuhangaikia. (Flp. 2:4)

Mirosław anasema hivi: “Mimi na bibi yangu tulipanga programu ya kusaidia dada ambaye ndoa yake imevunjika. Kwa mufano, tulitengeneza kufuli ya mulango wake, tulimupeleka pia kwa muganga.” Mambo hayo yanaonekana kuwa madogo; lakini yalikuwa ya lazima, na yalimusaidia. Dada huyo ambaye Mirosław na bibi yake walisaidia alipata nguvu pole kwa pole. Zaidi ya hilo, baadaye alianza kazi ya upainia na binti yake aliyekuwa na miaka 11 alibatizwa.

Bibi na bwana wanaohangaikia dada ambaye ndoa yake ilivunjika

Wahakikishie ndugu na dada ambao ndoa zao zimevunjika kwamba Yehova anaelewa hali yao.

Ikiwa ndugu ao dada anajisikia kuwa hafae kitu, unaweza kumuhakikishia kwamba Mungu anapendezwa sana na kila mutumishi wake. Bila shaka, sisi ni “bora kuliko shomoro wengi”; sisi ni tofauti na viumbe vingine na wenye maana sana machoni pake. (Mt. 10:29-31) Kwa kuwa ‘Yehova ndiye muchunguzaji wa mioyo,’ anaweza kuwaelewa wale ambao ndoa zao zilivunjika. Hatamuacha mutumishi wake mwaminifu hata mumoja. (Met. 17:3; Zab. 145:18; Ebr. 13:5) Unapomuonyesha kwamba unamuhangaikia, muhakikishie kwamba Mungu anapendezwa naye kwa sababu anapenda kweli na anafanya yote anayoweza ili kutegemeza ibada ya kweli.—Flp. 2:29.

Umutie moyo ndugu ao dada ambaye ndoa yake imevunjika abakie karibu na kutaniko.

Wanaposumbuliwa na mawazo mbalimbali yasiyofaa, wamoja kati ya ndugu na dada hao wanashindwa kukusanyika. Lakini mikutano inatutia nguvu na kututia moyo, ao ‘kutujenga.’ (1 Kor. 14:26; Zab. 122:1) Kuhusu jambo hilo, wazee wanapaswa kuwatembelea na kuwatia moyo. Wanda, ambaye tulizungumuzia hapo mbele, anasema hivi: “Tunaendelea kukumbuka namna wazee walituhangaikia kwa upendo.”

Umutie moyo ndugu na dada ambaye ndoa yake imevunjika atie nguvu uhusiano wake pamoja na Mungu kupitia sala, funzo la pekee, na kutafakari. (Yak. 4:8)

Hata ikiwa Yehova ni mweza-yote na anaishi mbinguni, yeye anahangaikia sana “yeye anayeteseka na kujuta rohoni na kutetemeka kwa ajili ya neno [Lake].” Uwahakikishie ndugu na dada ambao ndoa zao zimevunjika jambo hilo, na kuwaonyesha namna gani sala na funzo la pekee limesaidia kila mumoja wetu kumukaribia sana Mungu.—Isa. 66:2.

Ufanye mupango wa kuhubiri ao kutayarisha mikutano pamoja naye.

Ndugu wawili wanaohubiri pamoja

Kufanya hivyo kutasaidia ndugu na dada ambaye ndoa yake imevunjika ajisikie kuwa na nguvu anapoendelea kupambana na hali hiyo. Marta, ambaye alimutegemeza dada mumoja aliyekuwa na bidii lakini aliyeregea kisha ndoa yake kuvunjika, anasema hivi: “Mara nyingi tulihubiri pamoja naye. Tulifurahi tulipoona kwamba tumefikia miradi fulani ambayo tujiwekea sisi wenyewe. Wakati fulani tulitayarisha mikutano pamoja, na wakati fulani kisha kufanya hivyo, tulipika chakula kitamu.”

    Vichapo vya Swahili (Congo) (1996-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili (Congo)
    • Tumia Wengine
    • Préférences
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Kanuni za Matumizi
    • Kanuni za Kutunza Siri
    • Paramètres Kuhusu Kutunza Siri
    • JW.ORG
    • Ingia
    Tumia Wengine